Thursday, July 18, 2013

Miili ya askari JWTZ kuletwa Jumamosi

Dar/mikoani. Wakati miili ya askari wa Tanzania waliokufa Darfur ikitarajiwa kuletwa keshokutwa, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu wameanza kuwasili Dar es Salaam kwa ajili ya kuipokea.
Msemaji wa Mpango wa Kulinda Amani wa Umoja wa Mataifa na Afrika (UNAMID), kwenye Mji wa Darfur, Chris Cycmakick alisema jana kuwa miili hiyo ilikuwa ikiendelea kufanyiwa uchunguzi ambao unatarajiwa kukamilika leo.
“Hata kama uchunguzi ukikamilika kesho (leo), hatuwezi kusafirisha keshokutwa (kesho Ijumaa) kwa kuwa hapa Sudan ni kama siku ya mapumziko. Sasa utaratibu unafanyika kuisafirisha Jumamosi kwa ndege ya Umoja wa Mataifa,” alisema Cycmakick.
Wapiganaji hao saba waliuawa na moja ya vikundi vya waasi walipokuwa wakitekeleza majukumu yao ya kulinda amani kupitia UNAMID huko Darfur.
Uchunguzi wa gazeti hili, ulibaini kuwa wanajeshi hao wanatoka vikosi vya 42KJ Chabruma, Songea, 44KJ Mbeya, 36KJ Msangani, 92KJ Ngerengere, 94KJ Mwenge, Dar es Salaam, 41KJ Nachingwea na Makao Makuu ya Jeshi- Upanga, Dar es Salaam.
Familia zawasili Dar
Wakati miili ya wapiganaji hao ikiletwa, tayari familia zao zimeshawasili Dar es Salaam kwa ajili ya kuwapokea marehemu hao kwa maziko katika maeneo yaliyopangwa na wengine wakisubiri katika mikoa yao.
Akizungumza na mwandishi wetu jana eneo la Mji Mpya, Songea, Mama wa marehemu, Rodney Ndunguru, Lucy alisema wanachosubiri ni kupokea mwili wa marehemu watakapoletewa na jeshi kutoka Dar es Salaam.
Alisema mwili wa mtoto wake huyo aliyekuwa Kambi ya 92KJ, Ngerengere mkoani Morogoro utasindikizwa na mke wa marehemu, Fatma Hajj Ammen anayetokea Zanzibar alikokwenda kujifungua mtoto ambaye sasa ana miezi minne.Mama huyo alisema kuwa mwanawe huyo kifungua mimba na aliyekuwa katika kikosi cha makomandoo, atazikwa alikolala baba yake, eneo la Myangayanga, Songea.
Naye Maria Chaula, mke wa Koplo Oswald Chaula aliyekuwa Kikosi cha Mizinga katika Kambi ya Chabruma, aliondoka jana alfajiri kwenda Dar es Salaam kupokea mwili wa marehemu mume wake wakati watoto wake wanne wakitangulia Kijiji cha Mtitu Wilaya Kilolo, Iringa kwa taratibu nyingine za mazishi.
Mama wa marehemu Chaula, Zaina Mpagama, akiwa kijijini Mtitu, alisema askari huyo ambaye ni mtoto wake wa sita na ni pekee wa kiume, ameacha pengo lisilozibika... “Baba, nimepata pigo, mwanangu pekee wa kiume jamani...,” alisema huku akilia kwa uchungu.
Mjini Mbeya, huzuni na simanzi zimetawaka katika Kambi ya 44KJ Mbalizi baada ya taarifa za kifo cha askari wa miguu, Peter Werema.
Marehemu ameacha mke na watoto wawili na taarifa zinasema taratibu za mazishi na mahali atakakozikwa marehemu huyo zitafanyika mara baada ya mwili wake kuwasili.
Hata hivyo, taarifa zilizopatikana jana zilieleza kuwa marehemu ambaye ni mara yake ya pili kwenda Sudan ni mwenyeji wa Mkoa wa Mara na huenda akasafirishwa kwenda huko kwa mazishi.
Nayo familia ya marehemu Mohamed Chukilizo aliyekuwa Kambi ya Majimaji, 41KJ Nachingwea iliwasili Dar es Salaam jana kwa basi tayari kupokea mwili wa marehemu mpendwa wao.
Mtoto wa marehemu, Amina Mohamed anayesoma kidato cha nne Sekondari ya Nachingwea alisema jana kuwa anasikitika kumpoteza baba yake lakini anaamini kuwa ni mipango ya Mungu.
Amina alikuwa akisoma Nachingwea wakati mama yake yuko Dar es Salaam. Marehemu ambaye ni mwenyeji wa Mkoa wa Kigoma, huenda akasafirishwa kwenda mkoani humo kwa maziko.
Msiba mwingine uko nyumbani kwa kaka wa marehemu, Mohamed Juma, Lugalo Area J. Hata hivyo, hali ilikuwa tofauti kwani hakukuwa na watu kwa kile kilichoelezwa kuwa mke wa marehemu tayari ametangulia Zanzibar ambako mwili wa mpiganaji huyo utapelekwa kwa maziko.
Habari zilizopatikana jana zilisema marehemu Juma ambaye alikuwa mkazi wa Dar es Salaam, mwili wake utasafirishwa kwenda Zanzibar baada ya shughuli ya kuaga miili hiyo Makao Makuu ya Jeshi, Upanga Dar es Salaam.
Mpiganaji mwingine ni Sajini Shaibu Othman kutoka Makao Makuu ya Jeshi, MMJ, ambaye familia yake inaendelea na utaratibu wa maziko nyumbani kwake, Kigamboni, Dar es Salaam.
Marehemu huyo aliyekuwa askari wa miguu, ameacha mjane na watoto wawili. Mpiganaji huyo kama alivyo, Mohamed Juma wanatarajiwa kusafirishwa kwenda Zanzibar kwa maziko.
Mke wa mpiganaji, Christopher Msofe kutoka Kambi ya Jeshi Msangani, Pwani, Amina Juma akiwa nyumbani kwake Visiga alisema: “Bado tunapanga utaratibu wa kupokea mwili, lakini maziko yatakuwa Kange, Tanga.”
Msofe aliyekuwa askari wa kikosi cha ardhini aliyehamia kambini hapo akitokea Moshi Kilimanjaro, hakubahatika kupata mtoto.
Wapiganaji saba waliuawa na wengine 19 walijeruhiwa Jumamosi iliyopita na ilielezwa kuwa mauaji hayo yalisababishwa na askari hao kufuatilia magari yao yaliyokuwa yametekwa na kundi mojawapo la waasi.
Mmoja kati ya majeruhi walionusurika na kifo hicho amehamishwa kutoka Hospitali ya Nyala na kupelekwa Khartoum kwa matibabu zaidi.
Imeandikwa na Joyce Joliga, Songea; Geofrey Nyang’oro, Kilolo; Brandy Nelson, Mbeya; Julieth Ngarabali, Visiga; Christopher Lilai, Nachingwea na Patricia Kimelemeta, Dar.
Mwananchi

No comments: