Advertisements

Wednesday, April 16, 2014

Moto wa Katiba wavunja `ndoa` ya CCM, CUF Z`bar

Wabunge wao washambuliana vikali
Makamu Mwenyekiti Bunge Maalum la Katiba,Samia Suluhu.

Wajumbe kutoka Zanzibar wameliteka Bunge Maalumu la Katiba kwa kupashana na kuaibishana kila wanapochangia mjadala kuhusu muundo wa Muungano.Kadhalika, mjumbe mmoja kutoka visiwani, alitaka Tanganyika kuilipa Zanzibar fidia kutokana na kuinyonya kwa miaka 50.

Bunge lilianza kusikia matusi ya nguoni juzi, mjumbe Asha Bakari, alipomtusi mwakilishi Ismail Jussa Ladhu, matusi ambayo hayatamkiki, yakiwamo masuala binafsi.Jana wajumbe hao waliendelea kupashana wakisema ‘sisi ni Wazanzibari tuacheni tunajuana’.

Akichangia hoja ya kutaka serikali tatu, mjumbe Haji Hassan Haji, alidai fidia kutoka Tanganyika, kutokana na kuinyonya na kutumia rasilimali zake kupitia Muungano.

Haji, mwakilishi wa CUF (Kiwani), alisema Wazanzibari wote wanataka serikali tatu na wanaotaka mbili wanalinda maslahi yao.

Alisema wanaotetea serikali mbili bungeni, wakiwa kwenye Baraza la Wawakilishi, wanalalamika kuwa mawaziri wa Zanzibar wanawaogopa wa Bara, ndiyo maana wanashindwa kudai haki zao.

“Kuna mmoja alisema kwenye Baraza la Wawakilishi kuwa kama hamuwezi kudai pesa zetu kazi imewashinda wawapeleke wao wakadai. Leo anataka serikali mbili looh,” alisema Haji.

Aliwapasha mawaziri wa Zanzibar wanaotaka serikali mbili kuwa iwapo wanafukuzwa kazi watataka serikali tatu.

Alisema wapo waliocharuka wakati Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, aliposema Zanzibar si nchi bali ni sehemu ya Tanzania, lakini leo anataka serikali mbili.

Aliwahoji kama walitaka serikali mbili inakuwaje wamebadilisha katiba?

“Nawaulizeni CCM Zanzibar ni nani alibadilisha katiba? Ni CUF?” Aliwaambia wanaotaka serikali tatu ni wasaka tonge (wanaotafuta ulaji), wanaotetea maslahi yao.Alitaka kwenye ofisa za Bunge kuwe na mashine za kupima akili kama zilivyo za kukagua usalama.

Aliwaambia wanaotaka serikali mbili wakiwa Dodoma kwenye baraza wanaopinga Muungano.

“Kuna mmoja (Mohamed Raza) alisema tusipokuwa makini na huu Muungano hata vyeti vya ndoa vitatoka Dodoma yuko hapa,” alisema.

Mjumbe mwingine, Mwinyi Haji Makame, alisema Wazanzibari wanataka serikali mbili asiyetaka aondoke.

Kauli yake ilisababisha sauti za kuhoji waende wapi?

Dk. Makame alisema CUF wanaodai serikali tatu wanadanganya kwani wanalilia serikali ya mkataba.

“Wanataka serikali ya ‘nkataba’ hawa. Ajenda yao ni kuvunja Muungano wanataka wawe na kiti Umoja wa Mataifa, waanzishe benki kuu, uraia wao, sarafu pasi na kumiliki na kulinda anga la Zanzibar,” alisema.

Aliongeza: “Hilo haliwezekani serikali ya ‘nkataba’? asoweza aende kwao."

Vijembe zaidi vilirushwa na mjumbe mwingine, Makame Mshimba Mbaruku, aliyesema katiba imewafaa Wazanzibar, kwani sasa inawawezesha kuchimba mafuta na gesi.

Pia wanaruhusiwa kujiunga na Jumuiya ya Nchi za Kiarabu (OIC) na kukopa kwenye mabenki wanapotaka.

“Tuacheni wenyewe Wazanzibari tunajijua,” alisema.

Vijembe zaidi vilitoka kwa mjumbe Mbarouk Salim Ali, alipohoji nani kawapa ujuzi wa kutabiri kuwa serikali tatu zitaleta machafuko.

“Wazanzibari wamechoshwa na muundo huo wa Muungano. Kama kuna anayesema wanataka serikali mbili aende Tibirizi na Kibandamaiti akatangaze,” alisema.

Aliwaambia wanaotetea serikali mbili wanawadanganya wananchi maana wakiwa visiwani wanataja tatu.

Alihoji kuna mikakati gani ya serikali mbili kumaliza matatizo na kero za Muungano?

“Sisi Wazanzibari tumechoka na udhalimu huu na hatuwezi kuendelea nao,” alitishia Ali, lakini alikemewa na Mwenyekiti.

Alisema wajumbe wakiwa barazani wanaongea vingine na leo inashangaza kusikia eti wanataka serikali mbili.

“Kuna mwakilishi alisema wenzetu wa bara wanatudhoofisha kiuchumi, nyie mawaziri mkienda kwenye vikao Bara mnafuata kunywa chai.”

Fakhria Khamis, kwa upande wake aliwarushia mipasho wanaotaka serikali tatu.

“Wanaotaka serikali tatu ni mawakala, hawataki jingine ila Mwarabu arudi,” alisema na kumalizia: “ Zanzibar ni mbili na Mapinduzi daima.”

Wajumbe hao wakati wanazungumza, maneno kama wadaka tonge yalijiri, wengine wakisema CUF hao na kujibu kwa kejeli.

Yuko mjumbe aliyesema kuzomewa si tatizo yatumike hata mavuvuzela kuzomea.

Wengine walisema wanaotaka serikali tatu ndiyo wafuga ndevu wanamtaka Sultani, kwani ndiye mwenye ‘midevu mirefu’

HISIA ZA UZANZIBARI, UTANGANYIKA ZATAWALA
Hisia za Uzanzibar na Utanganyika zimejidhihirisha wazi miongoni mwa baadhi ya wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba, huku baadhi ya wajumbe wakizungumzia suala la Muungano kwa lugha kali.

Jambo hilo lilijidhihirisha wazi kwenye mijadala tangu hatua ya awali kwenye kamati 12 zilizoundwa kujadili sura za rasimu ya katika na kutokana na maoni ya wengi na wachache hadi katika mijadala ya Bunge zima.

Mijadala hiyo inayohusu sura ya kwanza inayoelezea jina la Jamhuri ya Tanzania na ya sita inayohusu muundo wa Muungano, wakati mwingine zimekuwa zikitumika lugha kali, kejeli, mipasho na zenye ukakasi ili kufikisha ujumbe.

Hisia kali zimekuwa zikitolewa zaidi na wajumbe wengi kutoka upande wa Zanzibar hoja yao kuu ikiwa ni madai kuwa Tanganyika inanufaika zaidi na kuinyonya Zanzibar, huku wa upande wa Bara wakijitetea kuwa Zanzibar ndiyo inanufaika zaidi.

Mjumbe wa kwanza kuwasha moto, alikuwa Juma Haji Duni Duni, wakati akisoma maoni ya wachache ya kamati namba 11, ambaye aliwasilisha kwa hisia kali akidai kuwa katika kipindi cha miaka 50 ya Muungano Tanganyika sehemu kubwa ya mapato ya Muungano yanayopatikana hutumika upande wa Tanganyika, huku Zanzibar ikipata kidogo hali inayorudisha nyuma maendeleo yake.

“Matumizi ya Tanganyika nje ya Muungano si chini ya asilimia 70 ya mapato ya Muungano na hii ndiyo maana akaunti ya pamoja haifunguliwi kwa sababu haitakiwi Zanzibar ipate,” alisema.

Kwenye mjadala wa Bunge ulioanza Jumatatu, ambao unaendelea hisia hizo zimejidhihirisha zaidi.Akizungumza baada ya kupewa fursa na Mwenyekiti wa Bunge, Samuel Sitta, baada ya kuomba mwongozo wakati wa mjadala wa sura ya kwanza na ya sita juzi, Mchungaji Christopher Mtikila, alisema wakati umefika Watanganyika kudai nchi yao kupitia katiba mpya, akisema Tanganyika haijafa, bali imefichwa ndani ya Muungano.

Mjumbe mwingine aliyezungumzia kwa hisia kali suala hilo, Ismail Jussa Ladhu, ambaye alidai Tanganganyika imekuwa ikifaidika zaidi na Muungaano kuliko Zanzibar na kwamba, Wazanzibari hawatakubali hali hiyo iendelee.

“Zanzibar imenyang’anywa mamlaka yake. Hatutakubali tena. Mambo ya Muungano yalikuwa ni 11, lakini yameongezwa. Hivyo, kuchukuwa mamlaka ya Zanzibar. Hatukubali, hatukubali,” alisema Jussa kwa hisia kali.

Mjumbe mwingine kutoka Zanzibar, Hija Hassan Hijja, alidai Tanganyika imeinyonya Zanzibar tangu Muungano ulipoanzishwa.
“Tanganyika inatakiwa kuilipa fidia Zanzibar kwa kuinyonya Zanzibar miaka 50 ya Muungano,” alisema wakati akichangia mjadala bungeni jana.

Mjumbe mwingine aliyewasha moto ni Chiku Abwao kutoka Tanzania Bara, ambaye alisema wakati sasa umefika Tanganyika kufufuliwa ili Watanganyika wawe na taifa lao kama Zanzibar.

Huku akizungumza kwa hisia kali, Abwao, ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalumu (Chadema), alisema ni bora Muungano ufe, lakini Tanganyika ibaki, kwani hilo ndiyo suluhisho la matatizo yaliyopo.

“Zanzibar ndiyo wananufaika zaidi na Muungano huu, lakini wanalalamika, tupiganie Tanganyika yetu kwa gharama yoyote, wananchi tunaomba watuunge mkono kwa njia yoyote kupigania kurudi kwa Tanganyika,” alisema Abwao.

Mjumbe mwingine kutoka Tanzania Bara, Hezekiah Oluoch, alisema Tanganyika itapatikana na hata isipopatikana sasa itapatikana baadaye kwa njia yoyote akisema ni hitaji la wananchi.

Hata hivyo, mjumbe mwingine kutoka Zanzibar, Mohamed Aboud Mohamed, alipingana na wajumbe wenzake kutoka Zanzibar kwa kusema kuwa kuzorota kwa visiwa hivyo kiuchumi hakutokani na kunyonywa na Tanganyika.

Badala yake, alisema Zanzibar ndiyo inayonufaika zaidi na Muungano kutokana na udogo wake na kutokuwa na shughuli nyingi za kiuchumi.

Alisema matatizo ya kiuchumi Zanzibar yanasababishwa na kushuka kwa uzalishaji wa zao la karafuu, ambalo lilikuwa likitegemewa sana kuingiza fedha nyingi za kigeni miaka ya nyuma.

“Miaka ya nyuma Zanzibar ilikuwa ikiuza hadi tani 24,000 za karafuu nje, lakini baada ya bei ya zao kushuka katika soko la dunia, sasa tunauza hadi tani tisa,” alisema.

Aboud aliongeza kuwa baada ya kuona zao la karafuu limeshuka serikali ya Zanzibar ikafanya jitihada za kuinua na kutangaza utalii ili kuingiza fedha nyingi za kigeni kukuza uchumi wake.

“Tumefanya jitihada kubwa kuinua sekta ya utalii. Lakini kutokana na vurugu zilizofanywa Zanzibar, ikiwamo matukio ya kuharibu mali za serikali na watu binafsi, uchomaji mali, na baya zaidi umwagiaji watu acid (tindikali), wakiwamo wageni kutoka nje, kumesababisha sekta hii nayo kuzorota, hivyo kuathiri pato la taifa,” alisema.

Naye mjumbe kutoka Tanzania Bara, Ezekiel Maige, alishangazwa na malalamiko ya baadhi ya wajumbe kutoka Zanzibar wanaodai visiwa hivyo vinanyonywa na Tanzania Bara ndani ya Muungano.Alisema Zanzibar ndiyo inayonufaika zaidi na Muungano kutokana na uchumi wa Tanzania Bara kuwa mkubwa, hivyo kusaidia maendeleo ya Zanzibar.

“Hata wajumbe wanaopinga Muungano wanakiri hapa kuwa huduma za afya Zanzibar ni bure, elimu ni bure na barabara zao nyingi wilayani ni za lami tofauti na Tanzania Bara. Tusipotoshe watu hapa kwa sababu hii ni hatari inaweza kuibua hisia mbaya kwa Wabara,” alisema.

Hata hivyo, alipendekeza ili kuondoa malalamiko yaliyopo, suala la Muungano lipelekwe kwa wananchi kupigiwa kura ili waamue aina ya Muungano wanaotaka, halafu suala hilo liwe ni sera ya taifa itakayofuatwa na chama chochote kitakachoingia madarakani kuondoa hisia kuwa muundo fulani ni wa chama fulani.

BUNGE KUAHIRISHWA APRILI 25
Bunge Maalumu la Katiba litaahirishwa Aprili 25, mwaka huu, kwa ajili ya kuruhusu kufanyika kwa Bunge la Bajeti.

Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta, alitangaza bungeni jana wakati akieleza utaratibu wa kuchangia mjadala wa Rasimu ya Katiba katika sura ya kwanza inayozungumzia Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ya sita inayozungumzia muundo wa Muungano.

Mjadala huo ulianza juzi jioni, lakini jana Sitta alitoa ufafanuzi huo kutokana na idadi ya wachangiaji kuongezeka na kuliko muda wa uchangiaji wa siku tatu ambazo zilikuwa zimetengwa.

Sitta alisema kwamba, wajumbe 337 walikuwa wamejiorodhesha kuchangia na kusema kwamba, kutokana na hali hiyo, itabidi kanuni itenguliwe ili kutoa muda zaidi kwa ajili ya kuchangia sura hizo, ambazo zinaonekana kuibeba rasimu.

“Kesho (leo) tutatengua kanuni badala ya siku tuongeze muda,” alisema Sitta na kuongeza kuwa muda wa kuchangia ukiongezwa angalau wajumbe 350 wanaweza kuchangia.

Sasa mjadala kuhusu sura hizo utaendelea hadi Bunge hilo litakaloahirisha ngwe yake ya kwanza Ijuma ya wiki ijayo.

Hata hivyo, alisema ili kutoa fursa kwa wajumbe wengi kuchangia, itabidi kupunguza miongozo.

Sitta alisema Bunge hilo litaahirishwa kesho kwa ajili ya Sikukuu za Pasaka hadi Jumanne na kuendelea na shughuli zake na kuahirishwa kwa ngwe ya kwanza ili kutoa nafasi kwa ajili ya Bunge la Bajeti.

Bunge hilo lililoanza Februari 18, mwaka huu, lilitakiwa kukamilisha kazi ya kujadili rasimu na kupendekeza Katiba mpwa kwa siku 70, ambazo zitamalizika Aprili 28, mwaka huu.

Hata hivyo, kutokana na Bunge hilo kusuasua, Rais Jakaya Kikwete amekubali na kuliongezea siku 30 kukamilisha kazi hiyo.

Uamuzi huo ulitokana na wajumbe kutumia muda mrefu katika kuanza kanuni. Vile vile siku nyingine zilitumika kusajili wajumbe, kuchagua mwenyekiti wa muda, kuchagua mwenyekiti wa kudumu na makamu wake, wajumbe kuapa na uundaji wa kamati 12.

Kazi ya kujadili na kuamua kwa kura sura ya kwanza na ya sita ya rasimu hiyo, ilianza mwishoni mwa Machi na kufuatia uwasilishaji wa ripoti za kamati bungeni ulioanza Alhamisi iliyopita hadi juzi mchana na kufuatia na mjadala jioni.

Kutokana na hali hiyo, Bunge hilo litarejea katika ngwe ya pili baada ya Bunge la Bajeti kuahirishwa.
Imeandikwa na Theodatus Muchunguzi, Abdallah Bawazir.

 
CHANZO: NIPASHE

1 comment:

Anonymous said...

Huu muungano ni feki Itakuwaje tumeungana na serikali ni mbili...hamna nchi yoyote duniani zimeungana na kuwa na serikali mbili. Sasa mnataka ya tatu...mbili Zimewashinda sasa mwataka serikali tatu. Solve the issue and have one serikali and zanzibar iwe mikoa au mkoa. Na wanaosema nani kamnyonya nani kaeni kimya maana nyie ndiyo wezi since no one has valid facts. Vunjeni muungano tujue moja enough with this stuff of nonsense. ..wabunge ni kelele no work done but getting paid
t