Advertisements

Thursday, April 25, 2024

TAADHARI IWE NGUZO KATIKA KIPINDI HIKI CHA MVUA NYINGI - KAMSAMBA


Na Issa Mwadangala
Wananchi wa Kata Mkulwa Tarafa ya Kamsamba Wilaya ya Momba Mkoani Songwe wametakiwa kuchukua tahadhari katika kipindi hiki cha mvua nyingi zinazoendelea kunyesha maeneo mbalimbali wilayani humo

Rai hiyo imetolewa Aprili 25,2024 na Mkuu wa Polisi Wilaya ya Momba Mrakibu Mwandamizi wa Polisi SSP Kennedy Msukwa wakati alipokuwa akitoa elimu juu ya madhara ya mvua nyingi zinazoendelea kunyesha maeneo mbalimbali wilayani humo.

SSP Msukwa amewataka wazazi na jamii kwa ujumla kuongeza umakini katika malezi ya watoto hasa katika kipindi hiki cha mvua nyingi zinazoendelea kunyesha ikiwa ni pamoja na kuwakataza kucheza michezo hatarishi kama kucheza na kuogelea kwenye maji yaliotuama (madimbwi) mabwawa na mito.
“Wazazi na walezi shughuli za kutafuta nguvu ya tumbo ziende sambamba na malezi ya watoto msiwaache watoto wajilee wenyewe kitendo ambacho kinapelekea watoto kusombwa na maji au kudumbukia kwenye mabwawa, mito na visimani kitendo hiki kinapunguza kizazi cha kesho ambacho ni hazina kwa taifa letu” alisema SSP Msukwa.

“Wavuvi mnatakiwa kufuata sharia na utaratibu wa shughuli zenu za kila siku ikiwa ni pamoja na kufanya uvuvi salama pia kuangalia hali ya hewa kabla ya kuingia kwenye shughuli zenu ili kujiepusha na madhara ambayo yanaweza kuepukika ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu pindi muonapo au mfanyiwapo kwa Jeshi la Polisi ili zishughulikiwe kwa haraka ili maeneo yenu yaendelee kuwa salama” alisisitiza SSP Msukwa.
Baada ya elimu hiyo Zaidi ya miti 100 ilipandwa katika Shule ya Sekondari ya Mkulwa iliyopo katika kata hiyo kwa lengo la kutunza mazingira shuleni hapo.

No comments: