Advertisements

Saturday, April 25, 2015

BASATA - KUSIMAMISHWA KWA SHINDANO LA UREMBO LA MISS TANZANIA KWA MISIMU MIWILI KUKO PALEPALE

Katika siku za hivi karibuni kumekuwa na taarifa kwenye vyombo vya habari na mitandao mbalimbali ya kijamii kwamba shindano la urembo nchini maarufu kwa jina la Miss Tanzania limefunguliwa na Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) na kwamba Kampuni ya Lino International Agency LTD ambayo ni waendeshaji wa shindano hilo imewataka mawakala wake kuanza maandalizi ya shindano hilo.

Taarifa hizo za kufunguliwa shindano hilo zilienda mbali kwa kueleza kwamba mawakala wametumiwa kalenda ya mashindano hayo kwa mwaka huu.

Baraza linapenda kutoa ufafanuzi kama ifuatavyo:

1. Wananchi wapuuze taarifa hizo kwani kusimamishwa kwa shindano la Miss Tanzania bado kuko palepale kama ilivyoelezwa katika barua ya BASATA ya tarehe 22/12/2014 waliyoandikiwa Lino International Agency LTD ambayo pamoja na mambo mengine iliwataka warekebishe kasoro kadhaa zilizojitokeza. Walisimamishwa kwa misimu miwili ya mwaka 2015 na 2016 ili kujipanga upya na kurekebisha kasoro husika.

2. BASATA kama msimamizi na mratibu mkuu wa sekta ya Sanaa nchini ndilo lililolisimamisha shindano hilo baada ya kubaini mapungufu mengi. Kusimamishwa kwa shindano hili ilikuwa ni kwa njia ya kuufahamisha umma na kwa maana hiyo kama shindano litafunguliwa njia hiyo-hiyo ya  kutoa taarifa kwa umma itatumika na si vinginevyo. 

3. BASATA linatoa wito kwa Lino International Agency LTD kutumia muda wake mwingi kufanyia marekebisho mapungufu yaliyojitokeza ili mashindano haya yatakaporejea yawe na mikakati na hadhi kuliko ilivyo sasa. 

4. Aidha, Baraza linawataka wasanii na wadau wote kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo katika kuendesha shughuli za Sanaa sambamba na kufuata mifumo sahihi ya mawasiliano.

Sanaa ni kazi, tuipende na kuithamini

Godfrey Mngereza
KATIBU MTENDAJI

1 comment:

Anonymous said...

Watu wanalia hapo. Ulikuwa radi wa kumaliza njaaa na kupata vidosho maskini!!