Advertisements

Wednesday, August 9, 2017

Askari tisa wa wanyamapori wasimamishwa kazi kwa tuhuma za kupokea rushwa mkoani Rukwa.

Waziri wa Maliasili na utalii Profesa Jumanne Maghembe, amewasimamisha kazi askari wa wanyamapori tisa wilayani Nkasi mkoani Rukwa, kwa tuhuma za rushwa wakipokea fedha kutoka kwa wafugaji na kuwaruhusu kuingiza mifugo kwenye msitu wa hifadhi wa Mfili na Pori la Akiba la Lwafi kinyume cha sheria na pia kutoa siri za serikali na amewakabidhi kwa taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa kwa uchunguzi zaidi.
Akizungumza mbele ya kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya ya Nkasi mjini Namanyere, Waziri Profesa Maghembe amesema amesikitishwa kuona licha ya juhudi mbalimbali zilizofanywa na wizara yake kuwarekebisha mienendo watumishi hao lakini bado wamekuwa wakiendelea kufanya mambo yasiyoendana na kanuni na taratibu za utumishi wa umma,kwa kufanya biashara ya kuchukua fedha kwa wafugaji na kuwaruhusu kuchungia mifugo yao katika pori hilo la akiba.
Mapema akiongea kwenye kikao hicho cha dharura, mkuu wa wilaya ya Nkasi Bw Said Mtanda, amesema imefikia sasa kutowashirikisha tena askari wanyamapori hao katika operesheni mbalimbali,kwani wakiwapa taarifa wanavujisha siri kwa wafugaji walioingia na mifugo kwenye pori hilo na msitu wa hifadhi wa Mfili, huku kamanda wa TAKUKURU wa wilaya ya Nkasi Bw Samson Bishati akisema anawasiliana na wakuu wake mkoani ili kuanza zoezi hilo mara moja.

No comments: