Advertisements

Tuesday, January 22, 2013

Sitta ampinga Makinda kuhusu mabunge mawili

SPIKA wa zamani wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samuel Sitta ametofautiana na mrithi wake, Anne Makinda kuhusu muundo wa Bunge katika Katiba Mpya, akisema nchi inahitaji Bunge moja tu.

Akitoa maoni yake Januari 15 mwaka huu, mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Spika Makinda alitaka kuwe na mabunge mawili; la kuchaguliwa na wananchi na lile la Seneti litakalotokana na wataalamu mbalimbali na viongozi wa zamani wenye uzoefu wa kuitumikia nchi.

“Tumetaka Bunge la Seneti lijumuishe viongozi waliolitumikia taifa ambao tunajua kwamba watakuwa na uzoefu wa kutosha katika masuala muhimu ya nchi. Tumetaka pia bunge hilo liwe na wataalamu wa mambo mbalimbali ili kuhakikisha tunakuwa na Serikali imara.”

Alisema hatua hiyo itasaidia kwani Bunge la Seneti litaondoa mambo ya itikadi za vyama bungeni kama ilivyo sasa na kujali masilahi ya taifa.

Lakini akizungumza muda mfupi baada ya kutoa maoni yake mbele ya Tume hiyo Dar es Salaam jana, Sitta ambaye pia ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki alisema hakuna haja ya kuwa na mabunge mawili, kwani bado nchi haina uwezo wa kumudu gharama za uendeshaji wake.

“Kiukweli sioni kama kuna haja ya kuwa na mabunge mawili kwani uwezo wetu wa kuendesha mabunge hayo bado ni mdogo. Ninachopendekeza ni kwamba Katiba Mpya ieleze wazi kwamba bunge linatakiwa kuwa na idadi fulani ya wabunge.”

Maadili ya viongozi
Sitta pia alizungumzia suala la maadili na kusema Tanzania inakabiliwa na tatizo la uadilifu wa viongozi na kupendekeza kuwa Katiba Mpya iwe na kipengele cha kuwabana wanaotaka kuwa viongozi kwa kuthibitisha maadili yao.

Alisema Katiba Mpya inapaswa iwe na kifungu kitakachowalazimisha viongozi kuwa wawazi na waadilifu akisema amependekeza hayo kutokana na viongozi wengine kuonekana kutokuwa na maadili.

Alisema amependekeza kuwa kifungu hicho kitamke wazi kwamba mtu anapotaka kuomba nafasi ya uongozi akubali kuhojiwa hadharani ili kuhakikisha kuwa taifa linakuwa na viongozi waadilifu.
“Tusipokuwa na viongozi waadilifu taifa litaelekea sehemu mbaya kwani watu wanapeana nafasi za uongozi kwa kujuana kitu ambacho mwisho wake wanyonge wataendelea kuwa chini na kukosa haki zao,” alisema.
Waziri Sitta alitoa mfano katika Ibara ya 39 ya Katiba ya sasa inayoeleza sifa mbalimbali ambazo anapaswa kuwa nazo kiongozi wa ngazi ya juu, lakini hakuna kifungu kinachoeleza masuala ya uadilifu. Alisema Katiba ijayo kuwe na kifungu kitakachosema kwamba sifa mojawapo ya kiongozi ni kuwa mwadilifu.

Mahakama ya Katiba
Waziri Sitta pia alipendekeza kuwa Katiba Mpya itambue uwepo wa Mahakama ya Katiba itakayokuwa inashughulikia kesi za uchaguzi.
Alisema kuna malalamiko mengi ya uchaguzi ikiwa ni pamoja na watu kwenda kinyume cha Katiba hivyo kusisitiza kuwa uwepo wa chombo hicho utasaidia kupunguza malalamiko ya ukiukwaji wa Katiba.

Pia alipendekeza kutambuliwa kwa mgombea binafsi katika Katiba Mpya ili kuongeza wigo wa demokrasia nchini... “Kuna watu wana uwezo wa kuongoza lakini hawako katika vyama, hawa wanapaswa kupata haki ya kuchaguliwa pia badala ya kuwalazimisha wawe kwanza wananchi wa chama cha siasa.”

Kuhusu Muungano alisema hakuna haja ya kuwa na Serikali tatu kwani huko kutakuwa ni kuuvunja Muungano uliowekwa na waasisi wa taifa hili.
Alisema anapendekeza Katiba Mpya iendeleze Muungano uliopo sasa kwani hakuna kitu chochote kinachouathiri.

“Ninavyoona ni vyema tukabaki na Serikali mbili kama kawaida. Hakuna haja ya kuwa na Serikali tatu kwani huko kutakuwa ni kutaka kuuvunja Muungano uliopo sasa,” alisema.
SPIKA wa zamani wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samuel Sitta ametofautiana na mrithi wake, Anne Makinda kuhusu muundo wa Bunge katika Katiba Mpya, akisema nchi inahitaji Bunge moja tu.

Akitoa maoni yake Januari 15 mwaka huu, mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Spika Makinda alitaka kuwe na mabunge mawili; la kuchaguliwa na wananchi na lile la Seneti litakalotokana na wataalamu mbalimbali na viongozi wa zamani wenye uzoefu wa kuitumikia nchi.

“Tumetaka Bunge la Seneti lijumuishe viongozi waliolitumikia taifa ambao tunajua kwamba watakuwa na uzoefu wa kutosha katika masuala muhimu ya nchi. Tumetaka pia bunge hilo liwe na wataalamu wa mambo mbalimbali ili kuhakikisha tunakuwa na Serikali imara.”

Alisema hatua hiyo itasaidia kwani Bunge la Seneti litaondoa mambo ya itikadi za vyama bungeni kama ilivyo sasa na kujali masilahi ya taifa.

Lakini akizungumza muda mfupi baada ya kutoa maoni yake mbele ya Tume hiyo Dar es Salaam jana, Sitta ambaye pia ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki alisema hakuna haja ya kuwa na mabunge mawili, kwani bado nchi haina uwezo wa kumudu gharama za uendeshaji wake.

“Kiukweli sioni kama kuna haja ya kuwa na mabunge mawili kwani uwezo wetu wa kuendesha mabunge hayo bado ni mdogo. Ninachopendekeza ni kwamba Katiba Mpya ieleze wazi kwamba bunge linatakiwa kuwa na idadi fulani ya wabunge.”

Maadili ya viongozi
Sitta pia alizungumzia suala la maadili na kusema Tanzania inakabiliwa na tatizo la uadilifu wa viongozi na kupendekeza kuwa Katiba Mpya iwe na kipengele cha kuwabana wanaotaka kuwa viongozi kwa kuthibitisha maadili yao.

Alisema Katiba Mpya inapaswa iwe na kifungu kitakachowalazimisha viongozi kuwa wawazi na waadilifu akisema amependekeza hayo kutokana na viongozi wengine kuonekana kutokuwa na maadili.

Alisema amependekeza kuwa kifungu hicho kitamke wazi kwamba mtu anapotaka kuomba nafasi ya uongozi akubali kuhojiwa hadharani ili kuhakikisha kuwa taifa linakuwa na viongozi waadilifu.
“Tusipokuwa na viongozi waadilifu taifa litaelekea sehemu mbaya kwani watu wanapeana nafasi za uongozi kwa kujuana kitu ambacho mwisho wake wanyonge wataendelea kuwa chini na kukosa haki zao,” alisema.
Waziri Sitta alitoa mfano katika Ibara ya 39 ya Katiba ya sasa inayoeleza sifa mbalimbali ambazo anapaswa kuwa nazo kiongozi wa ngazi ya juu, lakini hakuna kifungu kinachoeleza masuala ya uadilifu. Alisema Katiba ijayo kuwe na kifungu kitakachosema kwamba sifa mojawapo ya kiongozi ni kuwa mwadilifu.

Mahakama ya Katiba
Waziri Sitta pia alipendekeza kuwa Katiba Mpya itambue uwepo wa Mahakama ya Katiba itakayokuwa inashughulikia kesi za uchaguzi.
Alisema kuna malalamiko mengi ya uchaguzi ikiwa ni pamoja na watu kwenda kinyume cha Katiba hivyo kusisitiza kuwa uwepo wa chombo hicho utasaidia kupunguza malalamiko ya ukiukwaji wa Katiba.

Pia alipendekeza kutambuliwa kwa mgombea binafsi katika Katiba Mpya ili kuongeza wigo wa demokrasia nchini... “Kuna watu wana uwezo wa kuongoza lakini hawako katika vyama, hawa wanapaswa kupata haki ya kuchaguliwa pia badala ya kuwalazimisha wawe kwanza wananchi wa chama cha siasa.”

Kuhusu Muungano alisema hakuna haja ya kuwa na Serikali tatu kwani huko kutakuwa ni kuuvunja Muungano uliowekwa na waasisi wa taifa hili.
Alisema anapendekeza Katiba Mpya iendeleze Muungano uliopo sasa kwani hakuna kitu chochote kinachouathiri.

“Ninavyoona ni vyema tukabaki na Serikali mbili kama kawaida. Hakuna haja ya kuwa na Serikali tatu kwani huko kutakuwa ni kutaka kuuvunja Muungano uliopo sasa,” alisema.
Mwananchi


No comments: