ANGALIA LIVE NEWS

Monday, April 22, 2013

TANZANIA YATAKA MALENGO MAPYA YA MAENDELEO ENDELEVU YATOE KIPAUMBELE KUPUNGUZA UMASKINI

Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako Manongi, akifuatilia kwa makini majadiliano ya Mkutano wa pili uliokuwa ukijadili uandaaji wa malengo mpya ya maendeleo endelevu ( SDGs). Mkutano huo ulifanyika kwa siku tatu hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa na ni mmoja wa milolongo ya mikutano ya majadiliano yanayolenga kuunda malengo hayo endelevu ili kuendeleza maudhui ya malengo ya Milenia ambayo mipango yake itafikia tamati Mwaka 2015. Tanzania ni kati ya nchi Thelathini ambazo zimechaguliwa kuongoza majadiliano hayo. Akichangia majadiliano hayo, Balozi Tuvako Manongi, pamoja na mambo mengine alisisitiza kwamba malengo mapya ya maendeleo pamoja na kuzingatia mihimili mitatu ya ajenda za maendeleo yaani uchumi, jamii na mazingiria, suala la kuendeleza mapambano dhidi ya umaskini lazima liwe lengo kuu katika malengo hayo mapya.Nyuma ya Balozi, Ni Afisa Ubalozi Mwandamizi, Bw. Modest Mero.
Na  Mwandishi Maalum

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imependekeza na kushauri kwamba upunguzaji wa umaskini unatakiwa kuwa lengo kuu wakati wa uandaaji wa Malengo ya Mapya ya  Maendeleo Endelevu ( SDGs) kuliko hata ilivyokuwa wakati wa utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia  (MDGs).

Pendekezo hilo  limetolewa na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako  Manongi, wakati wa mkutano wa pili wa kujadili uundaji wa malengo mapya ya maendeleo endelevu.

Mkutano huo wa siku tatu uliomalizika mwishoni wa wiki ulifanyika hapa  Makao Makuu ya UMoja wa Mataifa,  na uliwakutanisha wajumbe wa nchi thelathini wanachama wa umoja wa mataifa,  zikiwamo asasi za kiraia na watalamu mbalimbali.


Tanzania ni miongoni mwa nchi hizo  thelathini ambazo zimechaguliwa   kuongoza majadiliano ya kuunda malengo hayo mapya ya maendeleo endelevu ambayo yatazingatia mihimili mitatu ya maendeleo ambayo ni   ya kiuchumi, kijamii na mazingira. 

“Maoni yetu ( Tanzania ) ni kwamba tunapoandaa malengo mapya ya maendeleo endelevu ni vema malengo haya yakawa mapana zaidi kuliko yale ya  Malengo ya Maendeleo ya Millenia ( MDGs), huku tukihakikisha kwamba upunguzaji wa umaskini unaendelea kuwa  lengo kuu” akasema Balozi Manongi

Na Kusisitiza kwamba ni katika mtizamo huo huo tunatakiwa kuhakikisha kuwa mwelekeo wa  kijamii wa MDGs yaani kutokomeza umaskini,  kuimarisha afya, elimu ya lishe bora na maendeleo ya kijamii  ni masuala yatakayoendelea kupewa umuhimu katika ajenda ya maendeleo baada ya mwaka 2015 huku tukihakikisha kwamba nchi ambazo bado ziko nyuma zinaendelea kusaidiwa.

Aidha Mwakilishi huyo wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, alisisitiza  kuwa  kupoteza  mwelekeo kuhusu mapungufu yaliyobaki wakati wa kufikia  MDGs kutadhoofisha imani katika mchakato wa SDGs na matokeo yake.

Akabainisha kwamba  nchi nyingi duniani  Tanzania ikiwa mojawapo   zimejaribu kutumia miaka kumi na tano iliyopita kuupunguza umaskini kupitia  MDGs. Lakini  bado juhudi  zaidi  zinahitajika za kuendeleza mafanikio ya malengo ya hayo  ili hatimaye kuutokomeza  kabisa umasikini  hasa katika  nchi za kiafrika. 

Balozi Manongi akatoka mfano kwa kusema, wakati wa utekelezaji wa  MDGs, Tanzania imejifunza kuwa ukijenga barabara, shule au kituo cha afya unafungua  fursa kubwa ya  upatikanaji wa masoko, elimu, ujuzi na ustawi wa jamii.

Alisema bado kuna masuala mengi mtambuka yanayohusiana na umasikini moja kwa moja mathalani ukosefu wa nishati mbadala kwa wananchi, maji safi, ajira na utunzaji wa mazingira kwa kuzingatia njia bora ya kuwekeza katika elimu ya mazingira ili rasilimali zake ziweze kuwa endelevu. 

 Mkutano huu wa pili ni mmoja wa milolongo ya mikutano ya majadiliano yanayolenga kuunda malengo hayo endelevu ili kuendeleza maudhui ya malengo ya Milenia ambayo mipango yake itafikia tamati Mwaka 2015. 

Majadiliano haya yataendelea hadi mwaka 2014 hatua kwa hatua ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba ushirikishwaji wa wadau wote unazingatiwa kufuatana na mfumo wa majadiliano hayo ulivyopangwa.

Katika mkutano huu majadiliano  yalihusu   masuala mtambuka na namna ya kuweka malengo mapya yatakayoweza kuondoa umasikini hususan katika nchi masikini na kupunguza ama kutokomeza kabisa umasikini wa njaa na  na umaskini wa kipato  cha dola  moja na nusu ya kimarekani.

No comments: