Advertisements

Thursday, August 6, 2015

ZARI ATESEKA SAA 48


HALI ni tete! Nyota wa Muziki wa Kizazi Kipya wa Uganda, Zarina Hassan ‘Zari’ (pichani) ambaye ni mpenzi wa Mbongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond’ anasemekana kuteseka kwa saa arobaini na nane (siku mbili) akisubiri kujifungua kutoka katika ujauzito wake, Amani lina mchapo wote.

Kwa mujibu wa chanzo cha ndani kutoka katika familia ya Diamond, Jumatatu na Jumanne zilikuwa siku mbaya kwa Zari baada ya hali yake kuwa tete kwa maumivu makali hali iliyoashiria kwamba, sekunde za kupata uchungu wa kuzaa zilishafika.

SIKU ZA MATARAJIO

Taarifa za awali zilidai kuwa, Jumamosi ya Agosti Mosi, mwaka huu ndiyo ilikuwa siku ya makadirio ya Zari kujifungua lakini siku hiyo jua likachomoza mpaka likazama, kukakucha. Siku ya pili ikaingia, Jumapili, ikafika Jumatatu, Zari akiwa bado hajajaliwa kupata mtoto ndipo hali ilipobadilika.

DIAMOND AMKIMBIZA HOSPITALI

“Hali ilikuwa mbaya sana. Ikabidi Diamond amkimbize kliniki anayotumia Zari iliyopo Masaki (Amani linaijua ni Hospitali ya Ami, Masaki, Dar),” kilisema chanzo hicho huku kikiomba hifadhi ya jina lake.

DAKTARI ATIA NENO

Habari zaidi zinadai kuwa, daktari wa Zari alimwambia Diamond kuwa, itabidi mjamzito huyo akomalie mazoezi, hasa yale ya kujaza pumzi kifuani ili aweze kujifungua kirahisi na ndivyo alivyofanya Zari.

HALI YAKE

“Ilibidi Zari arudishwe nyumbani lakini hali yake kiafya ikiwa ya kusuasua kwani hayuko kawaida. Si unajua wajawazito. Wakianza maumivu ya tumbo (uchungu) wanakuwa kwenye mateso makubwa. Hali yake ni ya kumtazamia sana.” Chanzo.

MAMA WA ZARI ATUA DAR

Habari zilizolifikia gazeti hili Jumanne iliyopita zilisema kuwa, mama wa Zari, Halima Hassan tayari yupo Dar nyumbani kwa Diamond baada ya hali ya Zari kuwa tete.

“Mama Zari ametua Dar tayari kwa dharura. Kaja tayari kwa kumsaidia mama Diamond (Sanura Kasim) katika harakati za kuhakikisha mzazi huyo (Zari) anahudumiwa sawasawa,” kiliongeza chanzo.

HOFU YA KUFICHA HABARI

Wakati hayo yakiendelea, tayari kuna hofu kwamba, habari za Zari kujifungua zinadaiwa haziwezi kuwafikia mashabiki moja kwa moja ili kumuepusha mtoto na watu wabaya.

DIAMOND AZUNGUMZA

Amani lilipata nafasi ya kuzungumza na Diamond juzi ambapo aliulizwa kuhusu Zari kujifungua.

“Teh! Teh! Nyie watu kwa kutafuta habari bwana…Teh! Teh!”

KUHUSU USIRI

Diamond alisema hakuna usiri wowote wa Zari kujifungua kwani ni jambo la heri kabisa.

“Usiri wa nini sasa? Kwani kujifungua ni jambo baya? Mbona ni tukio jema tu. Hakuna usiri wowote ule,” alisema Diamond.
CREDIT:GPL

No comments: