
Rais Kikwete
RAIS Jakaya Kikwete amewataka Watanzania kuwapuuza wanaotaka kuwagawa Watanzania kwa kisingizio cha dini zao akisema hao hawalitakii mema taifa.Alisema hayo jana alipokuwa akizungumza kwenye Tamasha la Pasaka lililofanyika kwenye Ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam.
"Tusiwasikilize wanaotaka kuwagawa Watanzania kwa dini zao, hawa wanapandikiza mbegu za chuki za udini na kama inawezekana tufanye kila njia kuwaepuka... hata Mwalimu Nyerere alipinga udini akataja dhambi nne akasisitiza dhambi ya udini ni mbaya," alisema.
Alisema dini haijawa kitu cha kutugawa, kutuchonganisha na kutukosanisha kwani zote zilitumika kudai uhuru mwaka 1961 na Mapinduzi ya Zanzibar mnamo mwaka 1962: "Kikubwa Watanzania tusifanye makosa kuvuruga amani, dini zisitumike kutuvuruga...," alisema Kikwete na kuitikiwa Ameen.
Awali, Askofu Onesmo Ndegi wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG), alisema Mungu amempa Rais Kikwete ujasiri wa kuvua gamba na kwamba hatua hiyo ya Rais ni maelekezo yanayotoka kwa Mungu.
"Tunachotaka kuona ni gamba kuvuliwa kikwelikweli na wasaidizi aliowaweka tuna imani watamsadia katika kuweka mambo sawa," alisema kabla ya Rais Kikwete kuwashukuru watu kuunga mkono hatua hiyo ya CCM kujikuvua gamba.
Naye Askofu Samuel Kameta pia wa TAG, alisema wakati umefika kwa kila Mtanzania kuwanyooshea kidole mafisadi na wala rushwa... "Tushirikiane kuwafichua mafisadi, tusiwaonee haya na Tanzania bila ufisadi inawezekana."
CHANZO:MWANANCHI
No comments:
Post a Comment