Advertisements

Friday, April 29, 2011

Babu arejea Samunge, tiba kuanza tena leo

Mchungaji Mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Ambilikile Mwasapila
Mussa Juma, Samunge
MCHUNGAJI Mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Ambilikile Mwasapila, maarufu kwa jina la 'Babu,' amerejea Samunge jana na leo anatarajiwa kuendelea kutoa tiba kwa wagonjwa waliokuwa wakimsubiri kwa siku tatu mfululizo.
Mchungaji Mwasapila aliondoka Jumanne jioni na jana alirejea kutoka wilayani Babati, mkoani Manyara alikohudhuria mazishi ya mtoto wake Jackson (43), akiwa anaongozwa na maofisa usalama na polisi.
Mchungaji Mwasapila, aliondoka kijijini Samunge saa 12:20 jioni katika gari la Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro ambalo lilibeba pia maofisa hao wa usalama, polisi na wasaidizi wake.  Awali, kabla ya kuondoka Samunge, watu mbalimbali walikuwa wamejitolea kumsafirisha mchungaji huyo, lakini walizuiwa kutokana na sababu za kiusalama.

 Mamia ya wananchi kutoka nchi jirani za Kenya, Uganda na Burundi, waliopo hapa Samunge, walimpokea Mchungaji Mwasapila kwa furaha kubwa wakitarajia leo kupata kikombe na kuondoka. Raia hao wa nchi jirani na Watanzania kutoka mikoa mbalimbali, wamelazimika kukaa siku mbili Samunge kumsubiri mchungaji Mwasapila arejee na kuendelea na tiba.
 Akizungumza na gazeti hili jana, Msaidizi wa mchungaji Mwasapila, Fredrick Nisajile alisema walimaliza mazishi Babati juzi salama na jana walirejea Samunge wakiwa salama. "Kesho (leo) tunaendelea na tiba."
 "Kesho (leo) tutatoa huduma ili kuwaondoa hawa wananchi tuliowaacha hapa Samunge,"alisema Nisajile.

Waliotibiwa kwa babu
waomba tiba kuboreshwa
Baadhi ya wagonjwa wa magonjwa na Kisukari, Pumu na Saratani ambao wametumia kikombe cha Mchungaji Mwasapila, wameomba tiba hiyo kuboreshwa kitaalamu ili iweze kuwa na mafanikio zaidi.
 Wakizungumza na gazeti hili, baadhi yao walisema walipotumia dawa hiyo walihisi kupona kabisa lakini baada ya muda, wakaanza kuona tena dalili za ugonjwa huo ingawa nguvu yake imepungua.
 John Timoth, mkazi wa Loliondo, aliyekuwa anasumbuliwa na kisukari, alisema alikunywa kikombe hicho mwezi Februari mwaka huu na mwezi huo wote hadi Machi, sukari yake ilikwisha lakini, sasa ameanza kuona tena dalili za ugonjwa huo.
 "Sasa sijui kama nilikiuka masharti ila juzi sukari ilipanda japo sio sana. Binafsi naamini dawa inaponya ila inadumu kwa muda gani mwilini, ndio nadhani uchunguzi unahitajika,"alisema Timoth.
 Anastazia Maziku, ambaye mtoto wake, Isaya Maziku alikuwa anasumbuliwa na Pumu alisema baada ya kumfikisha Samunge na kunywa kikombe, alipona kabisa na kurejea hali ya kawaida, lakini sasa anaona kidogo hali inataka kurejea.
 "Mwanangu karibu mwezi amekuwa vizuri tu. Juzi alipata shida ya kifua ila sio sana,"alisema Maziku.
 Wagonjwa hao, ambao tayari wamepata tiba walishauri watafiti wa afya kushirikiana na mchungaji Mwasapila kuboresha tiba hiyo ili iwe ya kitaalamu zaidi.
 Amir Mshana, alisema kuna wagonjwa ambao wamepona kabisa baada ya kutumia tiba lakini wengine wanaendelea kuumwa japo sio kama ilivyokuwa kabla ya kupata kikombe.
"Dawa nyingi za hospitali ni za asili ya mizizi, majani na vinginevyo, hivyo dawa hii inaonyesha inaponyesha lakini kuna baadhi wanapona moja kwa moja na wengine hali zinajirudia hivyo tafiti ni muhimu hapa" alisema Mshana.
 John Ezekiel, mkazi wa Wasso, Loliondo, alisema tiba hiyo kama ikiboreshwa kitaalamu inaweza kutolewa katika hospitali na maeneo mengine kwa wagonjwa ambao ugonjwa unatishia kurejea.
 Ezekiel alisema inavyoonekana mti wa Mugariga unaotumiwa na mchungaji Mwasapila, unatambuliwa na watafiti kuwa ni tiba, hivyo kama kutakuwa na maafikiano baina ya wataalamu na mchungaji huyo wanaweza kuboresha tiba hiyo.
 "Hii inaonekana ni tiba na kuna mambo ya imani hapa, ila kama inawezekana ikiboreshwa iwekwe hata kwenye chupa au vidonge inaweza kuwafikia wagonjwa wengi zaidi na kutibu,"alisema Ezekiel.
 Ezekiel pia alishauri kama inawezekana, wagonjwa wapewe fursa ya kurudia zaidi ya mara moja kunywa kikombe cha dawa ili waweze kupona kabisa. Hata hivyo, mchungaji Mwasapila, amekuwa akieleza kuwa mti huo unaotumika kama tiba pekee hauwezi kuponya bali nguvu za Mungu ndizo zinatumika sana. 
"Wagonjwa wa kisukari baada ya kunywa kikombe anaweza kuendelea kula vitu vya kawaida bila tatizo," anasema mchungaji Mwasapila. Mamia ya watu bado wanafurika Samunge kupata tiba hiyo ya kikombe ambayo mgonjwa anakunywa kikombe kimoja pekee na haitakiwi kunywa zaidi ya mara moja.

CHANZO:MWANANCHI

No comments: