Advertisements

Sunday, March 29, 2015

Hali ya Gwajima bado tete, Polisi, waumini wavutana hospitali inayofaa

Askofu wa Kanisa la Ufufuko na Uzima, Josephat Gwajima akiwa katika Chumba cha Wagonjwa Mahututi (ICU), hospitali ya TMJ ya jijini Dar es Salaam jana.

Wakati hali ya kiongozi wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Askofu Josephat Gwajima, ikiwa tete kwa siku mbili mfululizo, Jeshi la Polisi na waumini wa Askofu huyo wanadaiwa kuvutana hospitali inayofaa kumpa matibabu.

Askofu Gwajima, alizimia ghafla juzi majira ya saa 2: 45 usiku akiwa kwenye chumba cha mahojiano katika Kituo cha Polisi Kati, baada ya kutuhumiwa kumkashifu na kumtukana kiongozi wa kanisa la Katoliki Jimbo kuu la Dar es Salaam, Mwadhama kadinali Polycap Pengo.

Hata hivyo, mara baada ya kutokea tukio hilo, Askofu huyo alichukuliwa akiwa katika hali ya kuzirai na kuanza kuzungushwa katika hospitali tofauti wakati waumini walitaka apelekwe Hospitali ya TMJ Mikocheni, Jeshi la polisi lilitaka apelekwe hospitali za Jeshi na Muhimbili.

Tukio hilo ambalo NIPASHE ililishuhudia, lilianza majira ya saa 3:00 usiku alipopoteza fahamu hadi majira ya saa 8:00 usiku ambapo walikubaliana apelekwe Hospitali ya TMJ ambako anaendelea kupatiwa matibabu.


HALI ILIVYOKUWA POLISI KATI
Baada ya kuwasili kituoni hapo majira ya saa 8:15 alasiri, alikwenda moja kwa moja katika chumba maalumu kilichoandaliwa kwa ajili ya kuhojiwa tuhuma zinazomkabili.

Mahojiano rasmi yalianza majira ya saa 8:45 mchana.
Ilichukua muda wa saa saba ndani ya chumba hicho, na ilipofikia saa 1.05 usiku, hali ya Askofu Gwajima ilibadilika ghafla.

Baadhi ya askari na viongozi wenzake walionekana kujaribu kutumia njia mbalimbali ikiwamo kumpeleka chooni ili kumrudisha hali yake ya kawaida, lakini ilishindikana.

Aliporudi ndani, aliishiwa nguvu na kupoteza fahamu kitu ambacho kilizusha taharuki ndani ya ukumbi huo.

CHANZO CHA KUZIMIA
Taarifa kutoka ndani ya kikao hicho kilieleza, hali yake ilibadilika ghafla baada ya kuanza kuhojiwa kuhusu mali anazomiliki ikiwamo helikopta aliyoinunua hivi karibuni.

Aidha mambo mengine aliyotakiwa kueleza ni uhusiano wake na wanasiasa mashuhuri pamoja na akaunti anazomiliki na njia anazopata pesa.

“Mahojiano yalikwenda vizuri, lakini ilipofikia zamu ya kumhoji mali anazomiliki na ile helikopta aliyonunua, ghafla alibadilika na kuanza kutoka jasho kwa wingi na kuzimia,” kilisema chanzo hicho. Akithibitisha jambo hilo, Mchungaji Yekonia Behanaze alikiri kuwepo kwa maswali hayo, lakini alilalamikia namna alivyokuwa akihojiwa na askari hao kwamba haukufuata hali ya kibinadamu.

“Unajua hawakuwa na misingi mizuri ya kupata maelezo, walihojia mambo mengi sana hata yale tuliyoamini yangekuwapo tuliona hayakuzingatiwa badala yake iliegemea umiliki wa vitu,” alisema Mchungaji Behanaze.

ATEMBEZWA AKIWA AMEZIMIA
Baada ya kuzirai aliondolewa ndani ya chumba hicho ili kumuwahisha hospitali kwa ajili ya kupata matibabu.

Hata hivyo, kulitokea mabishano makali kati ya polisi na viongozi wa kanisa hilo, ambapo upande wa polisi ukitaka kumpeleka katika Hospitali za serikali, viongozi hao waling’ang’ania kwenda Hospitali ya TMJ.
Ilipofika Saa 3:00 usiku, polisi walimchukua na kumuingiza katika gari lenye namba T 215 aina ya Noah na kumpeleka Hospitali ya Kilwa Road inayomilikiwa na jeshi hilo.

Hapo alitibiwa kwa muda wa saa tatu na ilipofika saa 5:08 usiku alichukuliwa na gari la wagonjwa lenye namba DFP 6309 na kupelekwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Msafara wote ulikuwa chini ya ulinzi mkali wa polisi, ambapo wakati akielekea Muhimbili, msafara huo ulikatisha mitaa ya Kurasini, Kariakoo, Faya na kuishia Hospitali ya Muhimbili majira ya saa 5:18, usiku. Hata hivyo, pande mbili hizo kati ya polisi na waumini ziliendelea kushindana kuhusu hospitali inayofaa kumtibia.

Wakiwa Hospitali ya Muhimbili, viongozi wa kanisa hilo ndugu na jamaa wa Gwajima waliendelea kushinikiza kuondolewa hapo ili apelekwe TMJ ambako walidai ndipo alipokuwa daktari wake.

Hata hivyo, hoja hiyo ilipingwa na polisi wakiwaeleza Muhimbili ndiyo Hospitali Kuu na watakubaliana nao endapo madaktari watashauri kuondolewa kwa barua maalum.

Ilipofika majira ya saa 6:00 usiku gari la wagonjwa kutoka Hospitali ya TMJ lenye namba T 786 BYK liliwasili na kukaa tayari kumchukua.
Saa 7:00 usiku Askofu Gwajima alitolewa hospitalini hapo akiwa bado amezirai na kuingizwa katika gari hilo na kumkimbiza Hospitali ya TMJ. Katika msafara huo, magari yalipita mitaa ya Upanga, daraja la Selander, Morocco na hatimaye hospitalini hapo na kulazwa wodi ya wagonjwa mahututi (ICU).

HALI YAKE KWA SASA
Hata hivyo taarifa zilizopatikana kutoka Hospitali ya TMJ, zinaeleza bado hali yake si nzuri kutokana na kutorejewa na fahamu.
Kwa mujibu wa daktari anayempatia matibabu, Dk. Photonatus Mazigo, hali ya mgonjwa wake bado ni mbaya japokuwa kuna dalili ya kupata fahamu taratibu.
“Kwa ujumla hali ya mgonjwa siyo ya kuridhisha, hajazinduka tunachokifanya ni kumpatia tiba ili arejee katika hali yake ya kawaida,” alisema Dk. Mazigo.

DK. SLAA: TUMUACHIE MUNGU
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Wilbroad Slaa, alikwenda kumjulia hali kiongozi huyo na kusema kwa sasa Watanzania wasitafute chanzo, badala yake wamuachie Mungu amsaidie apone haraka.

Alisema hawezi kuzungumzia hali ya Askofu Gwajima kwa kipindi hiki kwa sababu jukumu hilo anaachiwa daktari anayemtibia.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments: