JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA
YA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA
Simu: 255-22-2114615,
211906-12
Nukushi: 255-22-2116600
|
20 KIVUKONI FRONT,
P.O. BOX 9000,
11466 DAR ES SALAAM,
Tanzania.
|
TAARIFA
KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais
wa Ujerumani, Mhe. Joachim Gauck anatarajiwa kuwasili nchini usiku wa tarehe 02
Februari, 2015 kwa ziara ya kitaifa ya siku tano kwa mwaliko wa Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete.
Mhe. Rais Gauck atapokelewa
rasmi na mwenyeji wake Mhe. Rais Kikwete Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 03
Februari, 2015 na atakagua Gwaride la Heshima na kupigiwa mizinga 21. Wananchi wanaombwa kuwa watulivu wakati
mizinga hii ikipigwa kwani ni salama.
Baada ya mapokezi
hayo, Mhe. Gauck atafanya mazungumzo ya faragha na Rais Kikwete yakifuatiwa na
mazungumzo rasmi. Aidha Marais hao watakutana na Waandishi wa Habari.
Baadaye siku hiyo ya
Februari 03, Mhe. Rais Gauck atakutana na Wafanyabiashara, atatembelea Kanisa
la Kilutheri la Azania Front, atakutana na Wawakilishi wa Taasisi za Kiraia na
kushiriki Dhifa ya Kitaifa itakayoandaliwa na mwenyeji wake Mhe. Rais Kikwete,
Ikulu.
Mhe. Rais Gauck
ambaye ameongozana na Mke wake Bibi Schadt, Viongozi Waandamizi kutoka Serikali
ya Ujerumani na Ujumbe wa Wafanyabiashara tisa, ataondoka Dar es Salaam
kuelekea Zanzibar tarehe 04 Februari, 2015 ambapo atafanya mazungumzo rasmi na
Mhe. Dkt. Ali Mohammed Shein, Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kabla ya
kushiriki kwenye Mkutano wa Kamati ya Pamoja ya Viongozi wa Dini kuhusu Amani.
Rais Gauck pia atakutana na Vijana kutoka Ujerumani wanaojitolea katika
Programu ya Weltwarts Visiwani humo.
Jioni ya Februari 04,
Mhe. Gauck ataondoka Zanzibar kuelekea Mkoani Arusha. Akiwa Mkoani humo siku ya
tarehe 05 Februari, 2015 atatembelea Taasisi mbalimbali za kimataifa ikiwemo
Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, Jumuiya ya Afrika Mashariki
(EAC), na kuhutubia Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA). Mhe. Gauck na
ujumbe wake watatembelea pia Hifadhi ya Wanyama ya Serengeti ambapo atazindua
Kituo kipya cha kudhibiti Ujangili.
Mhe. Rais Gauck anatarajiwa
kumaliza ziara yake hapa nchini tarehe 06 Februari, 2015 na kuondokea Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro
(KIA) kurejea Ujerumani.
Imetolewa
na:
Kitengo
cha Mawasiliano ya Serikali kwa Umma,
Wizara
ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
01
Februari, 2015
No comments:
Post a Comment