Advertisements

Wednesday, October 22, 2014

Mahabusi afia mikononi mwa polisi kwa kipigo

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camillius Wambura. Picha na Maktaba

Dar es Salaam. Mahabusi Daniel Alfred katika kituo cha Polisi Urafiki, eneo la Ubungo, amefariki dunia kwa madai ya kupigwa na baadhi ya askari wa kituo hicho.
Alfred aliyekuwa mkazi wa Sinza jijini hapa, alifikishwa kituoni hapo kwa kosa la wizi wa kuaminiwa na kuwekwa mahabusu wakati akisubiri kufikishwa mahakamani juzi(Jumatatu) ili kusomewa mashitaka yake.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camillius Wambura jana alithibitisha kutokea kwa kifo hicho, huku akisema kijana huyo alikuwa akifanya fujo na kuwapiga wenzake wakati akiwa chumba cha mahabusu.
Kamanda Wambura alisema kuwa baada ya kifo chake waliupeleka mwili wake hospitali.
Wambura alisema ripoti ya daktari baada ya uchunguzi, ilionyesha kwamba mahabusi huyo alikuwa mgonjwa.
Shuhuda ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini, alisema alikwenda kituo hapo kumuona ndugu yake lakini alikuta askari wakimpiga.
“Mimi sijui kama alikuwa na matatizo ya kiafya, lakini niliona akipigwa sana na askari wa kituo hicho...yaani inasikitisha sana, jamaa alipigwa kama mpira wa gombania goli, mimi nilikuwa najua kituo cha polisi ndiko usalama wa watuhumiwa unapatikana kumbe hapana ndiyo maana nikaja kuwaeleza nilichokiona,” alisema mtoa habari huyo.
Alisema hata kama kijana huyo alikuwa mgonjwa, anaimani kuwa aliuawa na polisi kwa kipigo kikali.
Mwananchi

No comments: