Advertisements

Thursday, February 21, 2013

Aliyetoboa bomba la maji Goba aonja joto ya jiwe

Wakazi wa Goba, Wilaya ya Kinondoni, jijini Dar es Salaam, jana walivamia nyumba ya mkazi wa Mbezi Tangibovu na kumfikisha kituo cha polisi baada ya kutoboa bomba la maji ya Kampuni ya Majisafi nja Majitaka Dar es Salaam (Dawasco) na kusababisha wakazi hao kukosa huduma hiyo kwa zaidi ya mwaka mmoja.

Wakazi hao walioonekana kujawa na jazba wakiongozwa na Diwani wa Viti Maalum, Teresia Chiwota, walichukua hatua hiyo kufuatia ukaguzi walioufanya kubaini maji yanapotelea sehemu gani na kutofika katika makazi yao.

Vurugu hizo zilizimwa na askari polisi wa Kituo cha Kawe waliofika katika eneo hilo.

Katika ukaguzi huo, wakazi hao wakiongozwa na askari hao, waliingia katika nyumba ya mkazi huyo, aliyefahamika kwa jina la Imran Rema na kukuta bomba hilo likiwa limekatwa na maji kumwagika ovyo.

Meneja wa Dawasco Kawe, Ramadhani Mtindasi, alisema kumekuwapo na vitendo vya baadhi ya watu kukata bomba la maji na kujiunganishia kiholela na kusababisha wakazi kukosa maji.
Alisema kukamatwa kwa mtu huyo kutakuwa fundisho kwa watu wengine wanaofanya vitendo vya kikatili vya kukata bomba linalotegemewa na wakazi zaidi ya 1,000.

Akizungumza na NIPASHE, mtuhumiwa huyo alisema hafahamu kitu chochote kuhusu kukatwa kwa bomba hilo na wala hajawahi kuona maji yakimwagika katika eneo lake.

Mmoja wa wakazi wa Goba, Solomoni Ruta, aliliambia NIPASHE kuwa hivi karibuni Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe, aliunda kikosi kazi kushughulikia tatizo la ukosekanaji wa maji Goba kikiongozwa na Mkuu wa Wilaya.

Alisema kikosi kazi hicho kilijumuisha viongozi kutoka ofisi ya diwani, Serikali ya Mtaa wa Goba, Dawasco na ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa kutatua katizo hilo.
CHANZO: NIPASHE

No comments: