Advertisements

Thursday, August 13, 2020

Mamia Wajitokeza Kuilaki Treni Baada ya Kuikosa kwa Miaka 34

MAMIA ya wananchi jijini Arusha wamejitokeza kwa wingi kwenye hafla ya mapokezi ya Treni ya mizigo ya majaribio iliyowasili ikitokea Dar es Salaam na mabehewa kumi ya Saruji yenye tani 400 na kupokelewa na Mkuu wa wilaya ya Arusha.

Akizindua hafla hiyo ya mapokezi ,mkuu wa wilaya ya Arusha, Kenani Kihongosi, amewaomba wananchi kuhakikisha wanailinda na kuitunza miundo mibinu ya reli ili iweze kudumu na kuwahudumia wananchi.
Ametoa wito kwa wafanyabiashara kuitumia treni hiyo ya mizigo kusafirishia bidhaa zao na hivyo kuwapa unafuu wa bei ya bidhaa na kuboresha maisha ya wananchi kama lilivyo lengo la serikali ya awamu ya Tano kuinua maisha ya watanzania.

Alisema kuwa ujio wa treni hiyo ya Mizigo ni mwanzo wa treni nyingine ikiwemo treni ya Abiria itakayosaidia kusafirisha na kushuka kwa bei za bidhaa ikiwemo saruji na usafiri wa Abiria kwa bei ya 18,000 badala ya elfu 30,000 hadi 35,000 kwa usafiri wa mabasi.

Aidha alisema kuwa treni moja itakuwa inapakia tani zaidi ya mia nane za Mizigo sawa na malori 80 na hivyo kusaidia kuokoa uharibifu wa barabara unaosababishwa na wingi wa malori ya Mizigo.

“Wananchi lindeni na kutunza miundombinu ya Reli ili isihujumiwe na kuturudisha katika zama za kale jambo ambalo tunatakiwa tuliona na kutoa taarifa kwa haraka katika kudhibiti matukio kama hayo”alisema Mkuu huyo.
Awali mkuu wa wilaya ya Arumeru, Jerry Muro aliyewasili na treni hiyo kutokea kituo cha Usariver wilayani Arumeru, hadi jijini Arusha alisema kwa mara ya kwanza treni hiyo ya mizigo inatambulishwa rasmi kwa wananchi na huo ni mwanzo wa safari ya maendeleo na kuashiria kupokelewa kwa treni ya abiria ambayo itaanza mwishoni mwa mwezi huu wa Augosti 2020.

Alisema serikali ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na daktari John Magufuli, inatekeleza Ilani ya uchaguzi kwa vitendo na sio maneno na wananchi ni mashahidi.
Muro, amewaomba wafanyabiashara kuituma fursa hiyo ya uwepo wa treni hiyo kusafirisha bidhaa za viwandani kutoka mikoa mbalimbali kuipeleka mkoani Arusha kutoka na kwenda mikoa mingine.

Akitoa salamu zake ,Katibu wa Chama cha Mapinduzi,wilaya ya Arusha, Denis Mwita, amesema ujio wa treni hiyo ni kurahisisha huduma ya usafirishaji wa mizigo na kuwapunguzia gharama za mizigo na usafirishaji wananchi.
Alisema sasa Chama cha Mapinduzi kimefikia mwishoni mwa utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya mwaka 2015-2020 ambayo imetekelezwa kwa vitendo na wananchi ni mashahidi kwa maendeleo yaliyopatikana katika kipindi cha miaka mitano ya awamu ya kwanza ya rais Magufuli.


Katibu mwita, alisema mkoa wa Arusha, una viwanda vingi ikiwemo vya mabati na chuma lakini ni mkoa ambao hauna kiwanda cha Saruji hivyo treni hiyo itatumika kusafirishia pia Saruji kutoka kwenye mikoa mingine inakozalishwa na kuileta Arusha hivyo kupunguza gharama za bei za bidhaa na kuwataka wananchi kuendelea kukiamini Chama cha Mapinduzi na serikali yake.

Aliwaambia wananchi kwamba hawana cha kumlipa rais Magufuli, kutokana na aliyoyafanya hivyo wahakikishe wanamlipa kwa kumpatia kura za kutosha kwenye uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba 28 mwaka huu.

Baadhi ya wananchi waliokuwepo kwenye hafla hiyo wameishukuru serikali ya awamu ya tano kwa kuwasogezea huduma hiyo ya usafiri na kuwapunguzia gharama za nauli kutoka kiasi cha 30.000 hadi Elfu kumi na nane.

GPL

No comments: