Advertisements

Thursday, November 17, 2016

RC MAKONDA AUMBULIWA NA WAZIRI MKUU MBELE YA KAMANDA SIRRO

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema atamwajibisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda iwapo hatasimamia ipasavyo kukomesha matumizi ya dawa za kulevya, aina ya shisha.

Hatua hiyo inatokana na kauli ya Makonda kuwatuhumu Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna wa Polisi Simon Sirro na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Kamishna Msaidizi Suzan Kaganda, kulegalega kusimamia suala hilo huku akihofia wanaweza kuwa wamehongwa na watu waliotaka kumhonga lakini akakataa.

Waziri Mkuu Majaliwa alisema hayo jana wakati wa uzinduzi wa Mradi wa Uboreshaji wa Miundombinu ya Umeme katika Jiji la Dar es Salaam.

Alisema katika udhibiti wa suala la shisha, mkuu huyo wa mkoa amefanya kazi nzuri, na kwamba kwa kuwa ameshatoa maelekezo, akiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, Makonda hana budi kuyatekeleza.


Alisema alivyosikia anawaagiza wakuu wake wa wilaya wote kusimamia maagizo yake na kama hawakusimamia atachukua hatua, basi naye atachukua hatua kwake (Makonda) asipotekeleza suala hilo ambalo kwa Mkoa wa Dar es Salaam ni tatizo kubwa.

“Sasa mimi nasema nakuagiza wewe usimamie na kama hutasimamia suala hilo nitakuchukulia hatua, hivyo hangaika na shisha kwa wanaopuliza wakiwa wamelala hakikisha unawadhibiti,” alisema Waziri Mkuu Majaliwa wakati akijibu sehemu ya salamu za Makonda alipopewa fursa ya kusalimia wananchi katika hafla hiyo.

Katika salamu zake, Makonda alisema Waziri Mkuu alipiga marufuku matumizi ya shisha, hivyo alimwagiza Kamanda Sirro kuhakikisha suala hilo linatekelezwa kwa kiwango kikubwa.

“Lakini Waziri Mkuu nimeshangaa kupita katika baadhi ya maeneo na kuona watu wameanza tena kuvuta shisha na nilipouliza wakasema wewe ndiyo umetoa kibali cha shisha,” alieleza Makonda na kuongeza alishangaa Waziri Mkuu alipiga marufuku shisha, ni lini ametoa kibali kuanza kutumika.

Lakini mkuu huyo wa mkoa alienda mbali zaidi na kudai kuna kikundi cha watu 10 waliokwenda kwake ambao anawatambua kama “maajenti wa shetani” ambao wanapata faida kati ya Sh milioni 35 mpaka Sh milioni 45 kwa mwezi kutokana na dawa hizo za kulevya.

Alidai watu hao walipanga mikakati ya kumshawishi kupokea Sh milioni tano kwa kila mmoja kwa mwezi yaani Sh milioni 50 ili asipige kelele kuhusu shisha na wao waendelee kupata faida. 

“Shisha imerudi katika Mkoa wa Dar es Salaam na nimeshamuagiza Kamishna Sirro, lakini nimeona kama ana kigugumizi… lakini sijajua kama hizi tano tano zimepita kwake na pia RPC wa Kinondoni nimemuona hapa, lakini hawa wana kigugumizi sijui kama hizi tano tano zimepita kwao,” alisema Makonda.

Alisema aliamua kufanya ziara mwenyewe na kushuhudia watoto wadogo wanavuta shisha, hivyo uwezekano miaka 10 ijayo vijana wengi kuwa matatizo ya afya, hivyo kumwomba Waziri Mkuu kutochoka kusimamia suala hilo na taasisi zote ili likome katika mikoa yote.

Kuhusu wafanyabiashara wadogo, alisema suala hilo linamnyima usingizi na kutoa rai kwa wakuu wa wilaya kuwa, kama kuna mkuu wa wilaya atachelewa kutekeleza yale aliyoagiza kuwapeleka machinga katika maeneo yaliyoruhusiwa atachukua hatua kabla ya Waziri Mkuu kufanya hivyo.

Aidha, alishukuru kwa mradi wa umeme akisema ukatikaji umeme una madhara sana na hasa kwa wajasiriamali wadogo wanaojishughulisha na biashara ndogo kama saluni na shughuli nyingine ndogo zinazojenga uchumi wa kati.

CHANZO: HabariLeo

2 comments:

Anonymous said...

Makonda sidhani kama anaweza kuchaguliwa kwa kura na wananchi hata ujumbe wa nyumba kumi. Baada ya magufuli huyu jamaa hata pata hata ukatibu kata, sioni kama amesoma, hana busara, utoto na ulimbukeni.

Anonymous said...

Kinachonishangaza ni namna ambavyo Makonda ana survive kutumbuliwa, maana hata kama ni on job training hii sasa too much.