Advertisements

Tuesday, January 8, 2013

Diwani wa CCM matatani kwa kuchana bendera ya Chadema

NA George RamadhanDiwani wa Kata ya Ngulumungu kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza, Claud Masingija, ameingia matatani baada ya kushusha na kuchana bendera ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Katibu wa Chadema wilaya ya Misungwi, Mussa Mwika, alidai kuwa diwani huyo alifanya tukio hilo Desemba 27, mwaka jana katika tawi moja la Chadema lililopo kijiji cha Chabusongo.

Kwa mujibu wa Mwika, diwani huyo alifanya tukio hilo baada ya kunywa pombe na kulewa ambapo alidai kuwa hataki kuona Chadema kikifanya shughuli zake eneo hilo.

"Nilipata taarifa kwamba huyu diwani siku hiyo alikuwa amelewa pombe, na alipofika katika kijiji cha Chabusongo alishusha bendera yetu na kuichana kisha akavunja mlingoti akidai kwamba hataki kuona Chadema eneo lake,” alisema.

Aliongeza kwamba tayari Chadema kimeripoti tukio hilo katika kituo cha polisi na kufungua jalada la mashtaka namba MIS/RB/1941/2012.

Mkuu wa Polisi wilayani Misungwi, Robert Kwayu, alithibitisha kuwapo kwa tukio hilo.

Kamanda Kwayu alisema diwani huyo anashikiliwa kwa muda kwa mahojiano huku upelelezi ukiendelea.

No comments: