Advertisements

Monday, July 3, 2017

Ma-DC Kibiti, Rufiji wajitosa kukabili janga jipya

By Azory Gwanda, Mwananchi agwanda@mwananchi.co.tz

Wilaya za Kibiti na Rufiji zimejitosa kushughulikia kilio cha uharibifu wa mikoko katika vijiji 10, huku zikiahidi kukabiliana ipasavyo na waharibifu.

Mikoko katika vijiji vya Kiongoroni, Jaja, Pombwe, Ruma, Mbuchi, Mbwera, Kiechuru, Twasalie, Kiasi na Msala inadaiwa kuharibiwa kwa kasi na wananchi, jambo ambalo limewaamsha wakuu wa wakuu hizo, Juma Njwayo (Rufiji) na Gullamuhussein Kifu (Kibiti).

Hata hivyo, vigogo hao ambao wilaya zao pia zimekumbwa na uharifu wa kiusalama wameitaka jamii kujitosa kuokoa jahazi kabla mkono wa sheria haujaanza kuwashukia waharibifu wa mikoko na mazalia ya viumbe hai wengine.

Kwa mujibu wa ofisa mazingira wa asasi ya Pakaya inayolenga kuzijengea uwezo familia zinazoishi kando ya misitu hiyo kuondokana na umaskini na kuendeleza jamii, Ally Yusuph kuna zaidi ya eka 15,000 za misitu ya mikoko na viumbe hai vilivyomo baharini katika wilaya hizo huenda vikaharibiwa kutokana na shughuli za kibinadamu zinazoendeshwa kwenye maeneo hayo.

“Hadi mwakani takwimu zinaonyesha zaidi ya eka 15,000 za misitu ya mikoko na viumbe hai zitakuwa zimeharibiwa kutokana na shughuli za kibinadamu zinazoendeshwa katika misitu iliyopo kandokando ya Bahari ya Hindi,” amesema.

No comments: