ANGALIA LIVE NEWS

Saturday, December 19, 2015

Magufuli amwagiza Mahiga kutatua mzozo wa Burundi



Rais John Magufuli      
Dar es Salaam, Tanzania. Rais John Magufuli amemwagiza Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Kikanda na Mambo ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Balozi Dk Augustine Mahiga kuanza kushughulikia mgogoro wa Burundi na ametaka kazi hiyo afanye kwa kushirikiana na waziri wengine kutoka Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).

Huu utakuwa mtihani wake wa kwanza kwa Balozi Mahiga ambaye aliapishwa hivi karibuni kwenye wadhifa huo baada ya kuteuliwa na Rais kuwa mbunge. Balozi Mahiga aliliambia gazeti moja akisema kuwa, ameagizwa kushughulikia kiini cha mzozo huo na tayari wakati wowote alitarajiwa kuwasili Bujumbura kuanza mazungumzo.

Hata hivyo, alitarajiwa kuwasili kwanza mjini Arusha kwa ajili ya majadiliano na Katibu Mkuu wa EAC, Dk Richard Sezibera na baadaye kuweka mikakati ya pamoja ya namna ya kushughulikia mzozo huo. Tanzania ndiye mwenyekiti wa EAC.

Wakati hali ya wasiwasi ikiendelea kujitokeza Burundi, ripoti zinasema kuwa zaidi ya raia 1O0,000 wamewasili nchini kwa ajili ya kuomba hifadhi tangu mzozo huo ulipoanza Aprili mwaka huu.

Wakati Tanzania ikianzisha juhudi mpya kuhusiana na mzozo huo, kuna ripoti kuwa Umoja wa Afrika (AU) umeanza kujadili uwezekano wa kutumwa jeshi la Afrika Mashariki nchini humo kwa lengo la kuzima ghasia na machafuko yanayotishia kuitumbukiza nchi hiyo kwenye vita vya ndani.

Baraza la Usalama na Amani la Umoja wa Afrika limesema hali ya Burundi ni mbaya na kwamba hatua za dharura zinahitaji kuchukuliwa ili kuepusha nchi hiyo kutumbukia kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Kamishna Mkuu wa baraza hilo, Ismail Chergui ameandika kwenye ukurasa wake wa Twitter akisema kuwa mauaji nchini Burundi ni lazima yakomeshwe. Baraza hilo la AU limefanya kikao cha dharura kujadili kadhia ya Burundi na pendekezo la kutumiwa kikosi maalumu kinachojulikana kama ‘East Africa Standby Force’ kwa ajili ya kudhibiti hali ya mambo katika nchi hiyo limetolewa. Kikosi hicho kiliundwa mwaka 2003 na kinajumuisha nchi za Kenya, Burundi, Comoros, Djibouti, Ethiopia, Rwanda, Ushelisheli, Somalia, Sudan na Uganda.

Huku hayo yakijiri, Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa amewalaumu viongozi wa Burundi kwa kuchochea ghasia na machafuko nchini humo na kulitaka Baraza la Usalama la umoja huo kuwawekea vikwazo vya usafiri viongozi kama njia moja ya kuwashinikiza wakomeshe ghasia hizo.
Mwananchi

6 comments:

Anonymous said...

Kumbe anaweza kuagiza kuangaliwa utatuzi wa migogoro ya nchi zingine lakini hawezi kuelekeza nia zake katika utatuzi wa matatizo ya amani yaliyopo Zanzibar?? Mbona anajiweka doa kidogo hapa. Hii kama vile matatizo ya Zanzibar iko nje ya uwezo wako Mzee wetu JPM. Tafadhali tafuta suluhisho la siasa Zanzibar kwanza achana na Burundi kwa sasa hivi kwani sio sehemu ya Jamhuri ya Muungano. Toa kibanzi jichoni mwako kwanza. Peace and May God Bless TZ.

Anonymous said...

very good in ordering but why dont you do the same and fix zanzibar issue as it shows sign of poor leadership.

Anonymous said...

Aliekuambia kuwa matatizo ya Zanzibar hayashughulikiwi ni nani?Unachotakataka kufahamu labda ni matokeo ya mazungumzo ambayo yamekuwa yakiendelea.
Maisha hayawezi kusimama kwasababu ya issue ya Zanzibar. Zanzibar mlilikoroga,mazungumzo yanaendea na solution itapatikana in due time. Don't go ahead of yourself.

Anonymous said...

Zanzibar je?

Anonymous said...

Ni lini yatatatuliwa?? Nyie CCM acheni uswahili wa Kikwete. You are just buying time here na kuwadanganya wananchi.

Anonymous said...

Wee CUF ukitaka kujua progress ya mazungumzo muulize kiongozi wako Seif Sharifu usituchoshe hapa..