ANGALIA LIVE NEWS

Sunday, July 22, 2012

SILAHA ZABADILISHWA NA MAGUNIA YA MAHINDI

WAKATI vitendo vya uhalifu vikizidi kuongezeka sehemu mbalimbali nchini, sasa silaha kutoka nchi jirani zinadaiwa kuingia kwa wingi na kuuzwa mitaani na baadhi yake kubadilishwa na mahindi, Mwananchi Jumapili limegundua.
Uchunguzi uliofanywa unaonyesha kuwa, kutokana na kushamiri kwa biashara hiyo ya silaha nchini, bunduki moja aina ya Short Machine Gun (SMG) sasa inauzwa kati ya Sh300,000 hadi Sh500,000, huku bunduki aina ya AK 47 ikiuzwa kwa Sh700,000 hadi Sh1 milioni.
Wakati vijiji kadhaa mkoani Tabora vilipokumbwa na uhaba wa chakula, bunduki aina ya SMG  katika Kijiji cha Usinge wilayani Urambo  zilibadilishwa kwa gunia moja la mahindi, huku AK 47 ilibadilishwa kwa magunia mawili ya mahindi.
Uchunguzi wa muda mrefu uliofanywa mikoa mbalimbali iliyopo mipakani umebaini kuwa, mtandao huo wa uingizaji silaha ni mkubwa na unawashirikisha matajiri na baadhi ya askari polisi wasiokuwa waaminifu.

Silaha hizo huingizwa nchini kupitia mkoani Kigoma, mpakani mwa  Rwanda, Kenya, na Burundi kwa kutumia njia mbalimbali ikiwamo, magari, pikipiki na boti kupitia Ziwa Victoria pamoja na  baiskeli ambapo bunduki hizo hufungwa kama mzigo ya kawaida.
Chanzo kimoja cha uhakika kililiambia Mwananchi Jumapili kuwa eneo la Usinge ndiyo kituo kikuu cha kupokelea silaha kutoka Burundi na Rwanda ambazo husambazwa mikoa mbalimbali nchini.

No comments: