Advertisements

Friday, December 7, 2012

MWANACHAMA WA CHADEMA AMSHUKIA DK. SLAA

MJUMBE wa Mkutano Mkuu wa Chadema, Katibu wa Chadema mkoa wa Mbeya ambaye amesimamishwa kwa kudaiwa kuwa mamluki wa CCM, Edo Mwamalala, akizungumza na Waandishi wa habari leo katika Hotel ya MIC, Ubungo jijini Dar es Salaam, ambapo amedai kwamba Katibu Mkuu wa chama hicho Dk. Willibrod Slaa, ni mamluki namba moja wa CCM kutokana na kumiliki kadi ya CCM kama alivyokiri hiviu karibuni. (Picha na Bashir Nkoromo).

Na Bashir Nkoromo
ZIKIWA ni siku chache baada ya Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa kukiri kuwa bado anamiliki kadi ya uanachama ya CCM, baadhi ya wanachama wa Chama chake wamemjia juu na kumtaka ajiuzulu nyadhifa zake zote mara moja ndani ya chama hicho.

Aidha wanachama hao wamemtaka Mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe na wajumbe wa Mkutano Mkuu wa chama hicho Taifa, kumchukulia hatua za kumwadabisha  ikiwemo kumsimamisha, kwa kile walichokiita kuwa ni kadhia mbaya na undumilakuwili alioonyesha kwa kumiliki kadi za vyama viwili vya siasa.

Hayo yamesemwa na Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Chadema,  Edo Mwamalala, alipozunfumza na waandishi wa habari leo, katika hoteli ya MIC, Ubungo mjini Dar es Salaam.

"Hatua ya Dk. Slaa kukiri tena bila woga wala aibu kwamba anamiliki kadi ya CCM, inamaanisha kwamba ni mwanachama wa vyama viwili vya siasa yaani CCM na Chadema, kwa tafsiri rahisi ni mamluki hai wa CCM ndani ya Chadema", alisema, Mwamalala ambaye amewahi pia kuwa mgombea wa Ubunge wa Chadema jimbo la Kyela katika uchaguzi mkuu uliopita.

Mwamalala ambaye alidai kuna wanachama wengi nyuma yake katika kutoa tamko hilo, alidai Dk. Slaa ni kama askari  wa kukodi ndani ya Jeshi la ukombozi, ndiyo maana amedai kulipwa mshahara mkubwa wa zaidi ya sh. milioni saba kwa mwezi kuwauzia Chadema gharama za ukumbozi.

"Itakumbukwa kwamba katika miaka ya tisini  kulikuwa na viongozi machachari ndani ya upinzani wenye maneno ya kuwaaminisha wananchi, huku wakijitutumua kwamba wamekuja kuleta mabadiliko katika nchi hii, kumbe walikuwa mapandikizi waliokuja kuwaacha Watanzania njia panda, sasa Dk. Slaa ni mfano wa hawa", alisema Mwamalala.

Alisema, kwa kukiri kuwa na kadi ya Chama kingine zaidi ya Chadema,  Dk. Slaa amepoteza sifa ya kuwa mwanachama halali wa Chadema kwa mujibu wa Katiba ya Chama hicho, Sura ya Tano, ibara ya tano, kifungu cha kwanza, kipengele kidogo cha nne.

Alisema, mbali na Katiba,  kwa hilo, Dk. Slaa amedhigirisha kuwa hana uadilifu  wala huruma kwa Watanzania walioweka rehani maisha yao kumuunga mkono katika harakati mbalimbali, kiasi cha baadhi ya vijana kuwa tayari kufukuzwa vyuoni wakitetea sera za Chadema.

" Tunawaomba Watanzania wote  wanaounga mkono Chadema, tuungane kwa pamoja kama kweli tunadhamiria kushika dola 2015, watu ndumilakuwili kama Peter Slaa (Dk. Willibrod Slaa) hawatufai tena hata kidogo", alidai Mwamalala na kuongeza;

"Watu kama Peter Slaa( Dk. Slaa), wapo kwa ajili ya kutumia shida za wananchi kujipatia umaarufu huku wakiendesha maisha yao na kuwaacha wananchi wakiteseka".

Mwamalala alidai kwa vyovyote Dk. Slaa bado ni mwanachama wa CCM, awe hai au mfu, kwa sababu hawezi kuikimbia CCM na kuhamia Chadema kwa uchungu mkubwa kama anavyodai, lakini akaendelea kuhifadhi kadi ya chama kisichomfaa tena.

"Ukihama nyumba ya kupanga huwezi kuhama na ufunguo wa akiba, vitu vikipotea kwa mpangaji mpya watajua ni wewe", alisema, na kufafanua kuwa, Kama ni kweli Dk. Slaa amekwisha hama CCM hana sababu ya kubaki na kadi ya chama hicho isipokuwa tu kama bado ana maslahi nacho.

Mwamalala licha ya kuwa bado ni mwanachama wa Chadema ambaye ni Mjumbe wa mkutano mkuu Taifa, ni miongoni mwa viongozi waliosimamishwa uongozi na Dk. Slaa hivi karibuni kwa madai kuwa ni mamluki wa CCM ndani ya Chadema, ambapo alikuwa Katibu wa Chadema mkoa wa Mbeya.


No comments: