Askofu Mkuu wa Kanisa la Full Gospel Bible Fellowship (FGBF) la jijini Dar es Salaam, Zachary Kakobe.
Kwa mujibu wa chanzo chetu, Kakobe alifikia hatua hiyo baada ya kukumbana na vikwazo mbalimbali katika kutoa huduma ya kiroho, hasa kutoka serikalini.
MANENO YA CHANZO
“Jamani Askofu Kakobe ameamua kuikimbia Bongo. Unajua kwa nini? Amechoshwa na vikwazo vya kila mara, hasa kutoka serikalini, hivyo ameamua kwenda kuishi Canada yeye na familia yake na atakuwa akihubiri Injili kimataifa akiwa huko,” kilisema chanzo hicho bila kuweka wazi vikwazo vya serikali alivyokumbana navyo mtumishi huyo wa Mungu.
KUMBUKUMBU ZA NYUMA
Mwaka 2007, Kakobe alikumbana na kikwazo cha kwanza baada ya serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, kufanya upanuzi wa Barabara ya Sam Nujoma kutoka Mwenge kwenda Ubungo ambapo barabara hiyo ilisababisha sehemu ya maegesho ya magari nje ya kanisa lake lililopo Mwenge, jijini Dar kufutwa.
Maegesho hayo yalikuwa yakisaidia waumini wa kanisa hilo kuegesha magari yao wakati wakiwa kwenye ibada.
Mwaka 2010, Kakobe alikumbana na kisiki kingine, aligombana na serikali kufuatia Shirika la Ugavi wa Umeme Tanzania (Tanesco) kupitisha umeme wenye msongo mkubwa wa KV 132 mbele ya kanisa lake.
Kakobe alilipinga zoezi hilo akidai licha ya madhara kwa waumini wake, umeme huo mkubwa utasumbua mitambo ya Televisheni ya Holiness aliyowaonesha waandishi wa habari ambayo aliifunga kanisani hapo kwa ajili ya kurushia matangazo ya kiroho.
Hata hivyo, serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini chini ya Waziri William Ngeleja ililikataa ombi la mtumishi huyo wa Mungu.
Mwaka 2010, serikali ikatangaza siku ya mafundi wa Tanesco kuanza zoezi la kupitisha nyaya za umeme nje ya kanisa hilo.
Askofu Kakobe akiwa na mkewe Bi. Helen.
KAKOBE AKESHA NJE YA KANISA
Askofu Kakobe na waumini wake waliweka kambi usiku na mchana kanisani hapo huku wakifanya maombi ili zoezi hilo lisifanikiwe.
Ili kudhihirisha malalamiko yao walivaa fulana maalum zilizoandikwa kwa mbele; ‘TANESCO Muogopeni Mungu’ na nyuma zikisomeka ‘Baada ya Richmond Mmegeukia Kanisa’. Lakini nguzo zilisimikwa, nyaya zikapitishwa.
Wakati wa mgogoro huo, Askofu Kakobe alilalamika kwamba utawala wa Rais Jakaya Kikwete unalikandamiza kanisa lake, akaongeza kuwa kama ingekuwa madhehebu mengine ya dini kitendo hicho kisingetokea.
Alibainisha kuwa awali njia hiyo ya umeme, ilikuwa ipite upande wa pili wa barabara mkabala na kanisa hilo, lakini wakazi wengi wa eneo hilo walipinga hata pale walipoahidiwa kufidiwa kwa fedha.
UZINDUZI WA TOVUTI
Baada ya mpango wa kuanzisha Televisheni ya Holiness kufa kwa sababu ya umeme mkubwa kupita nje ya kanisa hilo, Kakobe alianzisha tovuti mbili.
Mwaka jana wakati wa uzinduzi, alisema hatua ya serikali kupitisha umeme katika eneo hilo ilimpa changamoto zaidi katika kuhubiri injili ulimwenguni kwani tovuti hizo za intaneti, zitatazamwa na watu wengi zaidi kuliko ambavyo ingekuwa kwa Televisheni ya Holiness.
PAPARAZI ATINGA KANISANI KUPATA UKWELI
Kufuatia madai hayo yote, Jumapili iliyopita, paparazi wetu alifika kanisani hapo ili kujiridhisha kwa viongozi waliobaki kama kweli Kakobe atakuwa ameamua kutimkia nje ya nchini.
KAKOBE NYUMA YA MIMBARI
Katika hali ya kushangaza, paparazi alimuona mtumishi huyo wa Mungu akiwa nyuma ya meza ya kuwekea Biblia akitoa Neno la Mungu.
Wakati paparazi anaingia, alimsikia Kakobe akisema:
“Mengi yamesemwa kuhusu mimi kuondoka kwenda nje ya nchi, sasa nawaambia rasmi kwamba naondoka, nakwenda nchini Canada, nitakuwa kule katika maisha yangu nikihubiri Neno la Mungu.
“Kwa kuanzia, hivi karibuni nikiwa kule nitakuwa na mkutano mkubwa sana wa injili wa kimataifa. Mkutano huu utafanyika Juni 20 mpaka 23, mwaka huu na dunia itatikisika,” alisema Kakobe.
Akafafanua kuwa mkutano huo utafanyika katika Viwanja vya Tennis Rexell Center ambavyo ni vikubwa na maarufu sana nchini humo.
Hata hivyo, Kakobe hakumtangaza mrithi wa kanisa lake lenye matawi nchini kote. Baadhi ya waumini walilipuka kwa vifijo kuwa kiongozi wao anakwenda kuwa wa kimataifa zaidi.
Wengine walibubujikwa machozi wakidai huenda kuondoka kwa mtumishi huyo ndiyo mwanzo wa kifo cha Kanisa la FGBF.


2 comments:
KAKOBE NAMFAHAM KULIKO YEYOTE YULE ANAYEMFAHAMU NDOTO YAKE NI KUWA JUU TUU SIKU ZOTE IWE KWA KUDHURUMU KUNYANG'ANYA KIUJANJA ILI MRADI ATIMIZE LENGO LAKE KITABIA KAKOBE HASHAURIKI NA HAAMBILIKI KWA SABABU YA UTAMU WA JASHO LA WATU HIVYO VYOTE NI VISINGIZIO TUU MAJI SASA YAMESHAMFIKA SHINGONI KWA KUDHURUMU HAKI ZA WATU KILA ANALOSHIKA LINATEREZA SAWA NA KIFO CHA NYANI NA HUKO PIA HAKUTAMTOSHA LABDA ANGEHAMIA VATICAN ILI AWE KARIBU NA PAPA LABDA KUNGEMSAIDIA. LAKINI MUWEZA ASIYEWEZWA ALISHAAHIDI KATI YA MMDHURUMIWA NA MOLA HUKUNA PAZIA AKIOMBA TUU MOLA HULIPOKEA DUA LAKE, YEYE SI ALIKUWA ANA MIUJIZA SASA VIPI AMESHINDWA KUITUMIA MIUJIZA YAKE HAYO YOTE NI YA DUNIANI BADO YA SIKU YA MALIPO YANAMSUBIRI NI MIMI SULTAN MJUKUU WA MAREHEM USA.
Huu ni upotoshaji mkubwa sana; Ndugu mwogopeni MUNGU,namna yeyote ya kumsema vibaya Mtumishi wa MUNGU ni kujiweka katika laana na kukosa baraka kutoka kwa MUNGU.
Bishop Kakobe, si tapeli, ni mtumishi wa KWELI wa MUNGU ambaye watanzania hawamtambui. Si ajabu hata YESU mwenyewe alikataliwa na wayahudi.
We ndugu Saidi, Bishop Kakobe haumjui na ACHE kuposha watu, maana ukiendelea madhara yatakupata.
Bishop Kakobe, hajawahi kusema hata wakati mmoja kwamba atahamia NJE! "HUO NI UPOTOSHAJI". SI ajabu MAANA Shetani ni BABA wa UONGO.
Kanisa la FGBF haliwezi KUFA kamwe maana MISINGI yake imejengwa juu ya MWAMBA.
BISHOP KAKOBE YUPO NA ATAENDELEA KUWEPO.
"KELEE ZA CHURA HAZIMZUII TEMBO KUNYWA MAJI".
Mungu na awape ROHO ya kumjua yeye na mapenzi yake.
Post a Comment