Advertisements

Monday, January 14, 2013

MAKAMU WA RAIS DKT. BILAL AENDESHA KIKAO CHA MUUNGANO MJINI ZANZIBAR LEO

Na Salma Said, ZANZIBAR
WAKATI mjadala juu ya Muungano kati ya Zanzibar na Tanganyika ukishika kasi na kuzusha mtazamo tofauti Kamati ya Pamoja ya kutatua kero za Muungano imefanya kikao chake Zanzibar kujadili mambo kadhaa yanayoleta mgongano katika Muungano huo.

Mkutano huo uliofanyika Hoteli ya Zanzibar Beach Resort uliongozwa na Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk Mohammed Gharib Bilal, Waziri Mkuu Mizengo Pinda na Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ni mfululizo wa mikutano kama hiyo ambayo imewahi kufanyika mara ya mwisho Januari mwaka jana.


Baadhi ya Mawaziri kutoka Tanzania Bara na wa Zanzibar pamoja an wakurugenzi wa idara ambazo zinasimamia masuala yanayolalamikiwa ndani ya Muungano pia wameshiriki na kutoa maelezo yao kuhusiana na namna ya kuondosha kero zilizokuwepo ndani ya Muungano huo.


Kwa kuwa waandishi wa habari hawakuruhusiwa kuingia ndani ya vikao hivyo ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar imetoa taarifa ikielezea kuwa mkutano huo umepiga hatua katika kutatua kero za Muungano lugha ambayo imekuwa ikisikika kila baada ya mikutano kama hiyo.


Waziri wa Nchi Ofisi wa Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mohammed Aboud Mohammed ambaye ndio mwenye dhamana ya masuala ya Muungano kwa Zanzibar alisema miongoni mwa mambo amabyo yamepata ufumbuzi ni kuhusiana na suala la mgawanyo wa misaada kutoka nje pamoja na ajira kwa wazanzibari ndani ya taasisi za Muungano.

Alisema licha ya kuwepo na kasoro bado Muungano ni muhimu kuwepo kutokana na faida kuwa nyingi kwa pande zote mbili na kuahidi serikali zote mbili kuendelea kuwaelimisha wananchi juu ya faida ya kuendelea kwa Muungano huo wa Tanganyika na Zanzibar ambao umeshafikia miaka 49 tokea kuasisiwa kwake.

Hata hivyo kauli ya Mohammed Aboud haijaelezea kwa undani masuala ya uhusiano wa Zanzibar na nchi za nje pamoja na suala la mafuta na gesi asilia ambalo limechukua nafasi kubwa kujadiliwa hivi karibuni.


Kuhusu mafuta na gesi asilia Aboud amesema serikali zote mbili zimefikia hatua nzuri ya kuelekea kuondoa rasilimali hiyo katika orodha ya mambo ya Muungano ili Zanzibar kunufaika kiuchumi na rasilimali hiyo bila ya kuingiliwa na Tanzania Bara.

Wachunguzi wa kisiasa wanaeleza kwamba huu ni wakati mgumu kwa serikali ya Tanzania inapoelekea kuandika katiba mpya ambapo suala la Muungano limeibuka huku baadhi ya wananchi wakitaka uhuru zaidi kwa Zanzibar huku wengine wakipinga hilo.

Baadhi ya wazanzibari wakiongozwa na Maalim Seif Sharif Hamad wanashikilia msimamo wa kutaka mfumo mpya wa Muungano wa Mkataba kutokana na Muungano uliopo kuwa na kasoro nyingi ambazo zinainyima fursa Zanzibar kuendelea kiuchumi na kijamii.


Wajumbe wa Kamati ya pamoja kati Serikali ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wamekutana katika utaratibu wao wa kawaida wa kujadili masuala yanayohusu Muungano ambapo walipitia na kuridhia kumbukumbu za Kikao cha Kamati hiyo kilichofanyika Tarehe 28 Januari mwaka 2012 Mjini Dar es salaam pamoja na kupokea Taarifa ya utekelezaji wa masuala ya Muungano.

Aidha wajumbe hao walipitia na kuridhia mapendekezo kuhusu utaratibu wa muda wa mgao wa ajira kwa Taasisi za Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na kupitia makubaliano ya hoja zilizopatiwa ufumbuzi.

Wakichangia Hoja mbali mbali zilizowasilishwa kwenye Mkutano huo baadhi ya Wajumbe wa Kikao hicho wameelezea kuridhika kwao na hatua zinazochukuliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu na ile ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar chini ya usimamizi wa Wanasheria Wakuu wa Pande zote mbili katika kulishughulikia suala la mafuta na gesi kuondolewa katika mambo ya Muungano.


Walisema hatua ya kuridhiwa na kukubaliwa na Maraisi wa Serikali zote mbili Nchini limewawezesha na kuwapa nguvu wataalamu wa sheria wa pande zote mbili kuangalia namna ya kuandaa utaratibu utakachokidhi mahitaji ya kisheria ya kila upande kuhusu suala hilo.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan alisema mwenendo mzima wa utekelezaji wa masuala yanayoleta kero ndani ya Muungano unakwenda vyema kufuatia mfumo wa vikao vinavyohusisha watendaji wa pande zote mbili.

Waziri Samia alisema hata hivyo yapo baadhi ya masuala ambayo huchukuwa muda mrefu kuyapatia ufumbuzi kutokana na mfumo wa sheria unaohitaji mabadiliko ili kwenda sambamba na makubaliano yaliyoridhiwa.

Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Mizengo Pinda akitoa shukrani zake aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa maadhimisho mazuri ya sherehe za Mapinduzi ya Zanzibar za Mwaka huu zilizokuwa za mfano wa aina yake.

Pinda alisema jamii ingependa kuona sherehe za Mapinduzi za Mwakani kutimia nusu karne zikawa za mafanikio makubwa zaidi na Serikali ya Muungano wa Tanzania inaandaa fikra ya namna ya kuongeza nguvu za ushiriki na mchango wake katika kufanikisha sherehe hizo.


Kwa upande wake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema umahiri wa Mawaziri wa Pande zote mbili katika kikao chao cha sekreterieti umewezesha kamati ya pamoja ya SMT na SMZ kufanikiwa kwa hali ya juu.

Balozi Seif alifahamisha kwamba wajumbe wa kikao hicho wameweza kupokea na kuridhia masuala mbali mbali waliyoyaagiza katika kikao cha mwaka jana ambayo yalikuwa yakileta kero katika masuala ya Muungano.

Akikifunga kIkao Hicho Mwenyekiti wa Kamati ya pamoja na Serikali ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Dr. Mohd Gharib Bilal alishauri Viongozi wa Wizara za Serikali zote mbili kuendelea kushirikiana ili kuleta ufanisi zaidi.

Dr. Bilal alisema ushirikiano huo utakaoshirikisha pia watendaji na wataalamu wa sekta husika ndani ya taasisi zao utasaidia kupunguza na hatimae kuondosha kabisa kero zinazosababisha hitilafu ndani ya mfumo wa Muungano.

Masuala yaliyowasilisha katika kikao hicho cha Kamati ya pamoja ya SMT na SMZ na kupokewa na kuridhiwa na wajumbe hao ni pamoja na uwezo wa SMZ kukopa nje ya Nchi, malalamiko ya wafanyabiashara wa Zanzibar kutozwa kodi mara mbili, kodi ya mapato-pay as you earn { PAYE} pamoja na suala la Mafuta la kutaka kutolewa katika mambo ya Muungano.

Kikao kijacho cha Kamati ya Pamoja ya Serikali ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kinatarajiwa kufanyika mara baada ya Sherehe za mwaka huu za Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na kufanyika pahali zitakapofanyika Sherehe hizo.

No comments: