Wednesday, August 28, 2024

NBAA YAFANYA WARSHA KWA WATAHINIWA KWA NJIA YA MTANDAO

 

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Pius A. Maneno akizungumza kwa njia ya mtandao na watahiniwa wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi wakati wa kufungua mafunzo hayo.
Mkufunzi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, CPA Dkt. Emmanuel Christopher akitoa elimu kuhusu namna ya kujiandaa na kufanya masomo ya B1 na C3 kwa watahiniwa wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi waliokuwa wanafuatilia kwa njia mtandao.

Mkufunzi CPA Rashid Mganwa akitoa elimu kuhusu namna ya kujiandaa na kufanya masomo ya B2 na C1 kwa watahiniwa wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi waliokuwa wanafuatilia kwa njia mtandao.
Mkufunzi CPA Ansbert Kishamba akitoa elimu kuhusu namna ya kujiandaa na kufanya somo la B5 kwa watahiniwa wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi.


Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Elimu na Mafunzo NBAA, Peter Lyimo akijibu maswali pamoja na kufunga warsha kwa njia ya mtandaoni kwa watahiniwa wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi.
Baadhi ya Sekretarieti ya Warsha kwa njia ya Mtandao wa NBAA wakiwa kwenye picha ya pamoja na wakufunzi wa warsha kwa njia ya mtandaoni kwa watahiniwa wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi.


Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (​NBAA) imeendesha warsha kwa njia ya mtandao kwa watahiniwa wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi ili kuongeza ufanisi kipindi wanapokwenda kufanya mitihani hiyo.

Akizungumza wakati wa kufungua warsha hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Pius A. Maneno amesema wamefanya warsha hiyo kwa njia ya mtandao na kuwakutanisha watahiniwa wa ngazi mbalimbali wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi katika ngazi mbalimbali ikiwa na lengo la kuwanoa kwenye mbinu mbalimbali za mitihani hasa kwenye maeneo yanayokuwa na changamoto kwa watahiniwa wa Bodi.

CPA Maneno amesema yapo Masomo yanaleta changamoto na kiwango cha ufaulu unakuwa mdogo hivyo tumewaletea walimu wa Masomo hayo kutoka vyuo na Taasisi mbalimbali ili waweze kuwapa uzoefu na mbinu mbalimbali za kuweza kujiandaa na kufanya mitihani ya Bodi.

"Tumewasisitiza sana namna ya kujiandaa wasijiandae kiholelaholela bali waweke muda wa kutosha kwenye kujifunza kwasababu mitihani ya mwezi Novemba itatumia mtaala mpya " alisema CPA Maneno

Pia amesema lengo kubwa la NBAA ni kuona wanapandisha kiwango cha ufaulu kwa mitihani mbalimbali pamoja na kuongeza kiwango cha uelewa ili kipindi wanapomaliza mitihani yao waweze kuwa wabobezi kwenye masuala ya Uhasibu na Ukaguzi.

Naye Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Elimu na Mafunzo NBAA, Peter Lyimo anasema Bodi hiyo imejipanga vizuri ili kuhakikisha kila mtahiniwa anafanya mitihani vizuri na kuhakikisha wanaondoa changamoto zote zinazowakabili, pia aliwashukuru waliohudhuria mafunzo hayo muhimu .

No comments: