Advertisements

Friday, June 9, 2023

TRILIONI 1.2 KUDHIBITI UHALIFU NCHINI


 
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni (watatu kushoto) akishuhudia uwashwaji wa Pikipiki Maalumu ya kuongoza misafara ya viongozi iliyokabidhiwa kwa Jeshi la Polisi na mdau wa maendeleo, Mohammed Ibrahim (wakwanza kushoto). Wapili kushoto ni Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, Muliro Jumanne.Tukio hilo la makabidhiano limefanyika leo,jijini Dar es Salaam.Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, Muliro Jumanne akiwasha pikipiki Maalumu ya kuongoza misafara ya viongozi iliyokabidhiwa kwa Jeshi la Polisi na mdau wa maendeleo, Mohammed Ibrahim (kushoto).Tukio hilo la makabidhiano limefanyika leo,jijini Dar es Salaam.Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
Pikipiki Maalumu ya kuongoza misafara ya viongozi iliyokabidhiwa kwa Jeshi la Polisi na mdau wa maendeleo, Mohammed Ibrahim (hayupo pichani).Tukio hilo la makabidhiano limefanyika leo,jijini Dar es Salaam.Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Na Mwandishi Wetu,Dar es Salaam
Serikali imetenga jumla ya Shilingi Trilioni 1.2 katika Bajeti pendekezwa ya Mwaka 2023/2024 huku kukiwa na ongezeko, tofauti na Bajeti ya Mwaka 2022/2023 huku ongezeko hilo likilenga katika masuala mazima ya kudhibiti matukio ya uhalifu na uhalifu nchini katika ngazi za mitaa, kata, vijiji na vitongoji ambapo ongezeko hilo linaenda katika Uboreshaji wa Vitendea kazi ikiwemo pikipiki maalumu za kuongoza misafara ya viongozi wakuu, magari na boti za doria.

Akizungumza leo, jijini Dar es Salaam, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni baada ya kushuhudia makabidhiano ya pikipiki maalumu ya kuongoza misafara ya viongozi iliyotolewa na mdau wa maendeleo ikiwa ni moja ya misaada huku jumla ya pikipiki alizotoa ni tatu na akiahidi pia kutoa magari kwa Jeshi la Polisi ili kusaidia jukumu la ulinzi wa mali na wananchi.

“Napozungumzia vitendea kazi muhimu ni Vyombo vya Usafiri, yanapotokea matukio askari wetu waweze kufika kwa haraka, katika bajeti ya mwaka huu (2023/2024) tumeweza kutenga fedha na tumeshaanza ununuzi wa magari kwa ajili ya kupeleka kwenye wilaya zote nchini, pikipiki katika kata zote nchini, lakini pia bajeti ya serikali katika wizara yetu tangu Mheshimiwa Rais (Dkt.Samia Suluhu Hassan) ameingia madarakani imeongezeka kutoka Bilioni 900 Mpaka Trilioni 1.2, fedha hii nyongeza yake ni sehemu ya fedha ambayo inayokwenda kuhudumia mambo mbalimbali ikiwemo mafuta kwa ajili ya matumizi ya vyombo hivyo vya usafiri kwenye ngazi za juu na chini.” Alisema Waziri Masauni

Waziri Masauni pia aliweka wazi Mpango wa Ujenzi wa Vituo vya Polisi katika Kata na Shehia zote nchini huku akitoa wito kwa wadau kujitokeza kuiunga mkono serikali katika adhma yake ya kuhakikisha huduma za Ulinzi wa Mali na wananchi unafika katika ngazi zote ili kuweza kudhibiti wahalifu na matukio mbalimbali ya uhalifu.

Akizungumza baada ya kupokea moja kati ya pikipiki tatu zilizotolewa na mdau wa maendeleo, Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Jeshi la Polisi, Muliro Jumanne ameishukuru wizara kwa kuwaunganisha na wadau na ameahidi msaada huo kutumika katika dhamira iliyokusudiwa huku mdau wa maendeleo, Mohammed Ibrahim akilishukuru Jeshi la Polisi kwa msaada wanaotoa katika ulinzi wa mali na wananchi na akiahidi kuendelea kutoa misaada mbalimbali kwa jeshi hilo ili kusaidia mapambano dhidi ya uhalifu na matukio ya uhalifu.

No comments: