Advertisements

Friday, October 20, 2017

Kifaa kilichotumika kurekodi kashfa ya rushwa chawasilishwa TAKUKURU

Diwani wa Mbuguni wilayani Arumeru mkoani Arusha, Ahimidiwe Rico amewasilisha kwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kifaa anachodai alikitumia kuwarekodi  waliomshawishi kujiuzulu wadhifa huo.

Baada ya Oktoba 17,2017 kuhojiwa na maofisa wa Takukuru, jana Oktoba 19,2017 Rico alifika ofisi za taasisi hiyo saa nane mchana kukabidhi kifaa hicho chenye umbo la kalamu anachodai kimetengenezwa nchini Ujerumani.

Akizungumza na waandishi wa habari kabla ya kukabidhi kifaa hicho, alisema ameitikia wito wa maofisa wa Takukuru waliomtaka akiwasilishe.

Alisema anasimamia ukweli ambao utamuweka huru na haogopi kwa kuwa katika siku za hivi karibuni amekuwa akipokea baadhi ya vitisho kutoka kwa watu wanaomtaka asijihusishe na sakata hilo.

Diwani huyo wa Chadema alisema tangu aanze kushawishiwa apokee rushwa kwa lengo la kujiuzulu nafasi yake alirekodi matukio yote na mawasiliano ambayo amekuwa akiwasiliana na baadhi ya viongozi wa Serikali.

No comments: