Advertisements

Tuesday, April 23, 2024

DKT. DIMWA : AJIVUNIA HAZINA YA WAZEE WA CCM


NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dkt.Mohamed Said Dimwa, akizungumza na kada wa CCM ndugu Waalidi Psinarie Kavishe(wa kwanza kushoto) nyumbani kwake Kwa mchina mwanzo Unguja.
NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dkt.Mohamed Said Dimwa(upande wa kulia),akizungumza na Kadhi Mkuu mstaafu wa Zanzibar Sheikh Khamis Haji Khamis nyumbani kwake Mwanakwerekwe Unguja.
NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dkt.Mohamed Said Dimwa, akisalimiana na Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba mstaafu ndugu Salum Juma Tindwa nyumbani kwake kwa Mchina Unguja.
NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dkt.Mohamed Said Dimwa, akizungumza na aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Wanawake na Watoto Zanzibar ndugu Msham Abdallah Khamis nyumbani kwake Chuini Unguja.

NA IS-HAKA OMAR,ZANZIBAR.
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar kimesema kitaendelea kutunza,kuthamini na kuenzi hazi na ya wazee waliohudumu kwa uadilifu mkubwa katika nafasi mbalimbali za utumishi ndani ya Chama na Serikalini kwa ujumla.

Hayo ameyasema Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dkt.Mohamed Said Dimwa,katika ziara yake ya kuwatembelea wazee mbalimbali wa Chama hicho katika maeneo mbalimbali ya Unguja.

Alisema maendeleo yaliyopatikana nchini yalijengewa misingi imara na wazee hao enzi za utumishi wao hivyo wana mchango mkubwa katika mafanikio yaliyofikiwa hivi sasa ndani ya Chama Cha Mapinduzi na Serikali zake zote mbili zikiwemo ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Zanzibar.

Katika maelezo yake Naibu Katibu Mkuu huyo Dkt.Dimwa, alieleza kuwa Chama Cha Mapinduzi kinajivunia kwa kuwa na wazee mbalimbali wenye uzoefu na upeo mkubwa wa maarifa ya kushauri mambo mbalimbali yenye kuleta tija.

“Watu wengi wanajiuliza kwa nini CCM kila siku inazidi kuimarika ni kutokana na uwepo wa Wazee awa ambao wengi wao walifanya kazi kubwa ya utumishi katika maeneo mbalimbali ya Chama na Serikali na wanaendelea kutushauri mambo mema yanayoleta ufanisi ndani ya taasisi yetu.”, alisema Dkt.Dimwa.

Kupitia ziara hiyo aliwasisitiza Viongozi na Watendaji mbalimbali wa Chama na Jumuiya zake Zanzibar kuendeleza utamaduni wa kuwatembelea wazee na makundi mengine yenye mahitaji maalum ili nao wajione bado wanakumbukwa na kuthaminiwa juu ya kazi kubwa waliofanya katika kuimarisha maendeleo ya nchi.

Dkt.Dimwa, amewatembelea wazee mbalimbali wakiwemo Kadhi Mkuu wa Zanzibar mstaafu Sheikh Khamis Haji Khamis,kada wa CCM ndugu Waalidi Psinarie Kavishe, aliyekuwa Mkuu wa Mkoa Kusini Pemba ndugu Salum Juma Tindwa na aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Wanawake na Watoto Zanzibar ndugu Msham Abdallah Khamis katika ziara hiyo pia alitoa sadaka mbalimbali kwa ajili ya kuwafariji.

Akitoa shukrani zake kada wa CCM ambaye ni miongoni mwa Wazee waliotembelewa ndugu Waalidi Kavishe, amempongeza Naibu Katibu Mkuu huyo Dkt. Dimwa kwa ziara yake hiyo iliyojenga matumaini na upendo kwa wazee hao ambao nao wamejiona wanakumbukwa na viongozi wa sasa.

Ndugu Kavishe,alitoa wito kwa viongozi,watendaji na wanachama wa CCM nchini kuhakikisha Chama Cha Mapinduzi kinashinda kwa kura nyingi katika uchaguzi mkuu ujao wa dola wa mwaka 2025.

No comments: