Advertisements

Monday, June 4, 2012

MBUNGE WA BAHI OMARY BADWEL, AFIKISHWA KIZIMBANI LEO KWA KESI YA KUDAI RUSHWA


 Mbunge wa  Bahi (CCM), Omary Ahmed Badwel, akiwa chini ya ulinzi wakati alipofikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam leo kwa ajili ya kusikiliza kesi inayomkabili. Mbunge huyo alikamatwa jana kwa kile kilichodaiwa kudai na kutaka kupokea Rushwa baada ya kukamilika kwa mitego ya Wana TAKUKURU katika Hoteli ya Peacock iliyopo maeneo ya Mnazi Mmoja jana. 

 Mbunge wa Bahi (CCM), Omary Ahmed Badwel, akiwa chini ya ulinzi wa Polisi wakati akitoka Mahakamani huku baada ya kusomewa mashitaka mawili ya rushwa ya sh. milioni 1, aliyokuwa akiitaka kutoka kwa  Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga, Jonathan Liana.

Wakili wa Mbunge wa Bahi, Omary Ahmed Badwel, Mpare Mpoki (kushoto) akitoka Mahakamani.


Na Mwandishi Wetu, Jijini
MBUNGE wa Jimbo la Bahi (CCM), Omary Ahmed Badwel (43) leo amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kwa kosa la rushwa ya shilingi Milioni moja toka kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga, Jonathan Liana.
Wakili wa Takukuru, Janeth Machullia na Ben Lincoln, walidai mbele ya Hakimu Mkazi Faisal Kahamba, kuwa mshtakiwa huyo anakabiliwa na makosa mawili ya rushwa. 
Wakili Machullia, alidai kuwa kosa la kwanza ni la rushwa kinyume na kifungu cha 15(1) (a) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na.11 ya mwaka 2007, kuwa kati ya Mei 30 na Juni 2 mwaka huu katika maeneo tofauti jijini Dar es Salaam , Badwel, akiwa ni Mbunge wa Bahi na Mjumbe Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) na wakati huo akiwa ni ofisa wa serikali kwa maana ya sheria ya Takukuru, alitenda kosa la kushawishi ili apewe rushwa ya jumla ya Shilingi milioni nane kutoka kwa, Sipora Liana, ili kiasi hicho cha fedha aweze kuwapelekea wajumbe wenzake wa Kamati hiyo ya Bunge ili waweze kuipitisha ripoti ya fedha ya mwaka 2011/2012 ya Halmashauri hiyo.
 Wakili Machullia, alidai shitaka la pili ni kwamba kati ya Juni 2 mwaka huu, katika Hoteli ya Peacock, mshitakiwa akiwa na nyadhifa zake zote hizo alipokea rushwa ya Milioni moja kutoka kwa Liana ili aweze kwenda kuwashawishi wajumbe wa Kamati hiyo ili waweze kuipitisha ripoti ya fedha ya Halmashauri ya Mkuranga huku akijua kufanya hivyo ni kosa.
 Hata hivyo mshitakiwa huyo anayetetewa na wakili wa kujitegemea Mpare Mpoki, alikanusha mashitaka yote na wakili wa Machullia, alidai kuwa upelelezi wa shauri hilo umekamilika.
Kwa upande wake Hakimu Mkazi Kahamba, alisema ili mshitakiwa apate dhamana ni lazima awe na wadhamini wawili wa kuaminika ambao kila mmoja atasaini bondi ya shilingi milioni nne na kusalimisha hati zao za kusafiria mahakamani, sharti ambalo lilitimizwa na mshitakiwa huyo na akapata dhamana. 
Hakimu Kahamba, ameahirisha kesi hiyo hadi Juni 18 mwaka huu, kesi hiyo itakapokuja kwa ajili ya kutajwa na kupangiwa tarehe ya kuja kumsomea maelezo ya awali mshitakiwa huyo.

No comments: