Friday, February 8, 2013

Anayedaiwa kumteka, kumjeruhi Ulimboka alalamika mahakamani

Dk. Ulimboka.
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, imepiga kalenda kesi inayomkabili raia wa Kenya, Joshua Mulundi (21) ya kumteka na kutaka kumuua Mwenyekiti wa Jumuia ya Madaktari Tanzania, Dk. Stephen Ulimboka, hadi Februari 21, mwaka huu.

Kata hivyo, kabla ya kuahirishwa kesi hiyo, mshtakiwa aliilalamikia mahakama kuchelewa kwa upelelezi kwa madai kuwa anateseka sana mahabusu.

Hakimu Mkazi, Agnes Mchome, alisema kesi hiyo itatajwa Februari 21, mwaka huu na mshtakiwa ataendelea kukaa mahabusu.

Kabla ya kupiga kalenda kesi hiyo, Wakili wa Serikali, Mwanaisha Komba, alidai kuwa upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika na aliomba mahakama kupanga tarehe nyingine ya kutajwa.

Mulundi ambaye ni mkazi wa Murang'a nchini Kenya, anadaiwa kuwa Juni 26, mwaka huu, eneo la Leaders Club, Kimondoni, jijini Dar es Salaam alimteka Dk. Ulimboka.
Katika shtaka la pili, ilidaiwa kuwa siku ya tukio la kwanza, mshtakiwa akiwa katika eneo la Msitu wa Mambwepande, kinyume cha sheria alijaribu kumsababishia kifo Dk. Ulimboka.

Hata hivyo, Hakimu Mchome alisema mshtakiwa hatakiwi kujibu chochote kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza shauri hilo isipokuwa Mahakama Kuu.

CHANZO: NIPASHE

No comments: