
Marehemu Levina Mmasi akilishwa chakula na aliyetarajia kumuoa, Kasisi Masawe kwenye hafla ya kuagwa kwake (Send-Off Party) iliyofanyika Jumatano iliyopita.
Handeni. Katika hali isiyokuwa ya kawaida, Bibi Harusi ambaye ni mkazi wa Chanika mjini Handeni, Levina Mmasi (23) amefariki dunia saa moja kabla ya ndoa yake kufungwa katika Kanisa la Katoliki la Roma Wilaya Handeni Jumamosi na hivyo kuilazimu kamati ya maandalizi ya harusi kujigeuza na kuwa ya msiba.
Kifo hicho kilichotokea Jumamosi mwishoni mwa wiki iliyopita, kimekuwa gumzo mjini Handeni huku wananchi wakisema kuwa ni tukio ambalo halijawahi kutokea katika wilaya hiyo.
Msemaji wa familia ya marehemu aliyejitambulisha kwa jina la Firmin Mrimasha, alisema kuwa chanzo cha kifo cha Levina ambaye alijifungua mwanzoni mwa wiki iliyopita,ilikuwa ni homa aliyoipata ghafla siku ya Alhamisi na kupelekwa katika Hospitali ya Wilaya ya Handeni na kukutwa na malaria na kisha kulazwa kwa matibu.
“Huyu bibi harusi alikuwa ametoka kujifungua, alikuwa na mtoto wa kiume kutokana na ujauzito wa miezi saba, ndipo ghafla Alhamisi akapata homa tukampeleka hospitali alikolazwa na baada ya kupata nafuu, aliruhusiwa Ijumaa.
“Baada ya kuruhusiwa akaanza maandalizi ya harusi na Jumamosi ambayo ndiyo siku ya ndoa yake, alijiandaa lakini ilipofika saa 8.05 akafariki dunia akiwa nyumbani akisubiriwa kwenda kanisani kufunga ndoa ambayo ilikuwa ifungwe saa 9.00,” alisema Mrimasha.
Alisema, “Inasikitisha sana ila imeshatokea yaani marehemu amefariki saa moja kabla ya ndoa yake na baada ya kifo hicho, mtoto wake naye alifariki muda mfupi baada ya mama yake kufariki dunia,” alisema Mrimasha.
Akizungumzia mkasa huo, Mwenyekiti wa Kamati ya Harusi hiyo iliyogharimu Sh7.7 milioni, Abdi Kipacha alisema kuwa kwake ni tukio la kwanza kutokea tangu kuzaliwa kwake na kamwe hawezi kulisahau.
“Nilishazipangia kazi kamati za maandalizi, lakini ghafla tukapewa taarifa kuwa bibi harusi amefariki...Hatukuamini, ikabidi niwatangazie wanakamati wenzangu kuwa hakuna tena shughuli, bibi harusi amefariki,” alisema mwenyekiti huyo wa kamati na kuongeza:
“Kitu tulichokuwa tukisubiri ni kuambiwa bibi harusi angefika saa ngapi, lakini ghafla tukapewa taarifa za kifo, ilikuwa ni vigumu kuamini lakini ni kweli imetokea na inasikitisha kwani si jambo la kawaida,” alisema Kipacha.
Kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa na wanandugu ni kuwa marehemu alikuwa Mwalimu wa Shule ya Msingi Nndawa mkoani Lindi na kwamba alikuwa katika kundi la walimu wa ajira mpya ambayo hadi mauti yanamkuta alikuwa hajapokea hata mshahara wake wa awali.
Akizungumzia hali hiyo, Padri aliyekuwa afungishe ndoa hiyo, Max Sabuni wa kanisa hilo Katoliki Handeni alisema: “Nimesikitishwa na tukio hili kwa kuwa halikuwahi kunitokea...Kilichobaki ni wanandugu kuwa watulivu kwa kuwa Mungu amechukua kiumbe wake kwa muda alioupanga.”
Aliwataka ndugu, jamaa na marafiki kuwa na subira katika kipindi hiki cha majonzi.
Naye mume wa marehemu, Kasisi Masawe alisema: “Nimechanganyikiwa sana na hili...Ni jambo ambalo sikulitarajia. Ninamshukuru Mungu kwa yote japokuwa kifo hiki kimeniharibia mipango yangu mingi ya maisha na Levina.
“Nilipanga mengi na yeye, lakini Mungu hakupenda...Nilimpenda sana Levina,leo ameniacha. Amekwenda na mwanangu...Ni pigo kubwa kwa kweli, mke na mtoto kwa wakati mmoja, inauma sana.”
Mwili wa bibi harusi huyo ulisafirishwa jana kupelekwa Machame mkoani Kilimanjaro kwa maziko ambayo yanafanyika leo Jumatano pamoja na mtoto wake ambaye naye alifariki saa chache baada ya mama yake.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tanga, Costantine Massawe alithibitisha kutokea tukio hilo lakini akasema hawezi kuzungumzia kwa undani kwa kuwa ni tukio la kifamilia zaidi.
Mwananchi
6 comments:
Acheni hizo imani, lazima kuna tatizo la uzazi ambao waliukosa kutambua. Mama na mtoto kufariki muda mfupi baada ya kujifungua?????!!!!! Haya ndio matatizo makubwa yanayotukabili, " proper healthcare"!! Taratibu tutafika!InshAllah!!!
Itakuwa tu ni labor complications ambazo hazikuzingatiwa au kutiliwa maanani. labda na stress za harusi kuzaa premature vikachanganyika na malaria yote hayo yamechangia. Hakuna chochote kingine. Inabidi tubadilike jamani. So sad mungu awalaze mahali pema peponi.
Itakuwa tu ni labor complications ambazo hazikuzingatiwa au kutiliwa maanani. labda na stress za harusi kuzaa premature vikachanganyika na malaria yote hayo yamechangia. Hakuna chochote kingine. Inabidi tubadilike jamani. So sad mungu awalaze mahali pema peponi.
Inasikitisha sana sana....lakini kauli ya huyo kamanda mkuu mkoa wa Tanga imeniacha hoi...Kama hao viongozi wana imani hizo bado tutafika kweli?
Hapo huyo mtoto ni preemie...na Tanzania chances za preemie kuishi ni ndogo sana...pili huyo mama kujifungua within a week na kulazwa hospital ati malaria...napinga ..kila kitu Tanzania ni malaria..hawachunguzi zaidi ukiwa na homa tu na wakakupima wanaona kimalaria basi wanasema mlaria...nani asiye na malaria kwenye damu yake Tanzania? Huyo labda alipata infection alipojifungua na hawakugundua ili kuitibu...Juzi tu rafiki yangu kajifungua NY city kapata infection nusu afe..kama angekua hospital ya Tanzania ingekua ameshakuafa...
No Tanzania quality ya healthy care ni very poor hiyo ndio ukweli huyo mwanamke 23 yr old kafa bado mdogo sana....RIP
Tutasema mengi lakini binti Levina ndo mwenyezi Mungu ameisha mchukua. Chamsingi ni kutoa salaam nzuri za rambi rambi na sio kuandika vinginevyo maana ni kweli inauma sana unapoondokewa wewe utaifkiria unavyotaka jamani. Ndo ubinadamu. Roho za marehemu Levina na mtoto zipumzike kwa amani. Amen
both mama na mtoto wanaonekana walipata infection. basi na wabongo kwa kupenda arusi ikawa ndo wanampaka poda tu dada wa watu kumbe anaugulia
Post a Comment