Thursday, November 21, 2013

Magufuli awabana TEMESA

WAZIRI wa Ujenzi, John Magufuli ameagiza Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) kufufua karakana zote zilizokufa nchini.
Akizungumza katika hafla fupi ya kukabidhi mameneja vitendea kazi vyenye thamani ya zaidi sh milioni 800 vya karakana zote nchini zilizopo chini ya TEMESA, alisema anashangazwa na mameneja hao kutoa vibali vya magari ya serikali kwenda kutengenezwa katika gereji binafsi huku wakidai mishahara serikalini.

Magufuli alisema kupatikana kwa vifaa hivyo kuwe mwisho wa kupeleka magari ya serikali kwenye gereji binafsi.

“Kupatikana kwa vifaa hivyo kutakuwa ni changamoto ya kila mhandisi kutekeleza majukumu yake. Ninafahamu mnadai mamilioni katika taasisi za serikali, hii ni changamoto kwetu serikalini. Magari yakiletwa katika karakana zenu lazima kuwe na mikataba, na dereva lazima asaini kitambulisho, ili wakichelewa kuwalipa madeni hayo taasisi hizo zichukuliwe hatua,” alisema Magufuli.

Mtendaji Mkuu wa TEMESA, Injinia Marcellin Magesa, alisema vitendea kazi hivyo vilinunuliwa kwa awamu mbili ambapo awamu ya kwanza ilikuwa ni kwa ajili ya mikoa 10 ambayo ni Geita, Katavi, Njombe, Iringa, Kilimanjaro, Tanga, Shinyanga, Kigoma, Rukwa na Pwani na tayari vifaa hivyo vimeshasambazwa kwenye mikoa husika.

Alitaja baadhi ya vifaa vilivyonunuliwa kwa awamu ya pili vimepelekwa Dar es Salaam (Vingunguti), Dodoma, Tabora, Mbeya, Mtwara, Arusha, Simiyu, Mara na Morogoro.

No comments: