Wednesday, March 11, 2015

Giza totoro kura ya maoni katiba mpya.

Mwenyekiti wa Nec, Jaji Damian Lubuva

Baadhi ya wanazuoni, viongozi wa dini, wanasiasa na wanaharakati wamesema hakuna muujiza wowote unaoweza kufanyika hivi sasa kufanikisha kura ya maoni Aprili 30, mwaka huu.

Wamesema kulazimisha kura ya maoni kama ilivyotangazwa ni sawa na ‘kuchochea fujo’, jambo linaloweza kuepukika.

Wakizungumza na NIPASHE kwa nyakati tofauti jana, walisema nchi imegawanyika vipande vipande, huku wengine wakipinga mchakato wote, hivyo kulazimisha kura ni kuendelea kuligawa taifa.

DK. SEMBOJA: TUSILETE FUJO
Mhadhiri Mwandamizi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk. Semboja Hajji, alisema kulazimisha kura ya maoni ni sawa na kuleta fujo.

“Hii iko very clear (wazi kabisa), kwamba muda unapingana na jambo hili. Rasilimali muda ni jambo adimu na mimi sizungumzi siasa, ni hali halisi kwamba, muda hauko na sisi kwa sasa. Kwa ushauri wangu, tusilete fujo kulazimisha jambo hili. Unaweza kulazimisha kufanya jambo zuri, lakini mwisho likaonekana halina maana kabisa,” alisema.

Alisema hata kama kura ya maoni haitafanyika sasa hivi, Watanzania wapo na Katiba ni yao, hivyo hakuna mtu au chama chochote kinachoweza kufanikisha jambo hilo kwa sasa.

Dk. Semboja alisema hakuna sababu ya kufanya haraka kwenye jambo kubwa na zito kwa mustakabali wa nchi kwa miaka mingi ijayo na kusema Watanzania watamkumbuka Rais Jakaya Kikwete kwa uamuzi wake wa busara wa kuanzisha mchakato huo na hivyo ni busara sasa ikaachwa ili ipate muda wa kutosha kujiandaa kabla ya kura ya maoni.

POLEPOLE: TUPO VIPANDE VIPANDE
Aliyekuwa mjumbe wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Humphrey Polepole, alisema serikali haijajiandaa kufanikisha kura ya maoni kwa kuwa nchi imegawanyika na wananchi hawana uelewa wowote kuhusu Katiba inayopendekezwa.

Alisema kabla ya kura ya maoni, taifa linahitaji muda zaidi kujenga muafaka na kuelimishana kuhusu maudhui yaliyomo kwenye Katiba inayopendekezwa na namna ilivyopatikana.

Alisema siyo busara kwa nchi kuendelea na mchakato huo na hata kufika kwenye kura ya maoni ikiwa vipande vipande kama ilivyo sasa na kwamba, muda huo kwa sasa haupo.

“Tangu Katiba inayopendekezwa itolewe, Watanzania hawajaelimishwa vya kutosha juu ya maudhui, wala iliyopelekea kupatikana kwa rasimu hiyo kwamba, ni zao la kitu gani…Katiba hii inapaswa ipimwe na iliyokuwa rasimu ya tume ya Warioba siyo kwa katiba ya mwaka 1977 kama baadhi ya watu wanavyoeleza. Hatuwezi kwenda kwenye kura Aprili 30,” alisema.

Alisema hata elimu kwa umma iliyopaswa kutolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) kwa mujibu wa sheria ya kura ya maoni, bado haijatolewa na kwamba, hata asasi za kiraia, ambazo zilitakiwa kushiriki kutoa elimu hiyo, nazo bado hazijaanza kazi.

Polepole alisema kwa mwenendo wa sasa, kama serikali italazimisha kufanya kura ya maoni Aprili 30, itakuwa bora kura ya maoni, ambayo itazaa bora katiba na siyo katiba bora.

DK. BANA: TUIPE NEC MUDA
Mhadhiri mwingine wa UDSM, Dk. Benson Bana, alisema jambo la msingi linalopaswa kuwekewa mkazo sasa ni uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapigakura na siyo kura ya maoni.

“Kwa maoni yangu, nafikiri tuipe Nec fursa ya kuandikisha. Wameelekeza nguvu yao kwenye daftari, tusubiri wao ndiyo watatutangazia kama kura ipo au haipo. Hilo ndilo jambo la msingi sana kwa sasa,” alisema.

Alisema Nec ndiyo yenye mamlaka kisheria kutangaza tarehe ya kura ya maoni. “Wao ndiyo wana kalenda. Wakiona wana mwelekeleo mzuri, wataamua iwe Aprili 30 au vinginevyo. Sijawasikia wakiweka kura ya maoni kama kipaumbele. Kwa hiyo, tuwaache wafanye kazi yao.”

LHRC: KURA YA MAONI HAIPO
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimesema kura ya maoni ya Katiba inayopendekezwa haitakuwapo endapo vitu vya msingi vitazingatiwa.

Mkurugenzi wa Utetezi na Maboresho ya Sera wa LHRC, Harold Sungusia, alisema mpaka sasa hali inaonyesha kura ya maoni haipo kwa sababu bado mambo mengi yaliyotakiwa kufanyika kabla ya kura hiyo hayajafanyika.

Alisema endapo kura hiyo itafanyika, itakuwa imefanywa kwa kulipua “ya bora liende.”

“Kama suala hili litachukuliwa kiuhalisia, kura ya maoni haipo. Lakini kama litaendeshwa bora liende, inaweza kufanyika,” alisema Sungusia.

Aliongeza: “Hata ukimuuliza mtu wa kawaida kwa haraka haraka kuhusu kama kura ya maoni ipo au haipo, atakwambia haipo kwa sababu ya muda na maandalizi yenyewe. Labda kwa sababu nchi inajiendesha katika utaratibu, ambao inajua yenyewe. Unaweza ukashangaa inafanyika hata kama bora liende.”

Alisema tayari yapo mambo ya wazi yanayoonyesha kura hiyo haiwezi kufanyika, ikiwamo kushindwa kutoa elimu kwa wananchi, ambao wengi bado hawajajiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapigakura na kutokuwapo kwa muda wa kampeni.

JUKATA: KURA APRILI NI MUUJIZA
Makamu Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukata), Hebron Mwakagenda, alisema kuwapo kwa kura ya maoni Aprili 30, mwaka huu ni muujiza.

Alisema hadi sasa hakuna uwezekano wowote wa uandikishwaji kumalizika kabla ya tarehe ambayo imepangwa ya kupiga kura hiyo na haiwezekani kusogeza ratiba mbele kwa sababu itaingilia kalenda ya uchaguzi mkuu.

“Sisi tunadili na masuala hayo, tunajua. Hili suala technically haiwezekani. Labda iwe ni muujiza. Uandikishaji hauwezi kwisha kabla ya 30 Aprili na baada ya hapo huwezi kusogeza mbele kwa sababu itakuwa imeingilia kalenda ya uchaguzi mkuu,” alisema Mwakagenda.

ASKOFU BUNDALA
Askofu wa Kanisa la Pentekoste Kanda ya Kati (Pham), Julisa Bundala, aliitaka serikali kuacha kiini macho cha kuwadanganya Watanzania kuwa kupigia kura Katiba itawezekana kwa mafanikio makubwa.

Alisema muda uliopangwa na serikali kwa ajili ya kuandikisha wapigakura katika daftari lao, hautoshi, hususan kwa unyeti wa suala lenyewe.

“Nimesikia Katiba zimeanza kugawiwa kwa wananchi. Mimi mwenyewe sijaiona hiyo Katiba na nipo mjini. Je, wananchi waliopo vijijini walio wengi wataipata wapi?” alihoji Bundala.

Yahya Sayoni, ambaye ni mkazi wa Kisasa, alishauri Watanzania kufanya subira ili waone miujiza itakayofanywa katika kufanikisha uboreshaji wa Daftari la Wapiga Kura na upigaji kura ya maoni.

TUCTA: HAIWEZEKANI
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama Vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta), Nicholaus Mgaya, alisema kura ya maoni ya Katiba inayopendekezwa, haiwezekani kupigwa Aprili 30, mwaka huu.

Alisema haitawezekana kwa sababu kazi ya kuwaandikisha Watanzania wenye sifa kwenye Daftari la Kudumu la Wapigakura haijakamilika na wala hakuna dalili ya kumalizika kwa wakati uliopangwa.

Aliishauri serikali kujikita kwenye kutoa elimu kwa wapigakura kazi ambayo hadi sasa haijafanyika.

SHEIKH GODIGODI: INAWEZEKANA
Mwenyekiti wa Taasisi ya Tanzania Islamic Peace Foundation, Sheikh Sadiki Godigodi, alisema wanaamini mchakato wa kuipigia kura ya maoni Katiba inayopendekezwa itakayofanyika Aprili 30, itafanyika kama ilivyopangwa licha ya mitazamo tofauti katika jamii.

CUF: HAIWEZEKANI
Chama cha Wananchi (CUF) kimesema kura ya maoni Aprili 30, haiwezekani kutokana na ukweli kuwa uandikishaji wapigakura umekuwa wa kusuasua.

Kaimu Naibu Katibu Mkuu CUF, Shaweji Mketo, alisema hadi sasa uandikishaji umeshindwa kukamilika kwa mkoa wa Njombe na ni sehemu ndogo yenye wapigakura wachache, lakini Nec imetumia muda mrefu.

“Ili kura hiyo ifanyike Aprili 30, labda Nec ituambie kuwa kila Mtanzania atapiga kura bila kujali kama amejiandikisha au la jambo, mbalo ni kinyume cha sheria,” alisema.

Mketo, ambaye ni Mkurugenzi wa Mipango na Uchaguzi wa CUF, alisema hadi sasa Nec haijatangaza kura hiyo itafanyika lini, bali Rais Jakaya Kikwete ndiye alisema kura hiyo itakuwa Aprili 30, jambo ambalo linatia shaka.

Katibu Mkuu wa Baraza la Makanisa ya Kipentekoste, Askofu David Mwasota, alisema kura ya maoni Aprili haiwezekani, hivyo, akamshauri Rais Kikwete kutangaza kuiahirisha, lakini tume iendelee kuboresha daftari kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa Oktoba.

Alisema kazi ya kuandikisha wapigakura haiwezi kumalizika kwa muda uliobakia kwa sababu wananchi wengi wanajitokeza kuandikishwa tofauti na miaka ya nyuma.

“Hivi sasa wananchi wameamka. Wanatambua umuhimu wa kujiandikisha kwa ajili ya kupigakura. Hivyo, kazi ya kuandikisha wapigakura itachukua muda mrefu kumalizika na kuruhusu kufanyika kura ya maoni,” alisema.

ASKOFU SHAO
Askofu mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini, Dk. Martin Shao, alisema hakuna muujiza wowote unaoweza kufanyika kwa sasa na kulifanya taifa lifikie hatamu ya kuamua hatma ya upigaji wa kura ya maoni zaidi ya kuligharimu taifa iwapo kazi hiyo itaharakikishwa ili kukidhi matakwa ya watawala.

“Hakuna muujiza unaoweza kufanyika kwa siku 18, kwa watanzania wote kuandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga kura kwa njia ya mfumo wa BVR zaidi ya serikali kutengua tangazo lake la upigaji wa kura mwezi Aprili mwaka huu…Kama kanisa tulikwishaonyesha shaka yetu kuhusu zoezi hili lakini haraka hii inaweza ikaligharimu taifa,” alisema Dk. Shao.

PADRI ASANTERABI
Padri Patrick Asanterabi wa Jimbo Katoliki la Moshi, aliwashauri watawala kusikia kilio cha Watanzania wanaotaka kujipa muda wa kuamua na kutafakari namna ya kutekeleza mambo yao ili kulinusuru taifa kuingia katika mgawanyiko na kukaribisha hatari ya machafuko.

PROF. MAKUNDI
Gwiji wa Mabadiliko ya Tabia Nchi Duniani, ambaye pia ni Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu nchini Marekani, Profesa Willy Makundi, alisema kilichojitokeza kwa Nec kuonekana haiwezi kuandikisha wapigakura wanaostahili kwa muda uliopangwa ni kutokana na serikali kutokuwa wazi iwapo imeshindwa kuyakabili masuala ya kiufundi waliyoiga kutoka nchi nyingine duniani.

PROF. NKYA
Aliyekuwa Mtaalamu mbobezi wa Masuala ya Biokemia wa Wizara ya Afya na Hospitali ya Rufaa ya KCMC ya mjini Moshi, Profesa Watoki Nkya, alisema kwa haraka Nec inayokwenda nayo ikisukumwa na serikali ni wazi kwamba, haiwezi kufikia malengo ya kuandikisha wapigakura wote kwa muda unaotakiwa.

PROF. BAREGU
Aliyekuwa Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba na Mahadhiri Mwandamizi wa UDSM, Profesa Mwesiga Baregu, alisema serikali haina budi kuifuta tarehe ya upigaji kura ya maoni iliyotangazwa na kuipa Nec muda zaidi wa kuandikisha wapigakura.

“Rais Jakaya Kikwete na serikali yake akubali kwamba, kura ya maoni haiwezekani Aprili. Anapaswa kutengua tarehe iliyotangazwa na kuipa tume fursa zaidi ya kujiandaa na kuandikisha wapigakura wote wanaostahili badala ya kuharakia katiba mpya ipatikane akiwa madarakani…Kama taifa tujipange upya, tuache siasa za vyama, hakuna atakayenufaika taifa likivurugana,” alisema.

Aliongeza: “Kama ni siku ya harusi yako, kwa nini ujibane na ujipe dakika chache za kujiandaa wakati ni siku yako, ambayo hutaisahau duniani kwa kuwa umeandika historia mpya.”

KAIJAGE
Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria mkoa wa Iringa (TLS) na Mhadhiri Mwandamizi wa Kitivo cha Sheria cha Chuo Kikuu cha Ruaha (RUCo), Rwezaura Kaijage, alisema: “Tukubali kwamba, zoezi hili ni total failure (limeshindikana) kwa msingi kwamba, pilot project (mradi wa majaribu uliofanyika) umeshindwa kutoa majibu ya kukidhi vigezo vya uandikishaji.”

Katibu wa Halmashauri Kuu (Nec), Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nape Nnauye, alisema suala la kazi ya kusema kura ya maoni ipo au haipo ni kazi ya Nec, ambayo ina mamlaka ya kisheria ya kusimamia kura hiyo.

Wasiwasi wa kutofanyika kwa kura hiyo umekuja wakati, ambao Nec inaendelea kuboresha daftari la wapigakura katika Mkoa wa Njombe.

Hata hivyo, taarifa ya Nec iliyotolewa kwa vyombo vya habari wiki iliyopita ilieleza kuwa mchakato wa uandikishaji mkoani Njombe utakamilika Aprili 12.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mashine za kielektroniki za Biometric Voters Registration (BVR) zinazotumika katika uandikishaji, zina uwezo wa kuandikisha wapigakura kati ya 80 na 160 kwa siku. Wakati uandikishaji huo ulioanza Februari 23, mwaka huu, ukikamilika, kitendawili kinabaki kwa Nec kama itakamilisha uandikishaji kwa wakati kabla ya Aprili 30, mwaka huu ili kutoa fursa kwa kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa kufanyika.

Taarifa kwa umma iliyotolewa na Nec ilisemabaada ya kukamilika kwa uandikishaji itatoa ratiba ya mikoa mingine kuanza mchakato huo.

Kwa mjibu wa ratiba hiyo, Machi 3 uandikishaji ulianza Kata ya Kitandililo na utamalizika Machi 9. Kata ya Mahongole na Utengule utaanza Machi 11 hadi Machi 17. Machi 16 hadi Aprili 12 uandikishaji utaendelea Wilaya za Njombe, Makete, Ludewa na Wanging’ombe.

Mwenyekiti wa Nec, Jaji Damian Lubuva, amekuwa akikaririwa mara kadhaa akisema ili kura ya maoni iweze kufanyika ni lazima watu wote wenye sifa wawe wameandikishwa.
CHANZO: NIPASHE

2 comments:

Anonymous said...

mi nina wasiwasi na hawa akina godigodi wanaosema inawezekana. wanaufahamu au uelewa wa namna jambo kubwa kama hili la katiba ya NCHI ambalo linahusu taifa zima na vizazi vya baadae linavyotakiwa lifanyike au wanajiongealea bila uelewa. kama hujui ni bora ukae kimya kuliko kutoa maelezo ambayo watu wanakuwa na wasi wasi na uelewa wako.

Anonymous said...

Tatizo kubwa liko kwa viongozi wa CCM na wabunge walioongozwa na Aliyekuwa mwenyekiti wao! Walishapanga mbinu zote na kuandaa katiba kibao kulazimisha ipite hilo daftari la wapiga kura ni libovu kupindukia! Tunaelekea wapi hii ni kiini macho kwa Taifa letu. Kweni makini viongozi na ninyi wataka Ikulu msitupagawishe.