Advertisements

Wednesday, April 23, 2014

Jumuiya ya Kiislamu yaungana na maaskofu kumtetea Warioba

Msemaji wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini, Rajab Katimba akizungumza na waandishi wa habari jana, kuhusu mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na mchakato wa Katiba. Kulia ni Wajumbe, Shaban Ibrahim na Suleiman Abdallah. Picha na Rafael Lubava

Dar es Salaam. Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania imeungana na maaskofu mbalimbali kuwataka wajumbe wa Bunge la Katiba kuheshimu Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa kwa mujibu wa sheria na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Pia, taasisi hiyo imemtaka Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi kujiuzulu nafasi zake zote za uongozi kutokana na kauli waliyodai ya kichochezi, aliyoitoa katika Kanisa la Methodist, Jimbo la Dodoma kuwa ukipitishwa muundo wa serikali tatu, jeshi litachukua nchi kwa sababu itashindwa kuwalipa mishahara.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Msemaji wa Jumuiya na Taasisi hizo, Sheikh Rajab Katimba alilaani kauli kuhusu jeshi na kuwa makanisa yote yatafungwa na nchi itakosa amani kutokana na kupitisha muundo huo wa serikali.
Sheikh Katimba alisema Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa bungeni na aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba imetokana na utafiti na uchambuzi wa maoni ya wananchi wa Tanzania Bara na Visiwani ili kuboresha Muungano kutatua kero zilizodumu kwa miaka 50 sasa.
Msimamo
Jumuiya hiyo iliweka wazi msimamo wake wa kutaka serikali tatu na kutaka maoni ya makundi mbalimbali ndani ya Bunge la Katiba kuheshimiwa.
Mjumbe wa Jumuiya hiyo, Sheikh Ramadhan Sanze pia alisema si ustaarabu kwa kundi moja kuhodhi mchakato kwa masilahi binafsi.
Alisema kukosoa maoni ya waasisi wa Taifa si dhambi kwa sababu wao hawakuwa Mungu kwamba hawakosei, badala yake alipendekeza watu waachwe wazungumze kwa utashi wa matakwa yao juu ya kile kilichowasilishwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
“Nchi hii haithamini mchango wa wataalamu, tumeona Tume ilivyofanya kazi nzuri, leo hii wanatukanwa hadharani, nawashangaa sana viongozi wa nchi hii,” alisema.
Sheikh Sanze alisema miiko na misingi waliyoiweka waasisi wa Taifa inavunjwa na viongozi wenyewe ambao leo wanasema waasisi wanatukanwa kwa kuwa wamependekeza serikali tatu badala ya mbili walizounda waasisi.
“Kulikuwa na utaratibu wa kubadilishana awamu za uongozi katika Serikali ya Muungano, awamu hii rais akitoka Tanzania Bara, ijayo atatoka Zanzibar; hii ndiyo misingi waliyoiweka waasisi, mbona leo haifuatwi? Huu ni unafiki...” alifafanua Sheikh Sanze.
Jumuiya hiyo imewataka wananchi wote kuendelea na mshikamano katika kutengeneza Katiba Mpya yenye maridhiano na itakayoondoa kero zilizodumu kwa zaidi ya miaka 50.
Kuhusu Lukuvi
Sheikh Katimba alisema iwapo Lukuvi alikuwa anasisitiza suala la amani, basi angezungumzia ulipuaji wa mabomu unaotokea Arusha, tena kanisani, jambo ambalo hakugusia kabisa badala yake alikuwa akieneza propaganda za kuwa serikali mbili ndizo bora zaidi.
“Kama Lukuvi ana utafiti alioufanya, kwa nini asiutoe na kuwaeleza Watanzania? Kulikuwa na haja gani ya kutumia mabilioni ya pesa za wananchi kwa jambo ambalo Lukuvi na chama chake walishakuwa na mpango wao?” alihoji Sheikh Katimba. Jumuiya hiyo imepinga kauli nyingine ya Lukuvi kuwa Wazanzibari wanataka serikali yao ili wajitangaze kuwa nchi ya Kiislamu.
“Waislamu wameiita kauli hiyo kuwa ni ya kichochezi yenye lengo la kuwagawa kwa misingi ya kidini,” alisema.
Alisema Taasisi ya Uamsho ambayo Lukuvi aliituhumu kuwa na msimamo mkali, ni taasisi halali iliyosajiliwa na Serikali katika kuendesha shughuli zake. Alisema mpaka sasa Uamsho imeshinda baadhi ya kesi zilizokuwa zinawakabili viongozi wao na nyingine bado zinaendelea mahakamani.
Alihoji kuwa kama Lukuvi alikuwa na ushahidi wa kutosha kwa nini hakuupeleka mahakamani kuthibitisha kuwa kikundi hichi ni tishio kwa amani ya nchi kutokana na misimamo yake mikali.
Jumuiya hiyo imeitaka Serikali kukanusha kwa uwazi na kuwaomba radhi Waislamu na wananchi kwa jumla juu ya kauli ya Lukuvi.

“Tunamtaka Waziri Lukuvi ajiuzulu nafasi zake za uongozi kwa sababu anazitumia vibaya kuchochea chuki. Tunashangaa mpaka sasa Serikali haijachukua hatua yoyote, Rais amwajibishe,” alisema kiongozi huyo.
MWANANCHI

No comments: