Advertisements

Tuesday, May 26, 2015

A-Z MTOTO ALIVYONYONGWA MOROGORO


Marehemu Edyline Barnabas Mafwere enzi za uhai wake.

Na Dustan Shekidele, Morogoro
SIKU tatu baada ya mazishi ya mtoto Edyline Barnabas Mafwere (9), aliyedaiwa kuuawa kwa kunyongwa na mtoto wa baba yake mkubwa, simulizi kamili imepatikana baada ya ndugu jamaa na majirani wa marehemu kuzungumza na gazeti hili.
Judith, msichana anayedaiwa kufanya mauaji hayo ambayo yamegeuka kuwa gumzo mjini hapa, anadaiwa alijaribu kumuua msichana huyo mara ya kwanza Mei 10, mwaka huu, lakini akashindwa baada ya jirani mmoja kumuwahi na kumkuta akiwa amemkaba shingo.

Mwenyekiti mstaafu wa serikali ya mtaa huo, Hasda Msuya alisema akiwa nyumbani kwake, siku hiyo alisikia sauti ya mtoto akilia kwa muda mrefu, alipokwenda katika nyumba hiyo alimkuta Judith akimpiga marehemu huku akiwa amemkaba shingo, lakini akamkemea na kuondoka zake.
Mama mzazi wa Edyline Barnabas Mafwere akilia kwa uchungu.

“Jana (Mei 20, 2015) majira ya saa 12 jioni nilisikia kilio kwa mbali, wakati najiandaa kwenda, Judith akaja kwangu na kunieleza Edyline ameanguka na kutoka damu mdomoni, nilipokwenda nilikuta kweli hali hiyo nikampigia simu mama yake, alipofika tumekuta tayari mtoto amekufa, lakini tukaamua kumpeleka hospitali na madaktari wakathibitisha alishafariki muda mrefu,” alisema mama Msuya.

Mmoja wa wanafamilia hiyo aliyesafiri na wazazi wa mtuhumiwa wa mauaji hayo, alisema haelewi kwa nini baba na mama walishindwa kuhudhuria mazishini licha ya kuwa walishafika Morogoro.

Jeneza lililobeba mwili wa Edyline Barnabas Mafwere likiandaliwa kwa ajili ya mazishi.


“Sisi ni wakazi wa Ukerewe, wazazi wa Judith wamefika jana, wamefikia gesti moja ipo Kichangani wakiwa miongoni mwa watu tisa, lakini sijui sababu ya wao kushindwa kufika mazishini,” alisema mwanafamilia huyo huku akiomba hifadhi ya jina lake.

Baba mzazi wa marehemu, Barnabas Mafwere alisema siku ya tukio alikuwa kazini hivyo hana maelezo marefu, lakini akasema alimchukua mtoto huyo wa kaka yake ili aishi naye kama mwanaye kabla ya kupokea taarifa za kitendo chake cha kumnyonga mwanaye.

Akiongoza lbada ya mazishi Padri John Greyson wa Kanisa la Kolla la Mwili na Damu ya Yesu, aliwaliza watu baada ya kusema marehemu alikuwa miongoni mwa watoto waliokuwa wapokee Ekaristi Takatifu mwishoni mwa mwaka huu.

Wanafunzi wakiuaga mwili wa mpendwa wao Edyline Barnabas Mafwere.

Naye mwakilishi wa Shule ya Kata ya Kolla Hill aliyokuwa akisoma Judith, Mwalimu Neema Lupena alisema ni jambo la kusikitisha kuwa mtuhumiwa wa mauaji ni mwanafunzi wao wa kidato cha kwanza, lakini akasema alipokelewa shuleni hapo licha ya nafasi kujaa kutokana na heshima ya baba yake mdogo.

No comments: