Wednesday, September 25, 2024

MAKAMU WA RAIS WA PILI WA ZANZIBAR AZINDUA TAMASHA LA KILIMO HAI MWAKA 2024


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akizungumza Viongozi mbali mbali, watendaji kutoka Wizara ya Kilimo, Taasisi ya Kilimo hai, wadau wa kilimo na wananchi, kwa niaba ya Mhe.Dkt Hussein Ali Mwinyi Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi katikaTamasha la Kilimo hai Mwaka 2024 lililofanyika katika Viwanja vya Maonesho ya Kilimo Nanenane Dole Wilaya ya Magharibi " A " Unguja.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Hemed Suleiman Abdulla amesema kufanyika kwa Tamasha la Kilimo hai ni hatua moja wapo ya kuelekea kutimiza malengo ya Dira ya Maendeleo ya Zanzibar 2050, ambayo inalenga kuwa na maisha bora, endelevu na yenye ustahmilivu kwa Wazanzibar wote.

Ameyasema hayo kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dkt Hussein Mwinyi katika Tamasha la Kilimo hai la Mwaka 2024 lililofanyika katika Viwanja vya Maonesho ya Kilimo Nanenane Dole Wilaya ya Magharibi “ A” Unguja.

Amesema kuwa kufanyika kwa Tamasha hilo hapa Nchini kunapelekea kuwa na Utalii endelevu, kilimo cha asili, ustahamilivu wa hali ya hewa na kufikia malengo ya Kitaifa na dhamira ya Ulimwengu kwa Maendeleo endelevu.(SDGs)

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amesema dhamira ya kuifanya Zanzibar kuwa kitovu cha Utalii endelevu na kilimo hai imeanza kuzaa matunda ambapo jitihada mbali mbali zinaendelea kuchukuliwa ili kukuza uchumi na kulinda mazingira kwa ajili ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Aidha Mhe.Hemed amesema kilimo hai ni muhimu katika kuhakikisha usalama wa chakula, kuimarisha Afya na kulinda mazingira kwa kuiwezesha jamii kupata vyanzo vipya vya maisha pamoja na kuimarisha ustahmilivu wa mifumo ya kilimo dhidi ya mabadiliko ya Tabianchi.

Sambamba na hayo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeweka kipaombele katika mipango inayounga mkono mbinu mpya za kilimo hai, kuanzia kilimo hadi utengenezaji wa bidhaa za kilimo hai zinazoongeza thamani kwenye uchumi wa Zanzibar.

Naye Waziri wa Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo Zanzibar Mhe. Shamata Shaame Khamis amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Kilimo inajipanga kufanya jitihada za hali ya juu kwa kuwashajihisha wakulima na wananchi kwa ujumla kufanya Kilimo hai chenye kupunguza matumizi ya viatilifu sumu, kulinda mazingira na kuimarisha Afya ya Mlaji.

Mhe. Shamata amesema Wizara ya Kilimo itaendelea kushirikiana na wadau kuhakikisha Tamasha la kilimo hai linaleta Tija kwa kuongezeka kwa Chakula na kukua kwa uchumi kupitia Sekta ya Kilimo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kilimo hai Tanzania Dkt. Mwatima Abdalla Juma amesema Kilimo hai kinazidi kukuwa kwa kasi Duniani ambapo kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo wameweza kuandaa Mkakati wa Kilimo hai Afrika na kutoa nafasi kwa nchi mbali mbali kuja kujifunza Tanzani mbinu na mipango ya kuendeleza Kilimo hai.

Dkt. Mwatima amesema chamgamoto kubwa katika kuendeleza Kilimo hai Tanzania inatokana na kuendeleza matumizi ya Viatilifu sumu katika Kilimo ambavyo vinachangia kuongezeka kwa maradhi mbali mbali nchini, hivyo ameiomba Serikali kusimamia kuondoka kwa viatilifu sumu ili kuendeleza dhana ya kilimo hai nchini.

Aidha Dkt. Mwatima ameiomba serikali kuwapatiwa ruzuku kwa ajili ya kilimo hai ambayo itatumika kwa kuwasaidia vijana kufanya utafiti utakao ibua mbinu mbali mbali za kuimarisha kilimo hai sambamba kuiomba Serikali kuridhia Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar(SUZA) kuwa kitovu cha Kilimo hai hapa Zanzibar.

Mapema Mkurugenzi kutoka Taasisi ya Kilimo hai Zanzibar Ikram Ramadhan soraga amesema lengo la Tamasha la kilimo hai ni kuweka msingi wa maendeleo endelevu pamoja na kukuza uwelewa kwa jamii juu ya kukuza mbinu mpya za kilimo hai Zanzibar.

Soraga amesema Tamasha la Kilimo hai linatoa fursa ya kuwaunganisha pamoja wakulima nchini pamoja na kuwatafutia soko ndani na nje ya nchi kwa lengo la kuimarisha kilimo na kukuza utalii Zanzibar.

Mapema mkamu wa pili wa rais wa zanzibar ametembelea mabanda ya wajasiriamali,taasisi za serikali na binafsi pamoja na kujionesha shughuli mbali mbali zinazofanywa na taasisi hizo.

No comments: