Advertisements

Tuesday, May 21, 2024

MWENGE WA UHURU WAWASILI MKOA WA KASKAZINI UNGUJA


Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Idrisa Kitwana Mustafa kushoto akimkabidhi Mwenge wa Uhuru Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Rashid Hadidi Rashid ili kuukimbiza katika Mkoa wake na Kutembelea Miradi mbalimbali Zanzibar Ukiwa na Ujumbe "Tunza Mazingira na Shiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa Ujenzi wa Taifa Endelevu"


Mkuu wa Wilaya ya Kaskazini A Othman Ali Maulid akizungumza na Wananchi baada ya kufika na Mwenge wa Uhuru katika Shehia ya Chaani Kituo cha Afya ili kuangalia Mradi wa Utoaji wa Chanjo ,Matone na Vyandarua Wilaya ya Kaskazini A Unguja.

Na Sabiha Khamis Maelezo

Kiongozi wa mbio za mwenge wa Uhuru Kitaifa 2024 Godfrey Eliakimu Mzava, amesema utekelezaji wa miradi ya maendeleo ni hazina ya wananchi katika kukuza uchumi na pato la nchi.

Ameyasema hayo katika Uwanja wa Skuli ya Maandalizi ya Kiislam Mfenesini wakati wa makabidhiano ya mwenge wa uhuru 2024 kutoka Mkoa wa Mjini Magharibi na kukabidhiwa Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Amesema ni wajibu wa kila mwananchi kuitunza na kuilinda miradi ya maendeleo inayoanzishwa katika maeneo yao ili iweze kutumika kwa kizazi cha sasa na kijacho.

Aidha amefahamisha kuwa lengo la mbio hizo ni kuangalia utekelezaji miradi mbali mbali ya maendeleo sambamba na kujua fedha zilizotumika katika kuimarisha Nchi.

Samambamba na hayo amewataka wanachi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja kushiriki kikamilifu katika matembezi hayo ili kuweza kuyaunga mkono na kufikiwa malengo yaliokusudiwa.

Mapema ameushukuru uongozi wa Mkoa wa Mjini Magharib kwa ushirikiano waliotoa kwa kuwaratibu vyema matembezi hayo, katika kipindi chote walichokuwa katika mkoa huo jambo ambalo limepelekea kutekeleza vizuri miradi mbalimbali ya maendeleo.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kaskazini "A" Othman Ali Maulid ameahidi kushirikiana vyema na viongozi wa mbio za mwenge katika wilaya hiyo ambapo utatembea kwa urefu wa Kilomita 89 ili malengo lililokusudiwa yaweze kufanikiwa.

Nao wananchi wa wilaya kaskazini A wamefurahishwa na ujio wa mwenge huo wamesema watendelea kuunga mkono juhudi za Serikali ili kuhakikisha matembezi hayo ya mwenge wa uhuru yanaendelea kwa faida ya kizazi cha sasa na kijacho.

Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru 2024, ametembelea miradi mbalimbali ya maendeleo katika Wilaya ya Kaskazini "A" ikiwemo utoaji wa chanjo ya vatamini A na ugawaji wa Vyandarua katika kituo cha Afya Chaani Kikobweni, kukagua mradi wa Skuli ya Sekondari Mkokotoni, kutembelea darasa la mazingira na kutoa vyeti kwa wanafunzi wa mazingira katika Manispaa ya Wilaya ya Kaskazini "A", kutembelea mradi wa ujenzi wa barabara Nungwi pamoja na upandaji wa miti Kibeni.

No comments: