Monday, February 19, 2024

MAJALIWA ASISITIZA MPANGO WA SERIKALI WA KUENDELEA KUTUMIA TEHAMA SHULENI.


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema malengo ya Serikali ya Awamu ya Sita ni kuhakikisha Shule zote nchini zinakuwa na mifumo bora ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kurahisisha ujifunzaji na ufundishaji kwenye ngazi zote za elimu.

Ameyasema hayo leo (Alhamisi, Februari 22, 2024) wakati alipotembelea na kukagua miundombinu ya TEHAMA iliyowekwa katika Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Lucas Malia, Ruangwa Mkoani Lindi.
Akizungumza na wazazi na wanafunzi wa Shule hiyo Mheshimiwa Majaliwa ameipongeza Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa kwa kuwezesha kufunga mifumo ya TEHAMA katika shule hiyo.

Aidha, Mheshimiwa Majaliwa, amesema Shule hiyo ya Lucas Malia itakuwa kitovu cha ufundishaji kupitia mifumo ya TEHAMA kwa shule za Sekondari Wilayani Ruangwa.


Katika hatua nyingine Mheshimiwa Majaliwa amesema wana Ruangwa wana kila sababu ya kumshukuru Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kutokana na manufaa ambayo Wilaya hiyo imepata kutokana na utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika sekta mbalimbali.

"Wana-Ruangwa niwakati wetu wa kujivunia uwepo wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, jukumu lenu ni lilelile la kuniunga mimi mkono nifanye kazi, na kumuunga mkono Rais wetu Dkt. Samia afanye kazi yake vizuri, lazima mjivunie, mumuombee, mumsemee, mumtetee na kumuunga mkono katika kila jambo lake”

No comments: