Advertisements

Monday, July 9, 2012

Cheti cha ndoa chazua kizazaa

Mwakilishi mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR), nchini Somalia, Bruno Geddo, alijikuta katika wakati mgumu kutoka kwa mama mzazi wa mmoja wa Watanzania waliowasili nchini akiwa na mke wa Kisomali baada ya kutaka apatiwe cheti cha ndoa.

Mama huyo, Jina Othman Hamad, mkazi wa Chake Chake Pemba, aliishukuru UNHCR kwa kumleta mwanaye wa kiume, Rashid Abdallah Sai, akiwa mzima na mwenye afya njema, lakini akahoji, huyo aliyefuatana naye ni nani.



Alimuuliza mwakilishi huyo wa UNHCR huko Somalia, ambaye ndiye alikuwa kiongozi wa timu ya maafisa wa shirika hilo waliowasindikiza Watanzania hao waliokuwa wakiishi ukimbizini nchini Somalia kuwa huyo mwanamke aliyefuatana na mwanaye ni nani.

“Huyo ni mke wa mtoto wako, ni mkweo na sasa ni mjamzito,” alijibu Geddo.

Mama huyo aliendelea kuhoji: “Hata kama ni mjamzito, nataka kujua kama amemuoa na cheti cha ndoa anacho maana hawa vijana wa siku hizi hawaaminiki.”

Na ndipo Geddo alipokutwa na wakati mgumu, kwani nakala ya cheti hakuwa nayo yeye na kuagiza aulizwe Rashid, ambaye naye alisema: Ni kweli alikabidhiwa lakini hakumbuki wapi aliweka.

"Sitaki nimkufuru Mungu kwa kukubali mambo yasiyoruhusiwa na dini yetu. Sina tatizo na mwanangu kuwa na mke kwani ni haki yake, lakini awe mke halali,” alisema mama huyo.

Baadhi ya Watanzania kutoka visiwani waliokimbilia Somalia kufuatia machafuko ya kisiasa baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2000, walirejea nchini Jumapili iliyopita chini ya uratibu wa (UNHCR), Serikali ya Somalia na Serikali yaTanzania.

Watanzania hao 12 wakiwa na wake wa Kisomali tisa na watoto kadhaa, wakifanya idadi ya watu 38, waliwasili wakiwa kwenye ndege mbili za UNHCR na kupelekwa hoteli ya Bwawani ambako walilala kwa siku moja na Jumamosi walitawanywa kwenye maeneo mbalimbali walikotoka.

 
CHANZO: NIPASHE


No comments: