Sunday, February 10, 2013

Agizo la kuboresha bandari lagonga ukuta

AGIZO la mawaziri wanne wa Serikali ya Rais Jakaya Kikwete kutaka mashine iliyokuwa ikitumika kukagulia mizigo Bandari ya Dar es Salaam ambayo ilipelekwa Bandari ya Tanga miaka miwili iliyopita irejeshwe, limegonga mwamba.

Januari 18, mwaka huu mawaziri hao walifanya ziara fupi Bandari ya Dar es Salaam licha ya mambo mengine, waliagiza mashine hiyo yenye uwezo wa kukagua kontena bila kulifungua irejeshwe mara moja.

Hatua hiyo ilitokana na kuwapo madai kuwa mashine hiyo haifanyika kazi yoyote mkoani Tanga na kwamba, kukosekana kwake Bandari ya Dar es Salaam kunasababisha msongamano wa mizigo.Maagizo hayo yalitolewa na Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe, Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa, Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene baada ya kufanya ziara fupi ya pamoja Bandari ya Dar es Salaam.

Habari zilizopatikana jana, zilieleza kuwa mpaka sasa mashine hiyo haijarejeshwa, kwa maelezo kuwa mashine moja ya aina hiyo iliyopo Bandari ya Dar es Salaam haiwezi kufanya kazi kwa ufanisi kutokana na wingi mizigo.

Dk Mwakyembe alisema baadhi ya maagizo waliyoyatoa yametekelezwa, lakini kuhusu mashine hiyo alihoji: “Unataka kujua kitu kimoja au mafanikio ya maagizo yote tuliyotoa, kama ni hilo watafute watu wa wizarani kwa ufafanuzi zaidi.”

Akitoa ufafanuzi wa suala hilo, Kaimu Meneja wa Bandari ya Tanga, Freddy Liundi alisema mpaka sasa mashine hiyo ipo katika Bandari ya Tanga na kwamba, siyo ya TPA bali ni mali ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

No comments: