Advertisements

Sunday, November 29, 2015

Mwanaume afanya mauaji ya watu watatu kikatili


Polisi mkoani Ruvuma inamshikilia Amani Hyera (42), mkazi wa kijiji cha Kikunja wilayani Songea kwa tuhuma za kuwaua watu watatu.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma, Mihayo Msikhela, alisema tukio hilo limetokea juzi.

Alisema siku ya tukio Mkuu wa polisi wa Wilaya ya Songea akiwa ofisini kwake, alipokea taarifa ya mauaji ya watu watatu.

Alisema anayedaiwa kufanya mauaji hayo ni Hyera, mkazi wa kijiji cha Kikunja.


Alisema mtu huyo anadaiwa kuwaua watoto wawili na mama yao kwa kuwakatakata mapanga kwa kile kilichosadikiwa kuwa ni wivu wa mapenzi.

Alisema baada ya kufanya mauaji hayo, alijaribu kujiua kwa kujikata na panga shingoni, lakini hakufanikiwa kutokana na wananchi kufika kwenye eneo hilo la tukio na kumdhibiti.

Kamanda Msikhela alisema mtuhumiwa anaendelea kupata matibabu na taratibu za kisheria zinafuata mara tu baada ya afya yake kuimarika.

Aliwataja waliouawa katika tukio hilo kuwa ni Ester Kadege (48), ambaye ni mama mzazi wa watoto waliouawa, Edson Msuha (6) na Kazed Kadege (13).


Alisema marehemu Ester alikuwa na watoto wawili ambao walizaliwa kwa baba tofauti ambapo uchunguzi wa awali wa polisi umebaini kuwa mtuhumiwa katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita alikuwa na mahusiano ya kimapenzi na Ester na baadaye waliachana kufuatia Ester kudai kuwa ameokoka na kwamba hataki tena masuala ya kimapenzi.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments: