Advertisements

Wednesday, March 14, 2018

Polisi, CHADEMA watifuana msibani

Takribani watu 20 wanaodaiwa kuwa wafuasi wa Chadema akiwemo diwani wa Kata ya Mabatini, Deo Mbibo wanashikiliwa na polisi baada ya kukamatwa walipokuwa wameenda kuhani msiba wa mwanachama mwenzao.

Akizungumzia tukio hilo mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Mwanza, Leonard Nundi amesema tukio hilo limetokea jana  Machi 13, saa kumi jioni ambapo wafuasi hao wakiwa zaidi ya 500 walienda kuhani msiba huo na ghafla polisi waliwavamia na kumtaka mfiwa kuongea naye.

“Chanzo cha vurugu ni baada ya askari hao kuvamia msibani na kumhitaji mfiwa ambaye ni Laurent Chiro kwa ajili ya mazungumzo, waliposhindwa kuelewana walimchukua diwani na viongozi wengine waliokuwa meza kuu na kuwapandisha kwenye gari la polisi,” amesema Nundi.

Amesema wanachama waliokuwa msibani waliogomea kitendo hicho na kuanza kuwarushia mawe polisi ambao nao walianza kujihami kwa kupiga mabomu ili kuwatawanya.


Akizungumzia tukio hilo, kamanda wa polisi mkoani Mwanza, Ahmed Msangi pamoja na kudai yuko wilayani Kwimba, lakini amesema wafuasi hao wamekuwa na kawaida kukusanyika na kufanya vikao vyao vya kisiri.

Mmoja wa wanachama aliyekuwa eneo la tukio, Emmanuel Tumbo amesema wafuasi hao wametoka katika kata zote 18 za Jiji la Mwanza ambao wamejiwekea utaratibu wa kuhani misiba inapotokea kwa mwanachama anayefiwa au kufariki dunia.

No comments: