Advertisements

Friday, July 7, 2017

Hakimu kesi ya Lema ajitoa, kisa ‘ushosti’

Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema akichangia hoja Bungeni, Dodoma.
HAKIMU wa Mahakama ya Wilaya Arusha, Patricia Kisinda amejitoa kwenye kesi namba 441/2016 ya uchochezi dhidi ya Rais John Magufuli inayowakabili Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Akizungumza jana mahakamani hapo, Hakimu Kisinda alisema amekubali ombi la Wakili wa Serikali, Sabina Silayo la kumwomba ajitoe kutokana na urafiki na mke wa ndoa wa Lema.

“Ili kutendeka kwa haki pande zote mbili kwenye kesi hii, nakubaliana na ombi lililotolewa mahakamani hapa na najitoa, lakini haki ya kukata rufaa ipo wazi kwa asiyeridhika na uamuzi huu wa kujitoa,” alisema hakimu Kisinda.

Kabla ya kujitoa, Wakili Silayo aliomba hakimu ajitoe kwa sababu upande wa Jamhuri hawana imani naye, hivyo bora ajiondoe sababu ana uhusiano na mke wa ndoa wa mshitakiwa Lema na ushahidi wanao na halina pingamizi, “hivyo hatutatendewa haki, itakuwa busara hakimu akijiondoa”.

Akijibu ombi hilo, Wakili wa mshitakiwa, Sheck Mfinanga alisema Lema anaumwa na alikuwa anarejea Arusha akitokea bungeni Dodoma na alipofika Dar es Salaam alijisikia vibaya na kuwasilisha nakala ya hati ya matibabu, huku akidai nakala halisi atawasilisha.

Pia alipinga Hakimu Kisinda kujitoa kwa madai kuwa Watanzania wote ni marafiki na ndugu na sababu lazima ipimwe uzito na waangalie sababu za hakimu kujitoa, hivyo hoja hizo hazina mashiko.

“Ningefurahi niletewe ushahidi wa urafiki wa mke wa Lema na hakimu huyu, ili tuone kama kuna ukweli, maana hoja hii haina mashiko,” alidai Mfinanga. Hata hivyo, Hakimu Kisinda alipanga kesi hiyo Agosti 2, mwaka huu.

HABARI LEO

No comments: