ANGALIA LIVE NEWS

Tuesday, June 21, 2011

ACHA TABIA HIZI SITA MBAYA ZA ULAJI-GPL

Kama unajali afya na mwili wako, ama usipatwe na maradhi ya mara kwa mara au usinenepe kupita kiasi, huna budi kuzingatia ulaji sahihi na kujiepusha na tabia mbaya sita zifuatazo ambazo baadhi ya watu zimekuwa sehemu ya maisha yao:

ULAFI
Kwa kawaida, mtu anapokula vyakula ambavyo havina virutubisho vya kutosha na vyenye sukari au chumvi nyingi, hula kupita kiasi bila kujijua. Ndani ya saa 6, mtu huyu anaweza kula vyakula vidogovidogo vingi kama vile soda, biskuti, mihogo au chipsi za kukaanga, ice cream, koni, n.k.


Ulaji wa namna hii haufai kama vile ambavyo haufai ulaji wa vyakula vilivyoondolewa virutubisho wakati wa utengenezaji, kama vile unga wa mahindi mweupe, ngano nyeupe, n.k. Mtu anapokula vyakula hivi, uchomaji wake wa mafuta mwilini huwa mgumu na hivyo mafuta kurundikana mwilini na kuwa chanzo cha unene na ugonjwa wa kisukari.

KUJISHINDISHA NA NJAA
Kama hauko katika funga, hutakiwi kushinda na njaa. Kinachotokea wakati wa kula baada ya kushinda na njaa kutwa nzima ni kula chakula kingi kwa wakati mmoja ambacho hakiwezi kuyeyushwa chote na mafuta yake kutumika kama nishati ya mwili. Matokeo yake mafuta hujihifadhi mwilini na kusababisha unene. Kuepuka hali hii, kula kwa wakati na kwa kiasi kidogo.

KULA USICHOKIJUA
Watu wengi hawana uelewa wa kutosha wa vyakula wanavyokula kama vina faida au madhara yoyote katika miili yao, hasa wale wanaokula kwenye migahawa. Kujua sifa ya kila chakula unachokula ni jambo muhimu sana. Ni vizuri kujua mahitaji ya mwili wako ili kula chakula ambacho hakitabaki mwilini kama ziada, hasa kwa upande wa vyakula vyenye mafuta na sukari nyingi.

Ulaji wa vyakula vilivyotengenezwa kwa unga mweupe, kama vile mikate, ugali na ulaji wa vyakula vya sukari nyingi, kama vile soda na vinywaji vingine baridi, kunachangia kuongezeka kwa mafuta mwilini hivyo kusababisha unene na ugonjwa wa kisukari.

4. UKOSEFU WA MAZOEZI
Miili yetu imeumbwa kujishughulisha. Ndiyo maana utaona pale unapoamka na kujisikia mchovu, ukishaanza kufanya kazi unajisikia vizuri. Kujishughulisha kwa kufanya mazoezi kunasaidia kuyeyusha chakula na mafuta na kuyatumia kama nishati ya mwili.

5.KUTOFUNGUA KINYWA ASUBUHI
Usidhani kuwa tumbo ndilo linalokwambia halina kitu hivyo linahitaji chakula, bali ni ubongo ndiyo unaotoa taarifa ya chakula. Ni vyema ukahakikisha unafungua kinywa asubuhi ili kuulisha ubongo wako uweze kufanyakazi yake sawasawa. (labda kama uko kwenye funga).

6. KUTOKUNYWA MAJI
Ili chembe hai za ubongo na viungo vingine vya mwili vifanye kazi sawasawa, ikiwemo ngozi, unahitaji maji. Ili mwili uyeyushe mafuta unayokula kutokana na chakula, unahitaji kiasi cha glasi nane za maji kila siku (kikiwa ndiyo kiwango cha chini kabisa).

Faida za maji mwilini ni nyingi. Maji siyo tu yanakata kiu yako, bali pia yanasaidia kuondoa sumu mwilini na kukupunguzia njaa ya mara kwa mara. Vinywaji vingine kama vile soda na kahawa, siyo vinasaidia kukata kiu, bali vinachangia ukaukaji wa maji mwilini. Usitii kiu yako kwa kujidanganya kunywa soda.

Hayo ni mambo sita ya kuzingatia ili kudumisha afya bora, kama umekuwa ukifanya moja kati ya hayo mambo sita au yote, ni wakati muafaka wa kubadilika na utaona uamuzi ulioufanya ni wa busara.

Kwa wale wenye nia ya kupunguza unene, kama utaendelea hata na tabia moja kati ya sita zilizoainishwa hapa, kamwe huwezi kufikia malengo yako ya kupunguza uzito!

No comments: