Advertisements

Monday, September 29, 2014

CUF kuandamana kupinga diwani wao aliyehamia CCM


Chama cha Wananchi (CUF) wilaya ya Tanga kimesisitiza kufanya maandamano ya amani mwanzo mwa wiki hii ya kushinikiza aliyekuwa Diwani wa chama hicho Kata ya Marungu Mohamed Mambeya, ambaye amehamia Chama cha Mapinduzi (CCM) kuacha kuhudhuria vikao vya Baraza la Madiwani kutokana na kupoteza sifa.

Kwa mujibu wa Katiba ya CUF kifungu cha 9(1) G ya mwaka 1992 toleo la 2003,”Mwanachama yeyote atasita kuwa mwanachama ikiwa atakuwa mwanachama wa chama kingine cha siasa.

Diwani wa Kata ya Mwanzange na Mwenyekiti wa CUF Wilaya ya Tanga, Rashid Jumbe, alisema Mambeya ameendelea kuvunja kanuni za Halmashauri kupitia Baraza la Madiwani kwa kutaka kwa lazima kushiriki vikao ambavyo kisheria si mjumbe halali wa vikao hivyo.


Jumbe alisema pamoja na CUF kukaa katika meza ya mazungumzo na Katibu Tawala wa mkoa wa Tanga, Salum Chima, kwa niaba ya Mkuu wa mkoa huo, Chiku Gallawa, pamoja na Meya wa Jiji hilo, Omar Guled, lakini mpaka sasa hakuna mwafaka kutokana na viongozi hao kushindwa kuchukua hatua dhidi ya Mambeya.

“Sasa kwa sababu wao wameshindwa kumsimamisha Mambeya kushiriki vikao vya Baraza na hali wakijua kuwa hana sifa za kuendelea kuwa Diwani, sisi tutaendelea kugoma kushiriki vikao hivyo na hata tutafanya maandamano ya amani na tunawaomba wananchi watuunge mkoano katika hili,” alisisitiza Mwenyekiti huyo.

Jumbe alisisitiza kuendelea na mgomo huo hadi Mambeya atakapoacha kushiriki vikao hivyo kwa kuzingatia kuwa amepoteza sifa baada ya kujiunga na CCM.

Kuhusu barua,Mwenyekiti huyo alisema CUF ilishamwandikia Mkurugenzi wa Jiji la Tanga, Juliana Malange, wakiamini kuwa ndiye mtendaji.

“Kama utaratibu ni kumwandikia Meya basi leo hii, tunamwandikia na kumpelekea, ila wafahamu kuwa wanachofanya ni ujanja ambao hauna maana kwa maendeleo ya wananchi na watambue kama ataendelea kushiriki hatutakoma kufanya mgomo,” alisema Jumbe.

Meya wa Jiji la Tanga, Omar Guled, alisema kuwa kimsingi Madiwani wa CUF wanapaswa kutambua kuwa Mambeya bado hajavuliwa Udiwani na Waziri mwenye dhamana na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) ambaye ni Waziri Mkuu, hivyo wao hawanabudi kuwa wavumilivu wakati suala hilo likishughulikiwa.

“Kwanza wao wenyewe hawajaniletea barua ya uthibitisho ya kumvua Mambeya uanachama ili niweze kuipeleka kwa Waziri Mkuu sasa wao walete hiyo barua na wawe wavumilivu wakati jambo hili likishughulikiwa…kwanza leo wamewanyima haki wananchi ya kupata taarifa ya maendeleo ya Halmashauri yao”,alisema Mstahiki Meya huyo.
CHANZO: NIPASHE

No comments: