Advertisements

Monday, September 29, 2014

MARIE STOPES YAJIVUNIA UHUSIWANO WAKE NA SERIKALI

Balozi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Tuvako Manongi akiwa na Mwakilishi Mkazi wa MARIE STOPES TANZANIA Bi. Ulla E. Muller aliyefika Uwakilishi wa Kudumu na kisha kuwa na mazungumzo na Balozi. Bi. Muller pamoja na kuelezea shughuli za Shirika lake amesema anajivunia na kuridhishwa na ushirikiano uliopo baina ya Serikali na Shirika lake, ushirikiano ambao anasema amekuwa akiuelezea kila alipokutana na wafadhili wanaosaidia miradi mbalimbali nchini Tanzania.
Na   Mwandishi Maalum, New York

Ushirikiano  na uhusiano mzuri baina ya Serikali na  Shirika  lisilo la Kiserikali la Marie Stopes umeliwezesha shirika hilo  kuwafikishia wananchi wengi zaidi huduma mbalimbali  za afya zikiwamo za  uzazi wa mpango
Hayo yameelezwa siku ya  jumatatu na  Mwakilishi Mkazi wa Marie Stopes nchini Tanzania, Bi. Ulla E. Muller wakati  alipomtembelea na  kufanya  mazungumzo na Balozi Tuvako Manongi,  Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa  Tanzania katika Umoja wa Mataifa.
“ Tunafanya kazi kwa karibu sana na serikali na kwa kweli tumekuwa na uhusiano nzuri na ambao  tunajivunia,  uhusiano ambao pia nimekuwa nikiueleza kwa wafadhili wetu mbalimbali   wakiwamo  niliokutana nao  hapa New  York.”Akaeleza 
Kama sehemu ya  kudhihirisha uhusiano huo na serikali amesema Shirika lake kwa nyakati tofauti wamekuwa  wakizitumia   hotuba mbalimbali  za   Mhe. Rais Jakaya Mrisho Kikwete  hususani zile zinazohusu  masuala ya afya bora na uzazi salama.
Akabainisha kuwa matokeo hayo ya ushirikiano na maelewano na serikali,  siyo tu yamewezesha kuwafikia wananchi wengi wanaohitaji huduma mbalimbali za  afya hasa wale walio maeneo yasiyofikika,  bali pia kumelifanya  Shirika lake kuingia katika utekelezaji wa Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa.
Bi.  Muller ambaye kwa mara ya kwanza alifika nchini Tanzania mwaka 1994 na  kurudi tena miaka miwili iliyopita anasema Tanzania inasonga mbele kimaendeleo jambo analosema  ni la kujivunia.
Amesema. “ Nilifika mara ya kwanza mwaka 1994  na kuondoka lakini miaka 20 ya kuifahamu kwangu Tanzania ninaona mabadiliko makubwa kwa nchi hii mabadiliko ambayo kwa mtu au mgeni wa muda mfupi  hawezi kuyaona, lakini mimi nimeona tofauti kubwa ya wakati  huo na sasa”.  
Pamoja na kujikita katika utoaji na usambazaji wa huduma za afya  salama ya uzazi,  uzazi wa mpango na huduma nyinginezo,  Mwakilishi Mkazi, amemwambia  Balozi kuwa    Shirika  lake  pia  linataka kuwekeza zaidi kwa vijana ambao ndio wengi nchini Tanzania.
Amesema    takwimu za idadi ya watu zinaonyesha kuwa vijana ndiyo   wengi zaidi  kuliko kundi jingine la jamii.  Ni kwa sababu hiyo anasema kuna kila sababu ya  kuwekeza katika kuwasaidia vijana ili pamoja na mambo mengine kuongeza kasi ya kuupiga vita umaskini.
Kwa upande wake Balozi Tuvako Manongi amesifu na kushukuru mchango wa Marie Stopes katika kusambaza huduma zake kwa walengwa mbalimbali na kubwa zaidi kwa kufanya kazi  kwa karibu na Serikali.
Balozi amesisitiza  haja na umuhimu wa   Mashirika hayo  yasiyo ya kiserikali  kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia vipaumbele vya Kitaifa kwa kuwa ndivyo vyenye maslahi zaidi kwa watanzania.

No comments: