Advertisements

Tuesday, August 14, 2018

KUTONYONYESHA WATOTO MAZIWA YA MAMA PEKEE KWA MIEZI SITA KUMECHANGIA UDUMAVU

Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Songwe Dkt. Kheri Kagya akitoa zawadi kwa akina mama wa mfano walioweza kunyonyesha watoto wao maziwa pekee kwa muda wa miezi sita wakati wa maadhimisho ya wiki ya unyonyeshaji yaliyofanyika Halmashauri ya Mji wa Tunduma.
Akina mama wa mfano walioweza kunyonyesha watoto wao maziwa pekee kwa muda wa miezi sita wakiwa katika picha ya pamoja na wadau mbalimbali wanaojishughulisha na afya ya mama na mtoto mkoa wa Songwe.

Na Grace Gwamagobe-Afisa Habari Songwe

Ongezeko la hali ya udumavu Mkoani Songwe inachagizwa na kuwa ni asilimia 25 pekee ya akina mama wote wanaojifungua ndio huwanyonyesha watoto wao maziwa ya mama pekee kwa muda wa miezi sita.

Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Songwe Dkt. Kheri Kagya ameeleza kuwa udumavu mkoani hapa ni asilimia 37.7 ikiwa na maana kuwa kati ya watu 100, 37 wanatatizo la udumavu kiwango ambacho ni kikubwa licha ya Mkoa Songwe kuwa na Vyakula vya kutosha.

“Moja ya sababu kubwa ya ongezeko la udumavu Mkoani kwetu ni kutokana na akina mama wanaojifungua kutowanyonyesha watoto wao maziwa pekee kwa kipindi cha miezi sita, hali hii huwafanya watoto kukosa virutubisho muhimu katika hatua za awali za ukuaji”, amesema Dkt Kagya.

Ameongeza kuwa maziwa ya mama hujenga afya imara kwa watoto hivyo akina mama wanaojifungua wazingatie ushauri wa wataalamu wa afya wa kunyonyesha watoto maziwa ya mama pekee kwa miezi sita, na kisha kuendelea kunyonyesha na vyakula vingine mbadala mpaka mtoto afikishe umri wa miaka miwili.

Dkt Kagya amesema maziwa yanayopatikana ndani ya saa moja baada ya mama kujifungua yana virutubisho vyote kwa ajili ya ukuaji wa mtoto hivyo akina mama wazingatie hilo huku akiongeza kuwa ni asilimia 83 ya akina mama wanaojifungua mkoani Songwe huweza kunyonyesha watoto wao ndani ya saa moja.

“Kumekuwa na visingizio kadhaa kwa akina mama kutonyonyesha ndani ya saa moja baada ya kujifungua wengine husema maziwa ya kwanza yenye rangi ya njano kuwa ni machafu, hapana yale maziwa yana virutubisho vingi vya kwa ajili ya afya njema ya mtoto, pia wengine wanasema maziwa pekee hayamtoshi mtoto kwakuwa atasaikia kiu, hilo nalo sio sahihi maziwa ya mama yana kila kitu hata maji pia”, amesisitiza.

Amefafanua kuwa kumekuwa na upotoshaji kuwa mama mwenye Virusi vya Ukimwi akimnyonyesha mtoto atamuambukiza, kitu ambacho sio sahihi.

Mmoja kati ya akina mama anayeishi na Virusi vya Ukimwi Grace Kandonga amesema yeye ana watoto wawili ambapo akijifungua huwa anawanyonyesha maziwa yake pekee kwa miezi sita bila ya kuwapa chakula kingine na wote hawana maambukizi ya VVU.

Bi Kandonga amesema, “huwa nawanyonyesha watoto wangu kwa muda wa miezi sita bila kuchanganya na kitu chochote, baada ya hapo nawapa chakula mbadala kama vile uji na wote wako salama mpaka sasa, kwahiyo nawashauri akina mama wote tuzingatie ushauri wa wataalamu wa afya na watoto wetu watakuwa na afya njema”

No comments: