Advertisements

Friday, November 11, 2016

AFYA: FURSA YA KUJUA TEZI DUME NI NINI, SOMA HAPA


Viungo vya uzazi vya mwanaume vimegawanyika katika sehemu kuu mbili. Kuna viungo vya uzazi vya nje na vile vya ndani.
Viungo vya uzazi vya nje ni vile tunavyoviona kama uume na mfuko wa korodani.
Viungo vya uzazi vya ndani ni mirija ya mbegu za kiume ambacho ni kifuko cha akiba cha mbegu na tezi dume au tezi ya ‘Prostate’.
Viungo hivi vyote vina umuhimu mkubwa kwa mwanaume katika kumfanikisha kuweza kufanya tendo la ndoa kwa ufanisi pamoja na uzalishaji wa mbegu za kiume.Matatizo yakitokea katika sehemu yoyote hapo humuathiri mwanaume inategemea wapi athari ipo.
Athari ni kushindwa kufanya tendo la kujamiiana na kuzalisha mbegu au manii. Manii ni majimaji yanayolisha mbegu za kiume na kuzisafisha na huzalishwa na tezi dume.
Chanzo cha tatizo
Hutegemea mahali linapoathirika. Matatizo hutokea popote katika viungo vya uzazi vya mwanaume iwe nje au ndani.

Uume
Matatizo kwenye uume ni kupata maumivu katika njia ya mkojo kutokana na maambukizi au kuumia njia ya mkojo.Mwanaume mwenye tatizo hili hulalamika maumivu wakati wa kukojo, muwasho katika njia ya mkojo na mkojo kutotoka vizuri.

Kuumia kutokana na kuingiziwa mrija wa mkojo mara kwa mara katika njia ya mkojo.
Maambukizi inaweza kuwa Yutiai za mara kwa mara na magonjwa ya zinaa kama kisonono na mengine.

Ugonjwa wa kaswende huathiri sehemu ya nje ya uume zaidi ambapo vipele na vidonda vyenye muwasho na maumivu hujitokeza mara kwa mara.Tatizo hili hujitokeza kama tulivyoelezea hapo juu na huchunguzwa katika vituo vya afya.
Ni vema kuwahi hospitali endapo utahisi dalili hizo kwani ukichelewa itasababisha madhara makubwa mojawapo ni kuziba kwa njia ya mkojo, kusambaa kwa maambukizi katika viungo vingine kama kibofu cha mkojo, korodani na tezi dume.

Athari nyingine ni ugumba kwa mwanaume.

Tezi dume
Tezi dume ipo kwa ndani jirani na kibofu cha mkojo na mfuko wa haja kubwa. Kazi ya tezi hii ni kutengeneza na kutunza manii.Tezi dume hupatwa na matatizo mbalimbali kama maambukizi na kutanuka hadi kuwa saratani.

Kutanuka huanzia katika umri wa miaka arobaini na tano na huanza taratibu sana.
Maambukizi ya tezi dume hutokana na muendelezo wa maambukizi toka katika njia ya mkojo hadi kwenye kibofu cha mkojo na kufika kwenye tezi dume.

Tezi dume ikitanuka huanza dalili za uhafifu katika utoaji wa mkojo ambapo mkojo hautoki vizuri au unashindwa kabisa kutoka. Tezi hii inapotanuka inabana shingo ya kibofu cha mkojo.
Dalili dhahiri za ugonjwa huu hujitokeza kadiri umri unavyoongezeka, hasa zaidi ya miaka hamsini na sitini.

Endapo utachelewa kupata tiba hadi umri wa zaidi ya miaka sitini, kuna hatari ya tezi hiyo kuwa kansa au saratani.Uchunguzi wa awali wa tezi dume hufanyika kawaida katika kliniki kubwa kwenye hospitali za mikoa na wilaya kabla dalili hazijajitokeza rasmi.
Kuwa na tabia ya kufanya uchunguzi mara kwa mara hasa unapofikia umri wa miaka 45 na zaidi. 
Kadiri umri unavyoongezeka ndipo dalili zinapojitokeza taratibu hadi tatizo linakuwa kubwa.
Endapo utawahi kufanyiwa uchunguzi mapema , basi tezi dume inaweza kutibika au kuzuia isitanuke na ukaepuka upasuaji na saratani.

No comments: