Wednesday, January 13, 2016

UZINDUZI WA MAADHIMISHO YA CCM KUFANYIKA ZANZIBAR KILELE KUITIKISA SINGIDA

Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi Ndugu Nape Nnauye akizungumza na Baadhi ya Waandishi wa habari,mapema leo kuhusiana na uzinduzi wa maadhimisho ya sherehe za chama hicho pamoja na kilele chake ambacho kinatarajiwa kufanyika mkoani Singida,Mkutano huo umefanyika kwenye ofisi ndogo za chama hicho zilizopo mtaa wa Lumumba,jijini Dar .
 Mmoja wa Wanahabari akiuliza swali.

 Baadhi ya Wanahabari kutoka vyombo mbalimbali wakifuatilia mkutano huo. PICHA NA MICHUZI JR-MMG.

Na Chalila Kibuda,Globu ya Jamii.
CHAMA cha Mapinduzi (CCM) kinatarajia kuadhimisha miaka 39 ya kuzaliwa kwake na kumbukumbu hiyo itazinduliwa  Januari 31,Unguja –Zanzibar chini ya mgeni rasmi  Makamu Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati akitangaza maadhimisho ya chama hicho,Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa,Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye amesema baada ya uzinduzi wa maadhimisho hayo Zanzibara,kilele chake kitakuwa mkoani Singida ambako zitafanyika kazi mbalimbali ikiwemo na ya kuingiza wanachama wapya, kufanya kazi za kujiletea maendeleo kwa kujenga madarasa,kupanda miti,pamoja na kufanya kazi za usafi .
Amesema viongozi wa kitaifa na baadhi ya wajumbe wa Kamati Kuu watapangiwa shughuli za ujenzi wa chama na taifa kwa ujumla katika wilaya za Mkoa wa Singida siku tatu kabla ya kilele ya maadhimisho ambayo yatafanyika mkoani Singida.
Nape amesema mgeni rasmi katika kilele cha maadhimisho hayo yatakayofanyika Februari 6 mkoani  Singida,anatarajiwa kuwa ni Mwenyekiti wa Chama hicho,Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne,Dk.Jakaya Kikwete.
Kauli Mbiu ya maadhimisho kwa Chama hicho kwa mwaka huu kimetajwa kuwa ni “Sasa kazi,Kujenga Nchi na  Kukijenga Chama”.Maadhimisho ya CCM hufanyika kila Februari 5 ikiwa ni kumbukumbu ya kuzaliwa kwa CCM Februari 5 ,1977 iliyotokana kuungana kwa ASP na Tanu.

No comments: