Monday, July 15, 2024

SHILINGI BILIONI 4.4 KUJENGA SHULE YA SEKONDARI YA WASICHANA MKOANI RUVUMA


Serikali imetoa zaidi ya Sh.bilioni 4.4 kwa ajili ya kujenga shule ya Sekondari ya wasichana yenye michepuo ya masomo ya Sayansi wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma.
Shule hiyo imepewa jina la Dkt Samia Suluhu Hassan,imepangiwa kuchukua wanafunzi 610 wakiwemo wa kidato cha kwanza(138)kidato cha tano(265) na wanafunzi wa kidato cha sita(210)kwa mwaka wa masomo 2024.

Mkuu wa shule hiyo Dafrosa Chilumba  alisema, hadi sasa wanafunzi walioripoti ni 485 kati yao wanafunzi wa kidato cha kwanza 138,wa kidato cha tano 143 ambao wanatoka wilaya zote za mkoa wa Ruvuma na nje ya mkoa huo na wanafunzi waliobaki ni wa kidato cha sita.

Chilumba ametaja baadhi ya majengo yaliyokamilika kujengwa katika shule hiyo vyumba 22 vya madarasa maktaba,majengo ya Tehama,maabara nyumba za walimu,jengo la utawala na majengo mengine yanaendelea kujengwa na yapo katika hatua mbalimbali za ujenzi.
Chilumba,amempongeza Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi zilizowezesha kujengwa shule hiyo iliyotoa fursa kwa wasichana wengi wa mkoa wa Ruvuma na nchi kwa ujumla kupata nafasi kuendelea na masomo ya elimu ya juu.

“niseme tu ukweli katika shule hii kuna mazingira mazuri yanayomfanya mtoto kuwa na utulivu mkubwa na kusomo kwa bidii na walimu kufanya kazi zao kwa weledi mkubwa,tunampongeza Rais Dkt Samia kwa kutuletea fedha za ujenzi wa shule yetu”alisema Chilumba.

Aidha,amemshukuru Mbunge wa Jimbo la Namtumbo Vita Kawawa kutokana na juhudi zake za kupigania shule hiyo kujengwa wilayani Namtumbo,kwani imesaidia sana watoto wengi wa kike waliomaliza darasa la saba na kidato cha tano kuendelea na masomo yao na ingeweza kujengwa katika wilaya nyingine ya mkoa wa Ruvuma.

Mbunge wa Jimbo la Namtumbo Vita Kawawa,amewapongeza wanafunzi wa kidato cha tano kwa kufanya vizuri katika mitihani yao ya kidato cha nne hali iliyowawezesha kupata nafasi ya kujiunga na shule hiyo ili kuendelea na masomo yao.

Kawawa,amewataka wanafunzi kuliheshimisha jina la Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kusoma kwa bidii na kujiepusha na vishawishi vinavyoweza kukatisha ndoto zao ili waweze kufanya vizuri na kutimiza malengo yao.

Mwanafunzi wa kidato cha tano kutoka mkoa wa Iringa Groly Mgwama,ameishukuru serikali kwa kuwapa nafasi ya kujiunga na shule ya Sekondari Dkt Samia kwani itawasaidia kutimiza malengo ya ndoto zao.

No comments: