Advertisements

Thursday, July 24, 2014

Marekani yafunga Peace Corps Kenya

Shirika la Marekani la kutoa misaada ya matibabu US Peace Corps limetangaza kuwa linasitisha shughuli zake zote nchini Kenya.

Shirika hilo limeamuru kuondolewa kwa wafanyikazi wake wote zaidi ya hamsini nchini humo.

Hatua hiyo inajiri huku kukiwa na tashwishi kuhusu usalama nchini Kenya kufuatia msururu wa mashambulizi yaliyotekelezwa na makundi ya wanamgambo kutoka Somalia Al shabab na washirika wake.

Marekani majuzi ilikuwa imetangaza kupunguzwa kwa idadi ya wafanyikazi katika balozi yake iliyoko mjini Nairobi.

Balozi hiyo ni mojawepo ya maeneo yaliyoshambuliwa mwaka wa 1998 na washirika wa Al Qaeda nchini Kenya.

Aidha ripoti hiyo inawadia siku mbili baada ya Shirika linalosimamia usafiri wa Anga ya Marekani kupiga marufuku safari zote za ndege katika anga ya Kenya.

Hatua ya shirika la US Peace Corps kuwaondoa wafanyikazi wake kutoka Kenya imechukuliwa muda mfupi baada ya wanawake watatu kutiwa nguvuni nchini Marekani na Uholanzi kwa madai ya kutoa ufadhili kwa kundi la

wanamgambo wa kiislam wa al-Shabab nchini Somalia .

Wizara ya sheria nchini Marekani imesema kuwa mwanamke mmoja alitiwa mbaroni alipokuwa nyumbani kwake katika jimbo la Virginia na mwingine alishikwa mjini Washington.

Washukiwa hao wanadaiwa kutuma pesa katika mtandao wa malipo madogo madogo kila mwezi.

Marekani ililitangaza kundi la al-Shaabab kuwa kundi la kigaidi mwaka 2008.

Wizara ya sheria ya Marekani imesema kuwa washukiwa wengine wawili akiwemo Jama Mohammed Fardowsa wamejificha nchini Kenya na Somalia.

Maafisa nchini Kenya wamesema bado hawajapata habari kuhusu kuwepo kwa Bi. Fardowsa nchini humo.

Huku hayo yakiarifiwa Polisi nchini Kenya wanasema kuwa mtalii wa kike ameuwawa kwa kupigwa risasi katika mji wa Mombasa lakini wamesema kuwa bado hawana uhakika iwapo mauaji hayo yanahusiana kwa vyovyote na mashambulizi ya hivi karibuni yaliyotekelezwa na al shabaab.
BBC

No comments: